Uislamu na Mtindo wa Maisha
mada kuu ikiwa ni kuhusu suala lal afya na siha. Miongoni mwa mambo
muhimu katika mtindo wa maisha ni kutiliwa maanani masuala ya afya na
siha. Hii ni kutokana na kwamba hapana shaka kuwa siha na afya vina
taathira kubwa katika mtindo wa mtu wa maisha. Katika upande mwingine
mtindo wa maisha wa mtu yeyete una nafasi muhimu katika afya na siha ya
mwili wake. Katika maisha yake ya kila siku mwanadamu anahitaji mwili
wenye afya na siha na suala hilo ndilo linalomwezesha kufanya kazi na
shuguli zake nyingine za kimaada na kimaanawi. Uzima na siha ni miongoni
mwa neema kubwa za Mwenyezi Mungu na aghlabu ya watu hutambua umuhimu
wa neema hiyo baada ya kuondokewa nayo. Imam Swadiq (as) amesema: Afya
na siha ni miongoni mwa neema zilizojificha, inapokuwapo husahauliwa, na
inapoondoka ndipo inapokumbukwa." Vilevile babu yake, mtukufu Mtume
Muhammad (saw) anasema: Wanadamu daima hukufuru neema mbili, neema ya
afya na neema ya usalama."
Hapana shaka kuwa iwapo mwanadamu hatakuwa na siha na afya hawezi
kufanya kazi yoyote yenye maana na wakati huo atahitajia watu wengine
kufanya kazi zake za kila siku. Ni kwa sababu hiyo ndiyo maana pamoja na
kusisitiza sana juu ya siha na uzima wa roho na fikra, Uislamu pia
unatilia mkazo uzima, afya na siha ya mwili.
Hata hivyo tunapaswa kuelewa kuwa sisitizo la Uislamu juu ya afya na
siha ya mwili halina maana ya kile kinachoonekana katika dunia ya sasa
kwa maana ya kulea na kutunisha mwili na misuli. Kama tunavyojua, neema
zote ambazo Mwenyezi Mungu amemtunuku mwanadamu ikiwemo ya afya na siha
ni kwa ajili ya kuzitumia katika njia ya kufikia saada ya dunia na
Akhera. Imam wa Wachamungu, Ali bin Abi Twalib (as) anasema: Zaka ya
elimu ni kuisambaza, zaka ya urembo ni kujisitiri, zaka ya mwili ni
jihadi na kufunga saumu na zaka ya afya na siha ni kufanya jitihada
katika kumtii Mwenyezi Mungu.
Kwa kawaida mtu asiyekuwa na maradhi ya kimwili huitwa kuwa ni mzima
na mwenye afya. Hata hivyo uzima, siha na afya vina maana pana zaidi.
Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema kuwa uzima, siha na afya vina
maana ya kudhamini mahitaji na burudani zote za kimwili, kiroho na
kijamii na si kutokuwa na maradhi au nakisi ya kiungo cha mwili pekee.
Kwa utaratibu huo mtu asiye na maradhi ya kimwili hawezi kutambuliwa
kuwa ni mzima na mwenye siha bali mtu mwenye siha na afya kamili ni yule
mwenye uzima na siha ya kiroho na kimwili kwa pamoja na mwenye utulivu
katika upande wa masuala ya kijamii. Utafiti wa kisayansi unaonesha
kuwa, chanzo cha matatizo mengi ya kimwili ni matatizo ya kiroho na
kifikra. Kwa mfano msongo wa mawazo na matatizo ya kifikra vinaweza kuwa
sababu ya maradhi ya utumbo. Hivyo basi, kwa kuwa matatizo mengi ya
kifikra na kiroho ya mwanadamu yanatokana na mahusiano yake na wanadamu
wenzake na vilevile matatizo ya kiutamaduni ya jamii, uzima na siha ya
mwili vinafungamana kwa kiwango kikubwa na afya na siha ya fikra na
mazingira ya kiutamaduni na ya kijamii katika jamii husika.
Afya kiistilahi ina maana ya harakati na hatua zote zinazochukuliwa
kwa ajili ya kuboresha na kunyanyua juu afya na uwezo wa mtu au jamii
ambayo ni pamoja na elimu na mbinu zinazosaidia kulinda afya na uzima wa
mtu na jamii. Sasa hebu tutazame misingi na nguzo za mfumo wa afya na
siha katika Uislamu.
Kwa kuwa afya na siha ni miongoni mwa mahitaji ya kimaumbile na
yanayolinda na kudumisha kizazi cha mwanadamu, Uislamu umetayarisha
mazingira mazuri ya kufikiwa malengo hayo kwa kuharamisha vitu vichafu,
vyenye madhara na khabithi na kuhalalisha vilivyo safi, salama na mwendo
wa wastani katika kitu. Sheria na kanuni za afya za Uislamu zimebuniwa
na kuelezwa kwa njia nzuri na ya kuvutia ili ziweze kuoana na kuwiana na
maumbile asili ya mwanadamu. Huwenda pia suala la kuwekwa kanuni za
afya na siha katika mafundisho ya dini ya Uislamu ni kwa sababu ya
Mwenyezi Mungu ameiweka hisi ya kupenda usafi na vitu visafi na salama
na hisi ya kuchukia na kujiepusha na uchafu na vyenye madhara kwa mwili
na roho ya mwanadamu katika maumbile ya asili ya mwanadamu. Aya ya 30 ya
suratul Rum inasema: "Elekeza uso wako sawasawa kwenye dini ambayo
ndilo umbile la Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hapana mabadiliko
katika maumbile ya Mwenyezi Mungu...."
Kwa mujibu wa aya hii, mafundisho na sheria za Uislamu zimetayarishwa
kwa mujibu wa fitra na maumbile ya asili ya mwanadamu na maslahi yote
ya kiumbue huyo yamezingatiwa katika mambo yote yaliyohalalishwa au
kuharamishwa na sheria za dini hiyo. Imam Sadiq (as) anasema: Mwenyezi
Mungu aliyeumba viumbe anajua ni vitu gani vyenye faida kwa miili yao na
kwa msingi huo alivihalalisha na kuviruhusu na akaharamisha na kukataza
vile vye madhara kwa miili yao."
Kwa kuwa masuala ya afya na siha yana umuhimu mkubwa sana, Mwenyezi
Mungu Mtukufu aliamua kuyaweka baadhi ya masuala hayo katika taratibu za
kiibada za Waislamu. Suala hili la kuwekwa masuala ya afya na siha
katika mafundisho ya dini lina maana ya dhamana ya utekelezaji wake
kutokana na umuhimu wake kwa mwanadamu. Kwani pale masuala hayo
yanapowekwa katika safu ya mambo ya wajibu na ya lazima kutekelezwa,
itakuwa muhali kwa Mwislamu anayeheshimu mafundisho ya dini kuyapuuza au
kuyaacha.
Hivyo basi Mwislamu yeyote anayeelewa kwamba jambo lolote
linalosababisha utulivu, afya na siha kwa Waislamu na wanadamu wenzake
linamridhisha Mola wake Muumba, ataharakia kulinda usafi wa mazingira na
kusaidia jitihada za kuimarisha afya ya umma. Mwislamu kama huyo
hatakuwa radhi hata kidogo kumwaga au kutupa taka katika maeneo ya umma,
kuchafua maji na mazingira, kuharibu misitu na vyanzo vya maji na
kadhalika na daima huwa na mlinzi wa ndani ya nafsi anayemzuia kufanya
mambo kama hayo.
Uislamu umehimiza sana juu ya afya na usafi na kuvitambua kuwa ni
sehemu ya imani ya mja. Kwa hakika miongoni mwa sifa makhsusi za Uislamu
ni kuwahamasisha wafuasi wake kulinda na kuchunga usafi na afya katika
mambo yote ya maisha yao. Dini hiyo iliyaweka mambo ya usafi na afya
katika taratibu za kiibada za dini hiyo na Mtume Muhammad (saw) amesema:
Usafi ni katika imani. Vilevile amewahimiza Waislamu kuwa wasafi na
kula vilivyosafi na salama kwa kusema: Chungeni usafi kadiri mnavyoweza
kwa sababu Mwenyezi Mungu Mtukufu ameujenga Uislamu kwenye msingi wa
usafi."
Hivyo basi mpenzi msikilizaji usafi na afya vimepewa nafasi maalumu
katika Uislamu na wafuasi wa dini hiyo wanalazimika kuyatambua masuala
hayo kuwa ni sehemu ya imani na itikadi za dini yao.
Mfumo wa afya na siha wa Uislamu umeweka ratiba kamili ya afya ya mtu
binafsi na jamii katika pande zote za kimwili na kiroho. Mfumo huo una
sheria za afya na siha ya mtu binafsi, familia, jamii, mazingira ya
kazi, siha na afya inayohusiana na chakula na kadhalika. Kwa mfano tu
aya ya 169 ya Suratu Maryam inawaamuru Waislamu kula vyakula halali na
visafi na ile ya 24 ya Suratu Abasa inawataka wawe makini kuhusu vyakula
wanavyochagua kwa ajili ya kula, uhalali wake na kadhalika. Hii ni
kutokana na ukweli kwamba, chakula kina mchango mkubwa katika uzima,
siha na afya ya mwili na roho ya mwanadamu. Katika masuala hayo ya afya
na uzima wa mwili na roho Mtume Muhammad (saw) anasema: "Sisi ni kaumu
ya watu ambao hatuli chakula ila pale tunapohisi njaa, na tunapokula
basi hatushibi na kujaza matumbo." Vilevile anasema katika hadithi
nyingine kwamba: "Utumbo ni nyumba ya maradhi yote, na kujiepusha kula
hadi kujaza tumbo ndio msingi wa dawa zote." Wasii na khalifa wake, Imam
Ali bin Abi Twalib pia alimuusia mwanaye Imam Hassan (as) kwa kusema:
Unataka nikufunze mambo manne yatakayokukinga na maradhi? Alisema ndiyo.
Imam alisema: Usiketi kwenye meza ya chakula ila unapokuwa na njaa na
usiondoke kwenye meza ya chakula ila ukiwa bado una hamu ya kula. Tafuna
vyema chakula na nenda msalani kabla ya kulala. Utakapotekeleza mambo
hayo yote basi kamwe hutahitaji dawa na tiba nyingine."
>>>
Agmo Uislamu na Mtindo wa Maisha-27
Assalamu Alaykum wapenzi wasikilizaji na karibuni kuwa nasi tena
katika sehemu nyingine ya kipindi chenu cha Uislamu na Mtindo wa Maisha.
Katika kipindi cha wiki iliyopita tulianza kuzungumzia suala la afya na
usafi katika mtindo wa maisha wa Kiislamu. Kipindi chetu cha leo
kitaendeleza maudhui hiyo. Karibuni.
Kama bado mnakumbuka tulisema katika kipindi cha wiki iliyopita
kwamba afya ina maana ya majmui ya shughuli na harakati za kuboresha na
kuinua juu kiwago cha siha na uwezo wa mtu na jamii kwa ujumla. Hatua
kama hizo ni pamoja na elimu na mbinu zinazosaidia kuboresha na
kuimarisha afya na siha ya mtu na jamii.
Hapana shaka kuwa itikadi za kidini za kila jamii huwa na mchango
mkubwa katika uzima na siha ya watu wa jamii hiyo. Katika upande huo
dini ya Uislamu imeipa umuhimu mkubwa roho na mwili wa mwanadamu kwa
kadiri kwamba, katika kuhimiza na kuwahamasisha wafuasi wake kuhusu
suala la kuchunga na kulinda afya zao, imebainisha na kusisitiza sana
juu ya athari zake za kimaada na kiroho na taathira zake za kiduni na
ulimwengu wa Akhera. Huwenda pia tunaweza kusema kuwa, uhamasisho mkubwa
zaidi wa Uislamu kwa masuala ya kiafya ni kueleza taathira zake katika
kupata radhi na mapenzi ya Mwenyezi Mungu. Maneo kama "tayyibat" kwa
maana ya vitu visafi na neno "twahara" kwa maana ya usafi vimekaririwa
mara kadhaa katika Qur'ani Tukufu, suala ambalo linaonesha umuhimu
mkubwa wa afya na siha ya mwili na nafsi katika mafundisho ya Uislamu.
Kwa kuwa mwili ndiyo merikebu na chombo kinachobeba roho na kulinda afya
na siha yake kuna taathira kubwa sana katika roho ya mwanadamu,
mafundisho mengi ya Uislamu yaliyoelezwa katika sheria za fiqhi
yamelizingatia na kulipa umuhimu suala la afya, uzima na siha.
Miongoni mwa masuala ambayo yana mchango mkubwa katika afya na siha
ya mwanadamu ni mtindo wa maisha na na taratibu na desturi za kula na
kunywa. Suala hilo pia limepewa mazingatio katika mafundisho ya Qur'ani
Tukufu ambayo imetilia mkazo suala la kuchunga mwenendo wa wastani
katika kula na kunywa. Mwenyezi Mungu SW anasema katika aya ya 31 ya
Suratul Aaraf kwamba: Kuleni na kunyweni wala msifanye ufujaji, hakika
Yeye (Mwenyezi Mungu) hawapendi wafanyao ufujaji.
Maagizo hayo ya Qur'ani ni kanuni kuu ya afya na siha ambayo ina
mchango mkubwa katika afya na uzima. Utafiti uliofanywa na wataalamu wa
afya umebaini kuwa, chanzo cha maradhi mengi ya mwanadamu ni chakula
ziada anachokula kiumbe huyo ambacho kalori zake hubakia mwilini bila ya
kutumika. Nishati hiyo inayobaki mwilini huwa mzigo mkubwa kwa moyo na
viungo vingine vya mwili na huwa chanzo na sababu ya maradhi mengine.
Sababu kuu ya kalori hizo ni chakula ziada au kwa maneno mengine kula
chakula kingi. Kula chakula kingi huwa sababu ya maradhi ya kisukari,
ukakamavu wa mishipa, mafuta mengi kwenye damu, matatizo ya ini,
kunenepa kupita kiasi na aina mbalimbali za ugonjwa wa kiharusi.
Mafundisho ya Uislamu kuhusu jinsi ya kula na kunywa yanadhamini
uzima, siha na afya ya mwili na roho ya mwanadamu. Mtume wetu Muhammad
(saw) anasema: "Jiepusheni kula sana kwani kufanya hivyo kunaufanya moyo
kuwa na ukatili, kunavitia viungo uzembe wa kumtii Mwenyezi Mungu na
kuyafanya masikio yasisikie hekima na mawaidha." Imam Ali bin Abi Twalib
(as) pia amesema: Mtu anayetosheka kwa kula chakula kichache huwa na
siha zaidi na fikra bora." Imam Jaafar Swadiq (as) pia amesema: "Mtu
anayetaka kuwa na siha na mwili wenye nishati, apunguze chakula chake
cha usiku."
Imenukuliwa katika kitabu cha tafsiri ya Qur'ani cha Majmaul Bayan
kwamba, mtawala Haroun Rashiid alikuwa na tabibu Mkristo ambaye umahiri
wake mkubwa katika masuala ya tiba ulikuwa maarufu sana baina ya watu.
Siku moja tabibu huyo alimwambia msomi wa Kiislamu kwamba: Sipati
chochote kuhusu masuala ya tiba katika kitabu chenu cha mbinguni yaani
Qur'ani, ilhali elimu zenye faida ni mbili: Elimu ya dini na elimu ya
miili. Msomi Mwislamu alijibu kwa kusema: Mwenyezi Mungu ameweka kanuni
zote za tiba katika nusu ya aya ya kitabu chake, Qur'ani, na Mtume wake
pia ameweka kanuni hizo katika hadithi inayosema: "Utumbo ni nyumba ya
maradhi yote na kupunguza kula ndiyo kinara wa tiba zote." Baada ya
kusikia maneno hayo Tabibu Mkristo alisema: "Qur'ani yenu na Mtume wenu
hawakumbakishia Jalinos kanuni yoyote mpya ya tiba." Jalinos huyu
anayetajwa na tabibu Mkristo alikuwa gijwi la tiba la Kigiriki.
>>>>>>
Suala la kuchunga adabu na desturi nzuri za kula na kunywa
linaonekana kwa wingi katika sira na mwenendo wa Mtume Muhammad (saw) na
Ahlibaiti zake watoharifu. Imepokewa kuwa Imam Hassan bin Ali (as)
alisema kuhusu baadhi ya adabu na kanuni za kula kwamba: Tonge la
chakula linapaswa kuwa ndogo, chakula kinapaswa kutafunywa barabara na
si vizuri kuwatazama usoni watu wengine wanaukula. Vilevile Imam Swaqid
(as) anasema: "Mtu anayeosha mikono yake kabla na baada ya kula chakula
huwa amekitia baraka chala chake na kujikinga na maradhi ya mwili."
Kuhusu adabu na sira ya Mtume (saw) wakati wa kula, imepokewa kwamba
mtukufu huyo alikuwa akiwakataza watu kupuliza kwenye chakula na
kinywaji na amesema katika hadithi nyingine kwamba: Msiache vyombo vyenu
bila ya kufunikwa.
Suala jingine linalosaidia afya na siha ya mtu ni usafi na kuwa
nadhifu. Usafi umepewa umuhimu mkubwa sana katika Uislamu kwa kadiri
kwamba, Mtume (saw) ameutaja kuwa ni alama na dalili ya Imani ya mja.
Usafi na unadhifu umesisitizwa sana katika Uislamu kiasi kwamba
wanazuoni wa fiqhi wa Kiislamu wametenga mlango maalumu unaozungumzia
usafi mwanzoni mwa vitabu vyao vya fiqhi na sheria za Kiislamu. Suala
hili linaonesha kwamba amali nyingi za mwanadamu haziwezi kutimia na
kukubalika bila ya kuzingatiwa usafi. Mtume Muhammad (saw) amesisitiza
sana juu ya suala la usafi kwa kutumia maneno mbalimbali. Anasema katika
hadithi moja kwamba: "Jisafisheni sana ili muzidishiwe umri na Mwenyezi
Mungu SW." Vilevile anasema: "Uislamu ni nadhifu, basi kuweni wasafi na
nadhifu, kwa sababu hataingia peponi isipokuwa mtu nadhifu."
Vilevile baadhi ya hadithi zinasisitiza kuwa kuchunga kanuni za usafi
kuna matunda mbalimbali na miongoni mwa matunda hayo ni kuzidishiwa
umri, kuwa na afya na siha, kuwa na uzima wa mwili na roho, kupata radhi
na kupendwa na Mwenyezi Mungu, kukamilika imani ya mtu, kupata baraka,
kuondokewa na umaskini na kadhalika.
Imepokewa kwamba Mtume (saw) alikuwa kigezo cha usafi na suala hilo
limesisitizwa sana hata ndani ya Qur'ani Tukufu. Aya ya 4 ya Suratul
Muddathir inasema: Na nguo zako zitwahirishe. Vilevile Mtume (saw) daima
alikuwa akiwausia maswahaba zake kuwa wasafi na maridadi na amesema:
Safisheni mavazi yenu, punguzeni nywele zenu na kuweni maridadi na
wasafi. Mfasiri mkubwa wa Qur'ani wa zama hizi Allamah Muhammad Hussein
Tabatabai amesema: Nguo nyingi za Mtume Muhammad (saw) zilikuwa za rangi
nyeupe na mtukufu huyo daima alikuwa akisema: "Wavikeni watu hai mavazi
meupe na wazikeni waliokufa kwa mavazi meupe." Kutokana na weupe wake,
mavazi hayo huonesha uchafu haraka na wazi zaidi na kumlazimisha
aliyeyavaa kuyavua na kuyasafisha mapema.
Wanahistoria wanasema Mtume Muhammad (saw) alikuwa akionekana msafi
kupita watu wote na aliwahimiza mno Waislamu kujipaka manukato, kuchana
nywele na kupiga mswaki na yeye mwenyewe alikuwa mstari wa mbele katika
mambo hayo. Hii leo wapenzi wasikiliza, imethibitika kuwa usafi wa mdomo
na meno ni miongoni mwa mambo muhimu katika kulinda siha na afya ya
wanadamu. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, vijidudu maradhi wengi
huingia mwilini kupitia njia ya mdomo. Mtume (saw) alilipa umuhimu
mkubwa suala hilo na alikuwa akiwaambia masahaba zake kwamba: "Midomo
yenu ni njia na kuvuko cha Qur'ani, hivyo isafisheni kwa kupiga
mswaki."
>>>>
Wapenzi wasikilizaji kipindi chetu cha leo kimeishia hapa. Ni
matarajio yangu kuwa mnenufaika na yale tuliyokuandalieni. Asanteni kwa
kututegea sikio na kwaherini....
Agmo Uislamu na Mtindo wa Maisha-28
Hamjhambo wasikilizaji wapenxzi na karibuni kuwa nami tena katikja
sehemu nyingine ya kipindi chenu cha kila wiki cha Uislamu na Mtindo wa
Maisha. Lipindi chetu cha leo kitaendelea kujadili umuhimu wa afya na
siha katika mtindo wa maisha wa Kiislamu.
Kuwa na afya na siha ni miongoni wma haki za mtu binafsi na jamii.
Uchunguzi wa ndani ya aya za Qur'ani Tukufu na vitabu vya wanazuoni wa
Kiislamu unaonesha kuwa dini hii tukufu ya Mwenyezi Mungu umelipa
umuhimu mkubwa suala la afya, uzima na siha ya mtu na jamii. Tunaweza
kusema kuwa hakuna dini au mfumo wowote mwingine wa kifikra na kujiamii
uliohimiza mno suala la afya na siha kama Uislamu. Dini hii imebainisha
masuala mengi ya afya katika kalibu ya sheria za fiqhi. Kwa mfano dini
hiyo imeharamisha kula vitu kama damu, mnyama ya mzoga, nyama ya wanyama
walioharamishwa, udongo, pombe na vileo vinavyoondoa akili ya mwanadamu
na kuhatarisha afya yake na kadhalika.
Katika upande mwingine mafundisho ya Uislamu yameyaweka masuala mengi
ya afya yenye nafasi muhimu sana katika afya na siha ya mwanadmu katika
sura ya wajibu au mustahabu na suna. Kwa mfano miongoni mwqa mambo
yanayoambatana na ibada ya Swala ni twahara ya mwili na mavazi anayetaka
kuswali na kutia udhu ambako kumetambuliwa kuwa ni wajibu kwa ajili ya
kutekeleza ibada hiyo. uchunguzi wa kina katika sheria za Kiislamu
unaweka wazi ukweli kwamba kila moja kati ya sheria hizo ina hekima na
falsafa maalumu ambayo huwenda wengi wengi wahazujui. Suala pekee
tunalolitambua ni kwamba katika falsafa ya sheria hizo kuna maslahi
yanayohimizwa au madhara yanayokatazwa kuhusu mwili au roho ya
mwanadamu. Kila kitu kinachokuwa na faid na maslahi kwa mwili na roho ya
mtu au siha na uzima wa jamii kimefanywa halali au wajibu na kile
chenye madhara na hasara kwa mtu au jamii kumeharamishwa.
Hapa tunapaswa kutaja nukta hii muhimu kwamba, katika Uislamu maslahi
yanatangulizwa na kupewa kipaumbele zaidi kuliko manufaa kwani yuymkini
jambo likawa na manufaa kwa mwanadamu lakini kwa ujumla lisiwe na
maslahi kwake yeye au jamii.
Vilevile kuna kanuni inayokataza madhara na kuwasababishia madhara
watu wengine, kuchafua mazingiraya maisha ya wanadamu, na kuwalazimisha
watu kuchunga kanuni za afya ya mtu binafsi na jamii. Kwa mfano tu
mwenyezi mungu SW amewaamuru Waislamu kuzika maiti zao kwa ajili ya
kulinda uzima, afya na mazingira.
Kama tulivyotangulia kusema katika vipindi vilivyopita, suala la afya
na misingi ya siha limehimizwa sana katika Uislamu wka kadiri kwamba
Mtume (saw) alilitaja kuwa ni katika alama za imani ya mja. Hii ni kwa
sababu katika Uislamu kila amali inayofanyika kwa nia ya kutekeleza
wajibu na amri ya Allah na kuwahudumia watu na jamii inatambuliwa kuwa
ni ibada.
Kuwa na sifa ya mwili na roho ni katika mambo yanayafanya maisha
jkuwa yenye utulivu na kutayarisha uwanja mzuri wa kuwa mja mwema wa M,
Mungu. Wkani ili kuweza kuwa mja mwema wa Allah, mwanadamu anahitaji
kuwa na mwili mzima na wenye afya na sifa. Kwa msingi huo mafndisho ya
Uislamu yamewajibisha suala la kulinda afya ya mwili na nafsi na
hayawaruhusu wafuasi wa dini hiyo kuudhuru mwili na nafsi hata wakatri
wa kipindi cha mashaka na misiba mikubwa. Baadhi ya hadithi zinasisitiza
kuwa mwili na viungo vyake ni amana ya Mwenyezi Mungu kwa wanadamu na
kwamba kulinda na kuchunga amani ni katika sifa muhimu za waumini wa
kweli. Mtume (saw) amesema: Sikio, jicho, ulimi na moyo ni amana, na
kila mtu asiyelinda amana hana imani."
Mfumo wa mwili wa mwili wa mwanadamu umetayarishwa kwa njia ambayo
iwapo misingi na kanuni zote za usafi, afya na siha za mtu binafsi na
jamii zitalindwa na kuchungwa basi asilimia ya maradhi yanayompata
mwanadamu itapungua wka kiwango kikubwa na huwenda kutoweka kabisa. Hata
hivyo mtindo usio sahihi wa maisha ya mwanadamu unamuweka kiumbe huyo
katika hatari ya kukumbwa na matatizo na maradhi ya aina mbalimbali.
Wapenzi wasikilizaji katika kipindi kipichopita tulizungumzia baadhi
ya hadithi za Mtume na Ahlibaiti zake zinazobainisha adabuna taratibu
kula na kunywa kwa njia sahihi kama hadithi ya Mtume iliyosema: Tumbo
ndiyo nyumba ya maradhi yote na kujiepusha kula sana ni dawa la kila
maradhi. Hivyo basi kuleni vyakula vinavyowiana na miili yenu".
Suala jingine linalosaidia katika uzima na afya ya mtu ni kupumzisha
viungo vya mwili ambavyo ni muhimu kuwa na uadilifu na mwenendo wa
wastani katika kuvitumia. Imam Ali bin Abi Twalib amesema: "Kuushinikiza
moyo kunazuia fahamu, kwa sababu kila kiungo cha mwili kinahitaji
kupumzika." Vilevile Imam Swadiq (as) amesema Mtu anayefanyakazi usiku
na kitopumzisha mwili kwa sababu kukosa kulala (hadi akapatwa na
madhara)basi kazi yake hiyo ni haramu japo itamuingizia mali ya halali."
Miongoni mwa nguzo muhimu za kudhamini uzima wa mwili na froho ya
mwanadamu ni kuwa na moyo wa kuridhika na kutosheka maishani na
kujiepusha na tamaa na pupa.