DALILI ZA KIAMA

MwenyeziMungu Subhanahau wa Taala anasema:-
"Yeye ndiye Mjuzi wa siri wala hamdhihirishii yeyote siri Yake isipokuwa aliyemridhia katika mitume Yake".
Al Jinn- 26-27
Kutujulisha Mtume(SAW) kwa siri za Dalili za (kukaribia kwa) Siku ya Kiama, dalili ambazo hazikudhihirika isipokuwa katika wakati wetu huu, ni ushahidi wa ukweli wa ujumbe wake na pia kunathibitisha kwamba Kiama kipo kweli na kwamba kimekwisha karibia 

MIONGONI MWA DALILI ZILIZOKWISHA ONEKANA NI HIZI ZIFUATAZO

1)Mambo Makuu Ambayo Waliotutangulia Hawakuweza hata Kuyafikiria.
Maajabu hayo na mambo makubwa mengi yaliyovumbuliwa pamoja na mambo ya kisiasa, nidhamu mbali mbali, sayansi pamoja na mambo yanayotokea kila siku duniani, ni mambo ambayo waliokuja kabla yetu wakiwa ni Waislamu au makafiri, hawakuweza kuyafikiria kabisa.
Mtume (SAW) ametujulisha juu ya mambo haya aliposema;
"Haitosimama saa (kiama) mpaka mtakapoona mambo makubwa makubwa ambayo hamkuwa mkiyaona wala hamkuweza kuyafikiria katika nafsi zenu".

2) Waendao Miguu Chini Wasiomiliki Nguo Wanaochunga mbuzi Wanaoshindana Kujenga Majumba Marefu Marefu
Mtu asiyemiliki viatu, anaetembea uchi, asiyemiliki nguo ya kuweza kumsitiri mwili wake wote, na anategemea chakula chake kwa wengine, asiye na kazi isipokuwa kuchunga mbuzi.
Isingempitikia mtu yeyote hapo zamani kwamba mwenye sifa kama hizo ataweza kujenga nyumba yoyote, sembuse aweze kujenga nyumba refu, tena aweze kushindana na wenzake kwa kujenga majengo marefu kisha kushindana huko kwa watu wa nama hii, kuwe ni jambo la kawaida tu (mtindo) sio kwamba ni mtu mmoja tu atakayefanya hivyo, bali ni wengi sana miongoni mwa wachunga kondoo wasio na viatu wasio na nguo, wasiojitegemea, ni mambo ambayo mtu asigeweza kuyafikiria kwamba yatatokea.
Lakini haya yametokea baada ya MwenyeziMungu kuwafungulia Waislamu na wengineo katika mali zilizomo ardhini na hasa Petroli, tukawaona wachunga kondoo wasiovaa viatu, wala nguo (hata nguo zao wanategemea kushonewa na mataifa mengine), wasiojitegemea, wankishindana kujenga majumba marefu, kama alivyokwishatuelezea Mtume(SAW)  na akatubainishia kwamba hizi ni miongoni mwa Dalili za kukaribia kwa Kiama.
Akasema;
"Mtakapowaona wasiovaa viatu, wasiovaa nguo, wasiojitegemea wenyewe, wachunga kondoo, wakishindana kujenga majumba mrefu, basi muisubiri Saa (Kiama).
(Bukhari na Muslim)

3) Kuja Kwa Wanawake Waliovaa Huku Wakiwa Uchi, Wakiyumba Na  Kuyumbisha Na Vichwa Vyao (viko) Kama Nundu Ya Ngamia
Kulikuwa na tatizo katika kuwafahamu wanawake aliowataja Mtume (SAW) watakaokuja mwisho wa Umma huu, na kwamba watakuwa wanavaa nguo na wakati huo huo wako uchi.
Mtu anaweza kushangaa vipi mtu anaweza akawa amevaa nguo na yupo uchi  wakati mmoja, mpaka  tulipoyaona wenyewe katika wakati wetu huu. Utaona mwanamke amevaa nguo lakini zinambana ama ni nyepesi zikimkashifu sehemu zake za aibu na kuzidhihirisha, (au atakuwa amevaa nguo nyingi lakini fupi) au atakuwa mwenye kuvaa nguo mahali mwengine na mahali mwengine anazivua (Sehemu za mabwawa ya kuogelea au pwani).
Wanawake hao pia wanakuwa wanayumba yumba na huku wakiyumbisha.
Kumekamilika kuyumba kwao baada ya kuyumba mbali na njia iliyoonyooka, na kukapatikana kuyumba kwa miili yao walipowatilia visigino virefu katika viatu vyao ili wakamilishe kwa kuiyumbisha miili yao pia, na kwa njia hiyo wanayumbisha wengi miongoni mwa vijana wa kiume wakibabaika na urembo wao wanaoutembeza.
Na maana ya 'Vichwa vyao kama nundu ya ngamia inayoyumba';
Haya tunayashuhudia wakati wetu huu (kwa wanaovaa mawigi na katika staili mbali mbali za usukaji), yote haya yakisadikisha hadithi ya Mtume (SAW) aliyefunuliwa haya na Mola wake mia elfu na mia nne iliyopita aliposema:
"Aina mbili katika umati wangu ni katika watu wa Motoni, sikuwaona: Wanaume wenye viboko mikononi mwao (urefu wake) kama mikia ya ngo'mbe, wanawapiga watu (kwa kuwadhulumu na kuwaonea). Na wanawake waliovaa nguo (huku) wakiwa uchi walioyumba na kuyumbisha,  vichwa vyao (wanawake hao) mfano wa nundu la ngamia linaloyumba. (Watu hawa) Hawataingia Peponi wala  hawataipata (hawataionja) harufu yake".
(Ahmad na Muslim)

4)  Kuzungumza Kwa Vitu
Mtume (SAW) amesema:-
"Moja katika dalili za kukaribia kwa Kiama ni kuwa mtu aliyetoka nyumbani kwake, anaporudi anakuta viatu na fimbo yake vikimuelezea yote yale waliyofanya watu wake baada ya kutoka kwake".
(Imetolewa na Attirmidhy na Al Hakim.)
Kiatu ni kitu kisichokuwa na roho na fimbo ni kitu kisichokuwa na roho. Isingempitikia mtu wakati ule kufikiria kwamba vitu kama hivyo vingeweza kusema, lakini katika zama zetu hizi tunaviona vitu hivi vikisema.
Vipi kiatu na fimbo vitamueleza mtu yale yaliyotokea nyumbani?
Hivi sasa vimekwishaundwa vyombo ambavyo mwanaadmu anavibeba na vinamletea habari na sauti kutoka nyumbani kwake au kutoka nyumba za wenzake. (Hakuna kilichobaki isipokuwa kiundwe chombo (iundwe kamera) mfano wa fimbo ili ibebeke kwa urahisi au kiwekwe chombo hicho mahali ndani ya kiatu ili kisionekane), au kiwezekane kuwekwa katika sehemu ya fimbo au katika sehemu yoyote ya kiatu bila kuonekana.

Kuzuilika Kwa Elimu, Wingi Wa Mitetemeko Ya Ardhi Na Kukaribiana Kwa Wakati, Kuenea Kwa Fitina Na Kwa Majengo Marefu.
Kuzuilika kwa Ilimu maana yake ni Kufa kwa maulamaa na kutokupatikana kwa maulamaa wengine kuchukua nafasi zao, na makusudio yake ni maulamaa wa Kiislamu kama ilivyotufahamisha Hadithi.
Na Kukithiri kwa Mitetemeko ya ardhi, maana yake ni hiyo mitetemeko inayoangamiza tunayoiona na kuisikia kwa wingi siku hizi.
Na kukaribiana kwa wakati *, maana yake ni kwenda haraka kwa siku bila kuzihisi utafikiri masaa machache tu yamepita,  na hii inatokana na mambo mengi  yanayotokea ulimwenguni na kutufanya tusizihisi siku zinavyokwenda, na MwenyeziMungu ndie anayejua zaidi, kwani unapokuwa umejishughulisha na kazi saa hupita bila kuhisi kama kwamba ni dakika chache tu, lakini unapokuwa bila ya kazi wakati unauona mrefu, hauendi, na wakati wetu huu umejaa mambo mengi yanayosababisha siku zipite haraka sana. [1]

Kuenea kwa Fitna, maana yake ni wingi wa maasia yanayomtia mtu katika mitihani ya dini yake. Na maasia hayo hufanyika wazi wazi bila ya kificho.
Ama urefu wa majumba, ni juu yako msomaji kulinganisha majengo yaliyokuwa miaka hamsini iliyopita na ya hivi sasa na uone vipi yalivyorefuka.
Yote hayo amekwishatueleza Mtume wa Mwenyezi Mungu(SAW), aliposema:-
"Hakitosimama kiama mpaka izuilike ilimu na ikithiri mitetemeko ya ardhi na wakati ukaribiane na kuongezeka kwa mitihani na watu wawe wanashindana kwa kujenga majumba marefu."
Bukhari na Muslim

Kuhusisha Salamu, Kuenea Kwa Biashara, K upigana Pande Ndugu wa Nasaba, Kusoma Kwingi Na Ushahidi Wa Uwongo.
Kuhusisha salamu; ni kule kuwatolea salamu watu makhsusi.
Kuenea kwa biashara;  ni kule kuenea kwake.
Na Kuenea kwa kalamu;  ni kuongezeka utumiaji wake nayo ni dalili ya kusoma na kuandika kwa wingi.
Haya yote yameelezwa katika hadithi ya Mtume (SAW) isemayo:
“Kwa hakika kinapokaribia Kiama watu watawasalimia watu makhsusi, na biashara itaenea hata mke atakuwa akimsaidia mumewe katika kazi za biashara, na kupigana pande ndugu wa nasaba, na kuenea kwa kalamu na kuongezeka kwa ushahidi wa uongo na kuficha ushahidi wa kweli.
(Imetolewa na Bukhari).

Kuongezeka Uzinzi Na Ulevi
Mtume (SAW) amesema:-
"Hakika katika dalili za kukaribia kwa Kiama, ni kutoweka kwa Ilimu, kuongezeka ujinga, kuongezeka uzinzi, na kuongezeka kwa unywaji wa pombe.
Bukhari na Muslim
(Kongezeka Ujinga Maana Yake Ni Kuongezeka kwa ujinga wa Kutoijuwa Dini).

Kuenea Ulaji Wa Riba
Mtume (SAW) amesema:-
"Utawafikia watu wakati, hapatakuwepo mmoja wao asiyekula riba, na yule asiyekula basi litamfikia vumbi lake.
Abu- Daud na Ibnu Maajah

Wakati wetu huu sasa ulaji wa riba umekwisha enea kwa njia za mabenki na njia nyengine juu ya kuenea kwa benki za Kiislamu ambazo hazijishughulishi na ulaji wa riba, basi tunamwomba MwenyeziMungu aziongeze benki za aina hii.

9)   Kusalimiana Kwa Kulaaniana, Na Wanaume Kujifananisha Na Wanawake  Na Wanawake Kujifananisha Na Wanaume
Uislamu unatuamrisha tutoleane salamu njema na kuzijibu vyema. Hivi ndivyo walivyokuwa Waislamu hapo zamani, mpaka ulipofika wakati wetu huu tukaona watu wanasalimiana kwa kulaaniana.
Mtume(SAW) alisema:-
"Umma utakuwa bado unafuata sheria njema iwapo hayajawatokelea mambo matatu;
Iwapo bado hawakuzuwiliwa elimu, na hawakuongezeka miongoni mwao watoto wa haramu na kutokea miongoni mwao Al Saqaarun.
Wakauliza : Ni nani hawa Al Saqaarun?
Akasema : Vijana watakaotokea katika zama za mwisho watakuwa pale wanapokutana wanasalimiana kwa kulaaniana".
Ahmed na Al Hakim na Al Tabarani

Hapakuwa na mtu aliyeweza kufikiria kwamba iko siku mwanamme atajifananisha na mwanamke au kinyume cha hivyo mpaka ukatufikia wakati ulipotujia msiba huu.
Lakini Mtume (SAW) alikwisha kutupa habari hiyo.
MwenyeziMungu alimjulisha juu ya yale yatakayotokea ndipo Mtume (SAW) aliposema:-
"Miongoni mwa alama za kukaribia kwa Saa (Kiama) ni wanaume kujifananisha na wanawake na wanawake kujifananisha na wanaume".
Imepokelewa na Abu Daud

10)      Na Kundi Likidhiihirisha Haki
Kama utakavyozidi ufisadi, MwenyeziMungu kwa hikima yake ametaka libaki kundi la watu likiidhihirisha haki. (Kundi hilo) Linawasimamishia watu hoja kwa dalili huku likiwalingania na kuwaita katika njia ya MwenyeziMungu na katika kushikamana na kitabu chake na Mafundisho ya Mtume wake (SAW).
Na haya ndio tunayoyashuhudia sasa, kila mahali hawakosekani watu wanaoidhihirisha dini ya MwenyeziMungu wakishikamana na kitabu cha MwenyeziMungu na Mafundisho ya Mtume wake (SAW).
Kuhusu watu hawa Mtume amesema:-
"Litaendelea kubaki kundi  miongoni mwa umma wangu likiidhirisha haki (wala) hawadhuriki na wale wanaowaachia mkono mpaka itakapotokea amri ya MwenyeziMungu".   
(Attirmidhy Na Abu Daud).
Haya ni machache tu miongoni mwa mengi aliyotujulisha Mtume(SAW) tokea miaka elfu na mia nne iliyopita, yakiwa ni ushahidi juu ya ukweli wa bishara zake na  yakithibitisha kwamba ameletwa kuwa mwonyaji kwetu juu ya adhabu kali itakayowakuta (wanaomuasi MwenyeziMungu).
Basi kama tunavyoziona dalili za kukaribia kwa Kiama hivi sasa, tutakuja kukiona Kiama chenyewe kesho, kwa sababu aliyetujulisha juu ya yote hayo ni mmoja, naye ni msema kweli anayesadikiwa, Muhammad bin Abdillah (SAW).

USHAHIDI KATIKA QURANI TUKUFUKU JUU YA KUBADILIKA KWA NIDHAMU ZA MAUMBILE

MwenyeziMungu ameumba ulimwengu na anauendesha kwa nidhamu iliyo thabiti, lakini anapotaka, hubadilisha nidhamu hizo ili kuupa nguvu ushahidi wa Mitume yake na ili wasadikiwe.
Miongoni mwa mifano hiyo ni yale yaliyotokea mikononi Mtume wetu (SAW), nayo ni mengi yakiwa ni ushahidi uliowafanya watu wengi waukubali ukweli wa ujumbe wake na utume wake, yakiwemo yafuatayo:-

1) KUPASUKA KWA MWEZI

Nidhamu iliyoumbiwa mwezi ni kuwa Mwezi ni kitu kimoja,  hapana awezaye kuupasua sehemu mbili isipokuwa MwenyeziMungu, lakini makafiri walipomkadhibisha Mtume (SAW) na kutaka dalili ili wamsadiki, MwenyeziMugnu akaupasua mwezi pande mbili na Mtume (SAW) akawaambia makafiri;
"Shuhudieni"
Lakini makafiri walipoona vile wakasema;
"Ameturoga Muhammad".
Lakini hawakuikadhibisha dalili hiyo walipoiona, ndipo MwenyeziMungu alipoteremsha kauli Yake isemayo:-
"Saa (kufika kiama) imekaribia; na mwezi umepasuka. Na wakiona Muujiza hugeuka upande na kusema; "Uchawi tu (huu wake) unazidi kundelea!".
(Al Qamar 1-2)

ISRAA NA MIRAJI

  MwenyeziMungu alitaka kumpandisha Mtume wake(SAW) na kumfikisha penye "Sidratul Muntaha (mkunazi wenye kumalizika mambo yote) uliopo juu ya mbingu saba, na hakupandishwa kutokea Makka, bali alimpeleka katika usiku mmoja kutoka Makka hadi Baitul Maqdis (Jerusalem), na kutoka hapo ndipo alipopandishwa.
Kupelekwa kwake kutoka Makka hadi Baitul Maqdis katika usiku mmoja kulikuwa ni dalili kwa makafiri ikithibitisha ukweli wake, kwa sababu walimkadhibisha Mtume(SAW), kisha wakampa mtihani ili wahakikishe ukweli wake.
Wakamtaka awaelezee wasfu wa Baitul Maqdis, wakiwa wanaelewa kuwa yeye hajapata kuuona msikiti huo kabla ya hapo. Mtume(SAW) akawaelezea jinsi ulivyo msikiti huo kwa kuzitaja pembe zake zote. Kisha wakamuuliza juu ya msafara wa jamaa zao walokuwa wakiusubiri (ukitokea huko Jerusalem), akawaeleza mahali msafara huo ulipo kwa wakati huo, idadi ya watu waliokuwemo ndani yake msafara huo, kabila zao, aina ya ngamia waliokuwa nao, na akawaelezea hata wasfu wa ngamia anayeutangulia msafara huo na nini amebeba ngamia huyo, na akawaelezea hata wakati gani utawasili msafara huo, na ukawasili wakati ule ule alowaambia kuwa utawasili.
Haya yote yakawa ni ushahidi wa kupelekwa kwake Baytul Maqdis(Israa), na kwa hivyo unakuwa pia ni ushahidi wa kupandishwa kwake mbinguni (Miraji).
Qurani imeelezea juu ya Israa.
Mwenyezi Mungu anasema:-
"Utukufu ni wake Yeye ambaye alimpeleka mja wake usiku mmoja tu kutoka msikiti mtukufu wa (Makka) mpaka msikiti wa mbali wa (Baitul Maqdis-Palastina) ambao tumeubariki na (tumevibariki) vilivyoko pembezoni mwake."
Suratul Israa (Bani Israil ) -1

Ama kuhusu Miraji (kupandishwa mbinguni), MwenyeziMungu anasema:-
"Jee! Mnabishana naye juu ya yale anayoyaona (daima)?
Na Mtume akamuona (Jibril) mara nyengine (kwa sura ile ile ya Kimalaika katika usiku wa Miraji). Penye mkunazi wa kumalizikia (mambo yote). Karibu yake kuna hiyo Bustani, (Pepo) itakayokaliwa maisha (na hao watu wema). Kilipoufunika mkunazi huo kilichoufunika (katika mambo ya kiajabu ya kimbinguni). Jicho halikuhangaika wala halikuruka mpaka huo(uliowekwa). Kwa yakini aliona (Nabii Muhammad)  Mambo makubwa kabisa katika alama, (Qudra) za Mola wake".
(An Najm 12-18).

Pepo na Moto ni katika miujiza ya MwenyeziMungu aliyoyaona Mtume(SAW).
Hakika Israa na Miraji ni miongoni wa ubadilishaji wa nidhamu alizoziumba MwenyeziMungu na akazijaalia kuwa ni ushahidi wa kuthibitisha ukweli wa Mtume wake(SAW).

UPEPO NA ASKARI WASO ONEKANA UNAPIGANA VITA KUMSAIDIA MTUME NA SAHABA ZAKE

Waislamu walikuwa upande mmoja wa handaki kubwa walochimba ili kuwazuia washirikina wasiweze kuwafikia, na makafiri walikuwa  upande mwingine wa handaki hilo.
Ghafla upepo mkali ukatokea pamoja na askari waso onekana, na upepo huo ukazima moto wa makafiri na kuwapeperushia mbali vitu vyao pamoja kubomoa majumba yao na kun'goa mahema yao na kuwakimbiza farasi na ngamia wao.
Tahamaki washirikina waliokuja kutoka sehemu za mbali na kuwazunguka Waislamu kwa siku nyingi, wakaona wanafukuzwa wakitaka wasitake. Wakarudi huku wakiwa wamehizika. Waislamu pamoja na Mtume(SAW) wakawa wanaisoma na kuikariri kauli ya Mtume(SAW):-
"Alhamdu lillahi wah-dahu sadaqa waa-dahu wa nasara abidahu wa a-azza jundahu, wa hazama l Ah- zaaba wahadahu."
  "Shukurani zote anastahiki MwenyeziMungu Peke Yake, amesadikisha ahadi Yake, amemnusuru Mtumwa Wake, kawatukuza askari wake na akayashinda majeshi ya makafiri (Ahzabu) peke Yake".
Na kutokana na haya ndipo MwenyeziMungu alipoteremsha kauli yake katika Suratul Ahzab aliposema:-
"Enyi mlioamini! kumbukeni neema za MwenyeziMungu zilizo juu yenu; yalipokufukieni majeshi, tukayapelekea upepo na majeshi msioyaona (ya Malaika), na MwenyeziMungu anayaona (yote) mnayoyafanya".
(Ahzab  9)

4)  USINGIZI MVUA NA MALAIKA WALITEREMKA KUWASAIDIA WAISLAMU

 Waislamu walikuwa wakielekea "Badar" kupambana na washirikina huku wakiwa na hofu kwa ajili ya uchache wao na udhaifu wao. MwenyeziMungu akawateremshia usingizi ili iwe alama ya usalama juu yao. Wengine wakaota, na shetani akaanza kuwatia wasiwasi na kuwafanya waogope kufa wakiwa na janaba ili warudi nyuma wasipigane vita.
MwenyeziMungu akateremsha mvua ili waweze kukoga (kujitahirisha na janaba) na ili mchanga ukazane chini ya miguu yao (isizame ndani ya mchanga) wanapokwenda vitani. Kisha yalipokutana majeshi mawili hayo, Malaika wakateremka, na makafiri wakashindwa vibaya sana katika pambano la mwanzo baina ya makafiri na Waislamu. Ndipo ilipoteremka kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"(Kumbukeni) alipokuleteeni usingizi uliokuwa(alama ya) salama itokayo kwake, na akakuteremshieni maji mawinguni ili kukutahirisheni kwayo na kukuondoleeni uchafu wa shetani na kuzipa nguvu nyoyo zenu kuithubutisha miguu yenu chini (isiwe inazama zama mchangani) (kumbukeni) Mola alivyowafunulia Malaika akawambia (Malaika); Hakika mimi ni pamoja na nyinyi, basi watieni nguvu wale walioamini nitatia uwoga katika nyoyo za makafiri. Basi wapigeni katika shingo (zao) na wakateni katika kila ncha ya vidole vyao".
(Al Anfal 11-12)

5) MAASKARI WA MWENYEZIMUNGU WANAMSAIDIA MUHAMMAD(SAW) DHIDI YA MAKAFIRI KATIKA HIJRA

Makureish waliamua kumuua Muhammad (SAW), na vijana wao wakaizunguka nyumba yake, lakini Mtume(SAW) alitoka mbele yao huku MwenyeziMungu akiwa amewaziba macho, na akajificha katika pango liitwalo (Ghaari Hiraa) yeye na sahibu yake Abu Bakar Al Siddique (RA) aliyekuwa akihofia wale makafiri walokuwa wakiwatafuta wasije wakachungulia ndani ya pango hilo na kuwaona, lakini askari wa Mwenyezi Mungu waliwafanya wasichungulie ndani ya pango.
Mpanda farasi hodari Suraqa bin Malik aliwafuata Mtume(SAW) na sahibu yake baada ya kutoka pangoni, lakini alipowakaribia miguu ya farasi wake ilizama ndani ya mchanga mpaka tumbo la farasi huyo likagusa mchanga na akaanguka kutoka juu ya farasi wake. Ndipo Suraqa alipoomba amani kutoka kwa Mtume (SAW).
Na haya yanaelezwa katika aya ya Qurani inayosema:
"Kama hamtamnusuru (Mtume), basi MwenyeziMungu alimnusuru walipomtoa wale waliokufuru; alipokuwa (mmoja tu na mwenziwe) wa pili wake, (peke yao) walipokuwa wote wawili katika pango; (Mtume) alipomwambia sahibu yake, "Usihuzunike kwa yakini MwenyeziMungu yuko pamoja na sisi" MwenyeziMungu akamteremshia utulivu wake na akamnusuru kwa majeshi msiyoyaona, na akafanya neno la wale waliokufuru kuwa chini; na neno la MwenyeziMungu ndio la juu. Na MwenyeziMungu ndie mwenye Hikima".
(Attawba -40)

SUALI NA JAWABU

Mtu anaweza kuuliza:
"Inawezaje imani yangu juu ya miujiza hii iliyotokea, ikawa sawa na imani ya wale walioshuhudi yakitendeka?"
Jawabu;
"Kwa kuyazingatia, na kwa kutumia akili utaifikia imani hiyo;
Kwa mfano Muujiza wa Upepo na askari wasioonekana, na Muujiza wa Kugawika kwa mwezi, haya yametokea mbele ya mamia na maelfu ya Waislamu pamoja na washirikina, Kisha (aya katika) Qurani ikateremshwa na kuyaelezea matukio hayo. Waislamu wakasikia na makafiri wakasikia jinsi Qurani ilivyoyaelezea matukio hayo. Waislamu wakasadiki yaliyoelezwa na Qurani yale waliyoyaona kwa macho yao tena mbele yao yakitokea na hii ikasababisha kuipa nguvu zaidi Imani zao pamoja na kuwafanya wawe thabiti katika Jihadi na Ibada zao.
Makafiri pia wakasadiki yaliyoelezwa na Qurani juu ya Miujiza iliyotokea mbele yao, na wala hawakuyakanusha isipokuwa walifasiri kupasuka kwa mwezi na miujiza mingine kuwa ni uchawi unaoendelea. Makafiri hao hao baadae wakaingia katika dini ya Kiislamu, wakawa wao ndio walioiyanyua dini hii na kuineza Mashariki ya ardhi na Magharibi yake.
MwenyeziMungu ameihifadhi Qurani isiweze kubadilishwa kwa namna yoyote ile na kama unavyoona kuwa Msahafu uliopo Marekani uliopo Uchina uliopo Bara Hindi uliopo Urusi uliopo Ulaya uliopo Afrika, ni Msahafu ule ule uliosomwa na baba zetu na babu zetu katika Mashariki ya ardhi na Magharibi yake na ndio huo huo aloteremshiwa Mtume wa Mwenyezi Mungu Muhammad (SAW).
Kutokana na haya tunaelewa kwamba miujiza hiyo imeandikwa katika kitabu kitukufu kuliko vitabu vyote, kitabu ambacho watu wote ulimwenguni wanakubaliana juu ya ukweli huu. (kwamba yaliyomo ndani ya Qurani hivi sasa, ni yale yale yaliyokuwemo wakati ule Mtume (SAW) alipokuwepo duniani, bila ya kupunguzwa wala kongezwa neno).
Ingelikuwa Qurani imetoa habari juu ya jambo kwamba limetokea na kumbe halikutokea, mfano wa Kugawika kwa mwezi au Kusalitishiwa upepo mkali washirikina katika vita vya Al -Ahzab, basi wangeyakanusha hayo makafiri na Waislamu, na kwa hivyo asingebakia mtu katika dini ya Kiislamu.
Lakini yaliyotokea ni kinyume na hayo na huu ukawa ni ushahidi kwamba yote yaliyoelezwa katika Qurani ni ukweli uliotokea na kushuhudiwa na Waislamu pamoja na makafiri.
Na MwenyeziMungu ameyahifadhi yote hayo katika Qurani bila kuongezwa wala kubadilishwa.
   

USHAHIDI KATIKA KATIKA HADITHI ZA MTUME (SAW) JUU YA KUBADILIKA KWA NIDHAMU ZA MAUMBILE

Waislamu wameyahifadhi maneno ya Mtume wao (SAW), vitendo vyake pamoja na yale aliyoyakubali, na wakazihifadhi sifa za mwenendo wake na za umbile lake na kila kinachohusiana naye, na wakaelezea juu ya miujiza ambayo MwenyeziMungu ameijaalia itendeke mikononi mwake, miujiza iliyosababisha wengi wao Wasilimu na kuzinukuu habari hizo vizazi baada ya vizazi.
Maulamaa wa hadithi za Mtume(SAW) nao wakahangaika kuhakikisha ukweli wa hadithi hizo vizazi baada ya vizazi wakiyaweka sawa maneno na wakihakikisha juu ya ukweli wa mlolongo wa majina ya wapokezi wa hadithi hizo (narrators).
Miujiza mingi sana ilitendeka mikononi mwa Mtume (SAW) na kutajwa katika vitabu vya hadithi zake (mafundisho). Tutaelezea baadhi ya miujiza hiyo:

KUYAZIDISHA MAJI KIDOGO YAKAWA MENGI

Waislamu walikuwa na shida ya maji ya kutawadhia hapo Madina.
Anas(RA) amesema;
"Mtume (SAW) alikuja na chombo mahali paitwapo Zawraa akiwa pamoja na Sahaba wake. Akauweka mkono wake ndani ya chombo hicho na maji yakaanza kutoka vidoleni pake, watu wote wakatawadha."
Akasema Qatada;
"Nilimuuliza Anas: Mlikuwa wangapi?
 Akasema;
"Mia tatu".
Bukhari na Muslim
Na Imam Bukhari anasema:
"Yakatokea kama haya wakati Mtume (SAW) alipokuwa safarini pamoja na Masahaba sabini."
"Yalitokea tena kama hayo walipokuwa Hudaibiya na idadi ya Waislamu ilikuwa elfu na mia nne, yalipoongezeka maji kisimani".
Bukhari
Yakatokea tena Mtume(SAW) alipokuwa safarini pamoja na sahaba zake, alipogusa vyombo viwili vya maji vya bibi mmoja vilivyokuwa havina hata tone ya maji ndani yake, vikajaa, wakanywa Waislamu na idadi yao ilikuwa ni wanaume arobaini. Kisha kila mmoja akajaza kiriba chake, hata yule bibi akasema;
"Nimeonana na mchawi kupita wote ama yeye ni Mtume kama wasemavyo"
Watu wa kabila lake wote wakasilimu.
Bukhari

2)  CHAKULA KICHACHE KUONGEZEKA KIKAWA KINGI

Mtume (SAW) alikuwa na njaa akamjia  sahaba mmoja aitwaye Abu Talha akiwa na mikate michache ya ngano, Mtume (SAW) akawaamrisha masahaba wake waikate vipande vidogo vidogo, kisha akamwomba MwenyeziMungu Subhanahu wa Taala na akawataka masahaba waile mikate hiyo watu kumi kumi mpaka wote wakashiba na idadi yao ilikuwa ni watu sabini au themanini.
Njaa kali sana ilimshika Mtume (SA) pamoja na sahaba zake walipokuwa wakichimba handaki (Siku ya vita vya Khandaq). Jabir (RA) mmoja wa sahaba zake akachinja kondoo mdogo kwa ajili ya Mtume (SAW) na baadhi ya sahaba zake, lakini Mtume(SAW) akawakaribisha kula chakula hicho wote walokuwa wakichimba handaki hilo na idadi yao ilikuwa elfu  moja (RA), na MwenyeziMungu akaibariki nyama na mikate ile, wakala wote mpaka wakashiba.
Bukhari
Katika vita vya Khandaq (handaki)  na katika vita vya Tabuk, Waislamu walikuwa na shida kubwa ya chakula, wakamtaka ruhusa Mtume (SAW) wachinje ngamia.
Omar(RA) akatoa rai kwamba watu wote wakusanye vyakula vyao mahali pamoja kisha wamwombe Mtume(SAW) ili amwombe MwenyeziMungu awabarikie chakula hicho, Mtume(SAW) akakubali na Mwenyezi Mungu akawabarikia chakula hicho hata  watu wote kambini humo waliweza kujaza vyombo vyao chakula.
Kisha akasema:-
"Nashuhudia kwamba hapana anayestahiki kuabudiwa isipokuwa MwenyeziMungu (Allah) na kwamba mimi ni Mtume wa MwenyeziMungu."

 

3)   KUSIKITIKA KWA SHINA LA MTENDE NA CHAKULA KUMSABIHI MWENYEZI MUNGU

Mtume(SAW) alipoacha kuliegemea shina la mtende anapowahutubia Waislamu Hutuba ya Ijumaa baada ya kutengenezwa membari, shina hilo la mtende alokuwa akiliegemea miaka mingi lililia kwa masikitiko na kutoa sauti mfano wa ngamia anavyolia, hata likakaribia kupasuka, na Mtume (SAW) akalikumbatia shina hilo mpaka likatulia.
Bukhar, Attirmidhy na Annasai.
Imeelezwa na Maimam Al Bukhary na Attirmidhy kuwa masahaba walikuwa wakisikia chakula kikimsabihi MwenyeziMungu huku kikiingia kinywani mwa Mtume (SAW).

4)      KULINDWA KWA MTUME (SAW) KUTOKANA NA MAADUI ZAKE

Abu Jahal aliapa kwamba ataipindapinda shingo ya Mtume(SAW) kwa miguu yake atakapomwona anasali. Na alipomuona akisali, alimwendea ili aitimize  ahadi yake hiyo, lakini mara akaonekana akirudi kinyume nyume huku akijikinga kwa mikono yake.
Akaulizwa;
"Vipi, una nini"?
Akajibu;
"Baina yangu na yeye, pana shimo kubwa la moto na mnyama mkubwa wa kutisha mwenye mabawa".
Bibi mmoja wa kiyahudi pia alifanya njama ya kutaka kumwua Mtume(SAW), akatia sumu katika nyama ya mbuzi aliyomkaribisha Mtume wa MwenyeziMungu(SAW), Mtume akajuwa kuwa ina sumu, akaitema, lakini sumu ile iliwasibu baadhi ya masahaba (walokula nyama hiyo).

5)   KUJULISHA MAMBO YA GHAIBU

Mtume(SAW) aliwajulisha sahaba zake yale yatakayotokea akiwepo duniani na baada ya kufa kwake hadi siku ya kiama.
Sababu ya kusilimu kwa watu wa Yemen ni kuwa Mtume(SAW) aliwajulisha Wafursi  na Wayemen kwamba mfalme wa Wafursi keshauliwa, na kwamba Mwenyezi Mungu amefanya hivyo ili kulipa kisasi cha Mtume wake(SAW), na Mtume(SAW) akawatajia mpaka usiku aliouliwa Kisraa mfalme wa Wafursi.
Na hii ndiyo sababu iliyowafanya watu wa Yemen pamoja na Wafursi walokuwa wakiishi huko kuingia katika dini ya MwenyeziMungu makundi kwa makundi.

UTABIRI JUU YA KUJA KWAKE (SAW) ULIOMO KATIKA VITABU VILIVYOTANGULIA

Hapana awezaye kudai kwamba Muhammad(SAW) ndiye aliyewaandikia Mayahudi,  Manasara, Majusi,(walokuwa wakiabudu moto), na Mahindu  katika vitabu vyao wanavyovitukuza, juu ya wasfu wake, jina lake, wakati gani atakuja pamoja na nchi yake, hayo yakishuhudia kuwa yeye ni Mtume aliyeletwa na MwenyeziMungu, maana yote hayo yameandikwa katika vitabu vyao karne nyingi kabla ya kuzaliwa kwake (SAW).
MwenyeziMungu anasema:
"Na haya (yaliyomo ndani ya Qur-ani) yamo katika vitabu vya kale".
Ashuraa - 196
Kutabiriwa huko kulisababisha vizazi baada ya vizazi vya Manasara na Majusi  na Wahindu kumkubali kwamba yeye ni Mtume wa kweli wa Mwenyezi Mungu.
Isipokuwa wale waliopania kumfanyia uadui Mtume(SAW) wakabadilisha na kuongeza katika bishara hizo. Juu ya hayo, katika vitabu hivyo, bado zingalimo bishara zinazoshuhudia ukweli wa Utume wake Mohammad (SAW).

ZIFUATAZO NI BAADHI YA BISHARA HIZO:-

 

KATIKA TAURATI (TORAH)

Katika Taurati imeelezwa kwamba Nabii atatokea Makka (Nyumba alokuwa akiishi Qaydara), mmoja wa wana wa Ismail (AS),  na Qaydara huyu aliishi Makka kama inavyoelezea Taurati.
Na kwamba jina lake litanyanyuliwa hapo, na kwamba anapanda ngamia na anapigana kwa  panga na kwamba atashinda yeye na watu wake,  na kwamba atabarikiwa kila siku (na hivi ndivyo wafanyavyo Waislamu wanapotoa shahada (katika Sala zao), na kwamba wafalme wa Yemen watakuja kwake wakiwa na wanyama wa sadaka,  na kwamba alama ya utukufu wake yenye ukubwa wa yai la njiwa ipo juu ya bega lake, (alama hii ilikuwepo begani mwa Mtume (SAW)) .
Maelezo haya hayalingani na mwengine yeyote isipokuwa Muhammad (SAW).
Vile vile imeandikwa katika Taurat kwamba MwenyeziMungu amejitukuza juu ya  watu mahali patatu:-
1)  SINAI:   Alipoteremshiwa Nabii Musa(AS) Taurati
2)  SAIYR:  (Jabali katika Palestina) Alipoteremshiwa Nabii Issa (AS) Injili.
3) MAKKA: (Parani) alipoteremshiwa  Mtume Muhammad(SAW) Qurani.
Taurati iliyo mikononi mwa Mayahudi hadi hivi sasa inasema;
"Bwana alitoka Sinai, akawaondokea kutoka Saiyr, aliangaza katika kilima cha Parani".
Parani ni jina la zamani la mji wa Makka kama ilivyoelezwa katika Taurati.
Kumbukumbu la Taurati 21:22.

Wanavyuoni walikwisha eleza kwamba hata Qurani imezungumzia hayo katika kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"Naapa kwa Tini na Zaituni (miti hii inaota Palastina).
Na kwa mlima Sinai (alipopewa kitabu Nabii Musa).

Na kwa mji huu wenye amani (Makka alipopewa utume Nabii Muhammad (SAW)."
(Suratul - Tiyn -1-2-3)

KATIKA INJILI

Katika injili ya Barnaba mlango wa 220 imeeleza hivi:
"Issa (AS) Aliwaambia wafuasi wake:
"Haya yatabaki mpaka atakapokuja Muhammad Mtume wa MwenyeziMungu ambaye atakapokuja atazikashifu hizi hadaa kwa wale wanaoamini sheria za MwenyeziMungu )".

Na katika Yohana:16/7-14 - Injili inasema kwamba Issa (AS) aliwaeleza watu wake juu ya Nabii atakayekuja baada yake, aliposema:
"Hata hivyo bado ningali ninayo mengi ya kuwaambieni, lakini hamwezi kustahamili hivi sasa, lakini atakapokuja huyo roho wa kweli atawaongoza awatie katika kweli yote, kwa maana hatonena kwa shauri lake mwenyewe, bali kila atakalosikia atanena na atakuelezeeni juu ya yatakayokuja yote".
MwenyeziMungu amesema:-
"Na (wakumbushe) aliposema (Nabii)Issa bin Maryam (kuwaambia Mayahudi) "Enyi wana wa Israil)! Mimi ni Mtume wa MwenyeziMungu kwenu nisadikishaye yaliyokuja kabla yangu katika Taurat na kutoa habari njema ya Mtume atakaekuja nyuma yangu ambaye jina lake litakuwa Ahmad "(Muhammad na maana ya majina mawili hayo ni moja, na maana yake ni mwenye kuhimidiwa kwa maneno yake mazuri), lakini alipowajia kwa hoja zilizo wazi walisema: "Huu ni udanganyifu ulio dhahiri."
Suratus Saff - 6

KATIKA VITABU VYA WAHINDU

Katika kitabu kiitwacho (Alsa Mafida), kitabu kitakatifu cha Mahindus (Mabaniani), huko Bara Hindi, katika Ibara ya sita na ya nane katika sehemu ya pili imeandikwa ifufatavyo:-
"Ahmad anapokea sheria kutoka kwa Mola wake nayo imejaa hekima".
Na katika kitabu kiitwacho (ADRUW AFIDAM) kitabu kingine kitakatifu kwa Wahindu imeandikwa:-

"Wakati huo utakapofika ataletwa mgeni aitwaye Mahaamid[2] atakayejulikana kuwa ni Mwalimu wa ulimwengu[3] na Mfalme, akitahirisha kwa Tano zilizo tahiri[4]
"Enyi watu sikieni mfikiri, ataletwa Muhammad juu ya migongo ya watu  na utukufu wake utashukuriwa mpaka Peponi naye ni mwenye Kuhimidiwa."

Na katika kitabu kiitwacho (PHUSH PRANIM) ambacho  pia ni miongoni mwa vitabu vitakatifu kwa Kihindu imeandikwa;
Hii ni katika juzuu ya pili  sehemu ya tatu ibara ya tatu na kuendelea[5]

KATIKA VITABU VYA WAMAJUSI

Imeandikwa katika kitabu kiitwacho ‘ZINDA AFASTA’ kwamba Mungu atamleta Mtume na wasfu wake  ni huu:
Rehma kwa walimwengu
Atapambana na adui aitwaye Abu Lahab na atawalingania watu wamwabudu Mungu Mmoja.
Haya yanasadikisha kauli ya MwenyeziMungu isemayo:
"Wale tuliowapa kitabu wanamjua kama wanavyowajua watoto wao".
(Al - Baqarah -146).
Mayahudi na manasara ndio Ahlul Kitab (Watu walioteremshiwa vitabu), lakini Mtume (SAW) ametuamrisha tuwape heshima ya Ahlu Kitab Wahindu na Wamajusi (Zorosti), isipokuwa tusile nyama walochinja wala tusiowe wanawake wao, na Mwenyezi Mungu anajuwa zaidi, lakini huenda sababu yake ikawa ni kule kupitiwa na miaka mingi kwa vitabu vyao pamoja na mikono mingi iliyobadilisha na kugeuza yaliyomo.
Ubashiri huu ndio ulosababisha kusilimu kwa wingi kwa Mayahudi wa zamani, Manasara, Majusi na Wahindu.


TABIA NA MWENENDO WAKE UNAOSHUHUDIA UKWELI WA UTUME WAKE(SAW)

Yeyote atakayechukuwa jukumu la kuongoza watu, lazima atachunguzwa na watu ili wazijuwe Tabia na Mwenendo wake, na hautopita muda mrefu, watu watajuwa. Hasa mtu huyo atakapoingia katika mapambano baina ya udhaifu na nguvu, hofu na amani, ufakiri na utajiri, kuwa na wafuasi wachache dhidi ya wafuasi wengi, shida na utulivu kama ilivyomtokelea katika maisha yake Mtume (SAW) .
Tukiizingatia hali aloishi nayo, tutaiona kuwa ni hali asiyoweza kuwa nayo mwengine isipokuwa Nabii.

Miongoni mwa Hali hizo ni:-

1)    UKWELI

Watu wake walikuwa wakimjuwa kuwa ni Msema kweli, na hata kabla hajapewa Unabii alikuwa akijulikana kwa jina la; 'MSEMA KWELI, MWAMINIFU'.
Abu Jahal aliwahi kumwambia;
"Sisi hatukukadhibishi wewe isipokuwa tunayakadhibisha hayo ulokuja nayo".
Ndipo MwenyeziMungu alipoteremsha kauli yake:-
"Basi wao hawakukadhibishi wewe lakini madhalimu hao wanakanusha hoja za MwenyeziMungu".
(Al An- Am -33).
Alijulikana kuwa ni Msema kweli katika kila jambo lake, hata anapofanya mzaha (SAW). Na hii ni tabia isiyopatikana isipokuwa kwa Nabii aliyeletwa na MwenyeziMungu.

2)    KUTIMIZA KWA UKAMILIFU YOTE ANAYOWALINGANIA WATU

Nafsi ya Mwanaadamu kwa kawaida huchukizwa kutenda jambo kwa kulazimishwa, hasa mtu huyo anapokuwa keshajimakinisha baina ya watu.
Tukiichunguza hali alokuwa nayo Mtume(SAW), tutaona kuwa alikuwa mchaMungu kupita wote na mkamilifu wa tabia njema kupita wote, na alikuwa akifanya ibada nyingi kupita wote.
Alikuwa akifunga sana hata watu wake walimdhani hali chakula, na alikuwa akisali usiku mpaka miguu yake ikivimba.

Bibi Aisha (RA) aliwahi kumuuliza;
"Kwa nini unafanya yote hayo na MwenyeziMungu  keshakughufiria madhambi yako yalotangulia na yanayokuja?"

Mtume(SAW) Akajibu;
"Basi nisiwe mja mwenye kushukuru?"
Bukhari na Muslim
Alikuwa akitumia mali yake yote katika njia ya Mwenyezi Mungu, hakuwa akibakisha chochote nyumbani kwake, na alipokufa, ngao yake ilikuwa imewekwa rehani kwa Myahudi.
Kutokana na Utajo  wa Mwenyezi Mungu(Dhikri) pamoja na Dua zilizohifadhiwa kutoka kwake kunashuhudia kuwa alikuwa anamdhukuru Mola wake kila wakati usiku na mchana na katika kila jambo analotenda.
Alifanya yote haya akiwa ni Mtume wa MwenyeziMungu, Mlinganiaji wa watu katika dini ya Mwenyezi Mungu, Mkuu wa majeshi ya Waislamu. Na pale vita vikipamba moto, Waislamu walikuwa wakijikinga kwa kujificha nyuma yake(SAW). Alikuwa akipigiwa mfano katika ushujaa na ujasiri, na haya yalionekana katika vita vya Hunayni alipopigana na kuthibiti Yeye na Masahaba wake mia moja tu, dhidi ya washirikina elfu, na MwenyeziMungu akawapa ushindi juu ya maadui.
Washirikina wa Makka walimtaka achague iwapo anataka apewe Mali kiasi atakacho pamoja na Heshima na Ufalme ili aiache dini yake au achaguwe vita na kutiwa adabu iwapo atashikilia kutaka kuitangaza dini yake.
Akachaguwa kuufikisha ujumbe alopewa na Mola wake.
Na pale dunia nzima ilipokuwa chini ya amri yake, iliteremka kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"Ewe Mtume waambie wake zako ikiwa mnapenda maisha ya (hii) dunia na uzuri wake (mimi sinayo na siwezi kukulazimisheni kukaa na mimi (katika hali ya ufakiri); basi (mkipenda nikuacheni), njooni nitakupeni kitoanyumba na kukuacheni mwacho mzuri."
(Al Ahzab -28).
Lakini (wake zake) wote wakachagua kuishi na Mtume wa Mwenyezi Mungu(SAW), wakawa wachaMungu na kuyaacha matamanio na mapambo yote katika maisha yao ya hapa duniani.
Alikuwa mfano wa hali ya juu katika kuhukumu baina ya watu kwa uadilifu, akasema;
"Lau angeiba Fatima binti Muhammad, basi Muhammad angemkata mkono wake".
Alikuwa mfano wa hali ya juu katika kila jambo, ndio maana kila mmoja katika umma wake anajaribu kuigiza mwenendo wa Mtume wa MwenyeziMungu (SAW) katika kila nyanja za maisha yake na wala hapana anayeweza kuifikia daraja yake.
Bila shaka mkusanyiko uliokamilika wa mfano wa hali ya juu kama huu katika kila nyanja ya maisha, haupatikani isipokuwa kwa Mtume aliyeletwa na MwenyeziMungu, aliyeshuhudia Mola wake kwa kauli Yake isemayo;
"Hakika wewe ni mwenye tabia tukufu."
(Al Qalam 21)..
Na MwenyeziMungu aliyetukuka akataka awe mfano mwema baina ya watu, aliposema:-
"Bila ya shaka mnao mfano mwema (ruwaza nzuri) kwa Mtume wa MwenyeziMungu  kwa mwenye kumuogopa MwenyeziMungu na siku ya mwisho na kumtaja MwenyeziMungu sana".
(Al Ahzab -21)

ALIVYOUSIMAMIA UJUMBE NA KUUFIKISHA KWA WATU

Mtume (SAW) ameifanya kazi yake kwa ukamilifu na ameufikisha ujumbe kwa watu  kama alivyotakiwa.
Wakati mwingine alikuwa akiwaendea watu maalum au huwaalika watu chakula, na mara nyengine hujitolea kuyaendea makabila mbali mbali huku akiwa na subira juu ya yale yanayomkuta, na kabila moja baada ya moja humkatalia. Wakati mwingine huwaita watu ili akutane nao au huwaendea pale walipo, na mara nyingine huwatuma walinganiaji katika Sahaba zake (RA), na  mara nyingine hutuma wajumbe kwa wafalme na ma gavana, mara nyingine hupigana Jihadi dhidi ya wale wanaowazuia watu kuilingania njia ya MwenyeziMungu.
Makafiri walipambana na uenezi huu pamoja na waenezaji kwa kila namna ya ukatili, nguvu na udhia.
Maqureish wakati mwingine walikuwa wakiwafanyia mzaha Mtume (SAW) na Sahaba zake (RA), kisha ghafla wanawavamia baadhi ya Waislamu na kuwaunguza kwa moto, kuwauwa au kuwaadhibisha. Waliwapiga pande Waislamu na kuwazunguka wakiwemo katika nyumba za Abu Talib kwa muda wa miaka mitatu, hata iliwabidi Waislamu wale ngozi na miti. Udhia ukazidi na Masahaba wa Mtume(SAW) ikawabidi wahame na kukimbilia  Uhabeshi (Ethiopia) mara mbili, kisha wakahamia Madina.
Maqureish wakafanya njama ili wamuuwe Mtume wa MwenyeziMungu(SAW), lakini MwenyeziMugu akamwamrisha ahame ili aokoke  na hila zao.
Alikuwa akiwaelezea watu yote aliyotakiwa na MwenyeziMungu ayaeleze. Alitujulisha hata yale yaliyo na makatazo kwake yeye binafsi kutoka kwa MwenyeziMungu:
Mfano wa kauli ya MwenyeziMungu:
"Alikunja (Mtume ) paji na akageuza uso.
Kwa sababu alimjia kipofu.
Na nini kilichokujulisha (ya kuwa huyo Sahaba pofu hahitaji mawaidha mapya?)  Labda yeye atatakasika (kwa kusikia mawaidha mapya).
Au atakumbuka (aliyoyasahau). Ukumbusho huo upate kumfaa.
Ama ajionaye hana haja (ya dini).
Wewe ndie unayemshughulikia?
Na si juu yako kama hakutakasika.
lakini anayekukimbilia.
Naye anaogopa.
Wewe unampuuza (Usifanye hivyo)".
(Abasa -1-10).
Aliambiwa haya kwa sababu Mtume(SAW) alipokuwa akiwalingania baadhi ya viongozi wa makafiri alijiwa na kipofu Mwislamu aitwae Ibn Ummi Maktoum akimuuliza masuali, na Mtume (SAW) alichukizwa kwa kuulizwa masuali wakati alipokuwa akijaribu kuwasilimisha wakubwa wa makabila ambao wangelisilimu wao pamoja na wafuasi wao ingepatikana kheri kwa Waislamu.
Mtume (SAW) hakumfanyia lolote la zaidi kipofu huyo isipokuwa alikunja uso wake tu. Na Ibn Ummi Maktoum kwa vile ni kipofu, hawezi kuuona uso wa Mtume (SAW) ulokunjwa na kwa hivyo hakuudhika.
Lakini MwenyeziMungu akamteremshia Mtume(SAW) makatazo, na akayafikisha makatazo hayo kama yalivyoteremshwa.
Lengo la Mtume (SAW) katika maisha yake yote lilikuwa ni kuyafikisha yale aliyoamrishwa na Mola wake bila ya kujali ukubwa wa taabu au vikwazo atakavyopambana navyo.

Katika Hijja yake ya mwisho (Hijjatul Wadaa) aliwauliza Waislamu;
"Je! nimefikisha?"
Wakashuhudia kuwa amewafikishia kikamilifu dini ya MwenyeziMungu;

Kisha akasema:-
"MwenyeziMungu shuhudia".
Hakika ya hali yake ilivyokuwa katika kila nyanja ya maisha yake inashuhudia kuwa sifa kama hizi hawezi kuwa za mtu wa aina nyingine isipokuwa ni sifa za Mtume wa MwenyeziMungu (SAW) na mjumbe Wake.


HALI ZA WAFUASI WAKE NA MAADUI ZAKE ZINAZOTHIBITISHA

UKWELI WA UJUMBE WAKE

Uhodari wa mwalimu unaonekana katika wanafunzi wake, na ustadi wa mkufunzi unaonekana kwa wale anaowapa mafunzo, na ukweli wa Mtume unadhihirika katika wafuasi wake, kwa sababu wao ndio waloishi naye, akawalea, akawatakasa na kuwafunza.
Atakayezingatia hali za Masahaba (RA) atauona ukweli wa wasfu alowapa Mwenyezi Mungu aliposema:-
"Nyinyi ndio umma bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu".
(Al -Imran -110)
Mataifa yote ya ulimwengu wakati ule yalishuhudia kwamba Waislamu walikuwa ni Umma bora ulodhihirishiwa watu.
Hii ni kwa sababu ya kawaida ijulikanayo kwamba nchi yoyote au umma wowote ukifanya vita na kuiteka nchi nyingine basi kuteka huko kunasababisha chuki na wivu baina ya mataifa hayo, na haya yanaonekana mpaka hivi sasa baina ya wakoloni na wanaowatawala.
Lakini kawaida hii ilitoweka kwa wafunguzi wa Kiislamu waliokuwa mabwana wa ulimwengu wakati wao.
Ushindi wa Waislamu baada ya kuziteka nchi hizo ulisababisha mapenzi, nusura, utiifu na mchanganyiko baina ya Waislamu na wengine hata mataifa hayo yaliyoshindwa na Waislamu yalikuwa yakimshukuru MwenyeziMungu kwa kuletewa wafunguzi hawa wa Kiislamu.
Ukiitafuta sababu utaona kwamba mapambano yaliyopo baina ya watu ni kugombania matamanio ya dunia, lakini Waislamu walijitolea kukataa matamanio ya dunia kwa ajili ya kuwafurahisha watu huko Peponi, na hii ni kwa sababu waliiamini Akhera kama ilivyopaswa kuaminiwa na kwa sababu imani na mwenendo wao huo yalikuwa ni matunda ya usadikisho kamili wa ushahidi alokuja nao Mtume wa MwenyeziMungu (SAW) juu ya ukweli wa ujumbe wake na kwa matendo yake yaliyoeneza imani katika maisha yake (SAW).

MAADUI ZAKE

Baada ya kumfanyia inda muda mrefu sana, maadui zake wakageuka kuwa ni walinzi wake wakubwa kabisa na wengi miongoni mwa Ahlul Kitab wa mwanzo nao pia wakasilimu.
Yalipatikana yote haya baada ya kumsadiki Mtume wa MwenyeziMungu (SAW) na kumwamini.
         

KUFAA KWA SHERIA (ZA KIISALMU ) ZAMA ZOTE NA MAHALI POPOTE

Utungaji wa sheria na nidhamu yoyote ile unategemea elimu kamili juu ya yule anayetungiwa sheria hiyo na mazingara yanayoambatana naye.
Mwanadamu hauelewi uhakika wa roho yake na yale atakayokumbana nayo siku za usoni, na hii ndiyo sababu ya kushindwa kwake kutunga sheria na kanuni zilizo thabiti atakazoweza kuzitumia wakati wowote na zama zozote.
Lakini muumbaji Subhanahu wa Taala ndiye mwenye kujua uhakika wa kuumbwa kwa mwanadamu.

MwenyeziMungu amesema:-
"Oh! asijue aliyeumba! naye ndiye avijuaye visivyojulikana na vinavyojulikana".
(Suratul -Mulk -14)
Na Yeye ndiye aliyekizunguka kila kitu kwa kukijuwa, anayajuwa yaliyopita na yatakayokuja, na hii ndiyo sababu mwanadamu hawezi kuja na sheria iliyo thabiti, lainifu na inayoweza kunasibiana na kila zama na kila mahali, isipokuwa mtu huyo awe amepewa sheria hiyo na Mola wake Subhanahu wa Taala.
Waislamu waliitawala Mashariki ya ardhi na Magharibi yake kwa karne nyingi, na sheria ya Kiislamu ilifaa  kuhukumu karne zote hizo katika mazingara na sehemu mbali mbali.
Sheria ya Kiislamu imeweza kubaki hadi wakati wetu huu juu ya udhaifu wa Waislamu, na Umoja wa Mataifa umekubali kuitumia sheria hii kuwa ni moja katika misingi ya kutunga sheria zao ulimwenguni wakati kanuni za Kirusi na za Kimarekani hazitambuliwi kama ni msingi wa kanuni za Ulimwengu.
Na wataalamu mbali mbali wa kanuni ulimwenguni (wasiokuwa Waislamu) wamekubali kuwa sheria ya Kiislamu inafaa kwa kila zama.
Dr Ezekio Ensaba Tohin - Mmoja wa wataalamu wa kanuni ulimwenguni amesema;
"Dini ya kiislamu inakubaliana na kila kinachowalazimikia watu, kwa hivyo inaweza kustawi na kujiendeleza na kutumika bila ya kudhoofika kupitia karne na karne huku ikijihifadhi kwa nguvu zake zote za maisha pamoja na ulaini wake. Dini hii imeupa ulimwengu sheria iliyo thabiti kuliko zote. Sheria yake ni bora sana kuliko sheria zinazotumika katika nchi za Ulaya."
Mkutano wa ulimwengu wa sheria uliofanyika huko Lahai mwaka 1932, ndio ulioutaka Umoja wa Mataifa uikubali sheria ya Kiislamu kutumika kama ni msingi katika misingi ya kutunga kanuni za ulimwengu baada ya kukiri kwa wataalmu wa kanuni  ulimwenguni juu ya utukufu wa sheria hiyo na kwa ajili ya faida kwa watu katika wakati huu.
     Ama mkutano wa kimataifa juu ya ulinganishi wa kanuni uliofanyika huko Paris mwaka 1952, ulilitaka baraza la ulimwengu la kutunga sheria uruhusu kufanyika mkutano wa kimataifa juu "Fiq-hi ya Kiislamu" kila mwaka badala ya kila miaka kumi, na sababu waliyotoa ni kuwa wanataka kujifunza zaidi na kupata faida nyingi kutokana na kuidurusu sheria ya Kiislamu, na wakasema katika mkutano wao huo:
"Kutokana na yaliyothibiti kwa walioshiriki katika mkutano juu ya  faida iliyopatikana katika utafiti uliofanywa katika "Wiki ya Fiq hi ya Kiislamu", na kutokana na yaliozungumzwa katika utafiti huu pamoja majadiliano, imetuthibitikia kwamba Fiq hi ya Kiislamu imesimama katika misingi ilio na kima kikubwa kabisa, na haya ni yenye uhakika usio na shaka yoyote juu ya manufaa yake, na kwamba misingi ya hitilafu iliyopo katika sheria hii kuu inatokana na utajiri (hazina) wa rai mbali mbali za fani ya sheria (fiq-hi) ambayo huipa sheria hii uwezo wa kunasibiana na hali zote za maisha ya kisasa kwa ulainifu wake mkubwa.
Kwa hivyo wajumbe wa mkutano wanatoa mapendekezo yao kuwa; " Wiki ya Fiq-hi ya Kiislamu iendeleze kazi yake kila mwaka."
Basi atawezaje mtu asiyejua kusoma wala kuandika, aliyekuja miaka elfu moja mia nne iliyopita, aje na sheria kama hii, iwapo mtu huyu si Mtume aliyeletwa na Mola wake?
Utashangazwa kuwaona wajinga miongoni mwa Waislamu wanaotaka sheria hii ya MwenyeziMungu ifutwe na kubadilishwa na sheria za wanadamu.










KUITAKASA IBADA


KWANZA: NINI IBADA ?

Ibada ni jina lililokusanya kila anachokipenda MwenyeziMungu na kuridhika nacho na akakiamrisha.
Kwa hivyo kila alichotuamrisha MwenyeziMungu kukitenda ni ibada, na kila alichotukataza kujiepusha nacho ni ibada. Ama matendo ya kawaida yaliyoruhusiwa na sheria kama vile kula, kunywa na kuvaa huwa ni ibada yakikusudiwa kufuata amri ya MwenyeziMungu na kusaidia katika kumtii MwenyeziMungu.
Ibada haisihi isipokuwa iwe halisi kwa ajili ya MwenyeziMungu, ikubaliane na sheria yake na ikusanye baina ya utiifu mkubwa na unyenyekevu kwa MwenyeziMungu pamoja na ukamilifu wa kumpenda.
MwenyeziMungu katika kuwasifia walioamini, anasema:-
"Lakini walioamini wanampenda MwenyeziMungu zaidi sana".
(Al - Baqaraha -165)
Kwa ajili ya Ibada ndiyo Mwenyezi Mungu ameumba viumbe na kuwapelekea Mitume.
MwenyeziMungu amemdhalilishia mwanadamu vyote vilivyo mbinguni na ardhini ili naye avitumilie hivyo katika kumtii Yeye Subahanahu wa Taala.
MwenyeziMungu anasema:
"Jee! Hamuoni ya kwamba MwenyeziMungu amekutiishieni vilivyomo mbinguni na vilivyomo ardhini, na akakukamilishieni neema zake zilizo dhahiri na za siri".
(Luqman -20).
Na anasema:-
"Sikuwaumba majini na watu ila wapate kuniabudu."
(Adh -Dhariat -56)
Na akasema:-
"Na bila ya shaka tulimpeleka Mtume katika kila umma ya kwamba mwabuduni MwenyeziMungu na mwepukeni mwovu (Iblisi au kila kinachoabudiwa kisichokuwa MwenyeziMungu). "Basi wako miongoni mwao ambao MwenyeziMungu amewaongoa, na wako miongoni mwao ambao upotofu umethubutu juu yao".
(An - Nahli -36)

Yafuatayo ni Masharti Mawili Ya Msingi Na Haikubaliwi Ibada Yoyote Bila Ya Kuyatimiza Masharti Hayo:-


KUITAKASA KWA AJILI YA MWENYEZIMUNGU

Na maana yake ni kuwa; Ibada yoyote isikusudiwe kwa ajili ya mwengine asiyekuwa Allah, na kusudi lake liwe kwa ajili ya kutaka radhi za MwenyeziMungu Subhanahu wa Taala.
MwenyeziMungu anasema:-
"Wala hawakuamrishwa ila kumuabudu MwenyeziMungu kwa kumtakasia dini, wawache dini za upotofu na wasimamishe Sala na kutoa Zaka, hiyo ndiyo dini liliyo sawa."
(Al - Bayinah -5)

  KUMFUATA MTUME (SAW)

Nako ni kutomuabudu MwenyeziMungu isipokuwa kwa njia aliyotufundisha Mtume wake(SAW).
MwenyeziMungu anasema:-
"Sema", Ikiwa nyinyi mnampenda MwenyeziMungu basi nifuateni (hapo) MwenyeziMungu atakupendeni na atakughufirieni madhambi yenu."
(Aali - Imran -31)
Na anasema:-
"Oh! Wana washirika (wa MwenyeziMungu) waliowawekea dini asiyoitolea MwenyeziMungu ruhusa (yake)?"
(Ash - Shuraa -21)
Kwa hivyo anayesali Magharibi raka nne kwa mfano, basi sala yake inabatilika na anayesali raka tatu inakuwa sawa. Hii ni kwa sababu njia ya pili ndiyo aliyotufundisha Mtume(SAW), ama ya kwanza  ni kinyume na mafundisho ya Mtume (SAW).
Na Mtume (SAW) amesema:-
"Atakayeongeza jipya katika amri yetu hii jambo ambalo halimo, basi halitakubaliwa."
Bukhari na Muslim

PILI: AINA ZA IBADA

Ibada sahihi inapatikana pale unapopatikana unyenyekevu kamili tena halisi ndani na nje yake mwanadamu, itikadi iwe moyoni na kwa kutamka na kwa vitendo. Vyote hivyo vikiwa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala.

IBADA ZIKO AINA NYINGI; MIONGONI MWAKE:


IBADA ZA ITIKADI

1)            Kuamini Kuwa Hapana Mola Anayepaswa Kuabudiwa Isipokuwa Allah Na Kwamba Muhammad Ni Mtume Wa Allah:-
Haya hupatikana kwa njia ya elimu sahihi  inayoondowa kila aina ya shaka.
MwenyeziMungu anasema:-
"Juwa ya kwamba hakuna aabudiwaye kwa haki ila  MwenyeziMungu na omba maghufira kwa dhambi zako."
(Muhammad - 19)
Na anasema:-
"Je! Anayejua kwamba yaliyoteremshwa kwako kutoka kwa Mola wako ni haki (akayafuata basi) ni kama kipofu? Wenye akili ndio wanaozingatia".
(Raad -19).

2)            Kumpenda MwenyeziMungu Aliyetukuka:
MwenyeziMungu anasema:
"Lakini walioamini wanampenda MwenyeziMungu zaidi sana”.
(Al -Baqraha - 165)
Nayo ni mapenzi yaliyofungamana na udhalilifu na unyenyekevu pamoja na kusalimu amri, mapenzi ambayo hayapatikani isipokuwa kwa kufuata alokuja nayo Mtume (SAW).
MwenyeziMungu anasema:-
"Sema; 'Ikiwa nyinyi mnampenda MwenyeziMungu basi nifuateni, hapo MwenyeziMungu atakupendeni."
(Al - Imran 31)
Katika ukamilifu wa kumpenda MwenyeziMungu ni kumpenda Mtume wake (SAW) na kuipenda dini ya Kiislamu.
Ama kuwapenda watoto na jamaa sio ibada kwao maana hulazimiki kuwa mnyenyekevu na kusalimu amri kwao. Na juu ya hayo kwa Muislamu mapenzi hayo hayawi makubwa kuliko mapenzi yake juu ya MwenyeziMungu na Mtume wake (SAW). Na iwapo mapenzi ya MwenyeziMungu na Mtume wake yatapambana na mapenzi mengine basi pendo lisilokuwa la MwenyeziMungu litatoweka katika moyo wa Muislamu.
MwenyeziMungu mtukufu anasema;
"Sema kama baba zenu na wana wenu na ndugu zenu na wake zenu na jamaa zenu na mali mlizozichuma na biashara mnazoogopa kuharibikiwa na majumba mnayoyapenda (ikiwa vitu hivi) ni vipenzi zaidi kwenu kuliko MwenyeziMungu na Mtume wake na kupigania dini yake, basi ngojeni MwenyeziMungu alete amri yake na MwenyeziMungu hawaongozi watu waasi(njia iliyonyoka)."
(At - Tawba - 24)

3)            Kumuogopa MwenyeziMungu Pamoja Na Kuwa Na Tamaa Katika Rehma Yake:
MwenyeziMungu anasema:-
"Jee! afanyae ibada nyakati za usiku kwa kusujudu na kusimama na kuogopa akhera na kutarajia rehema ya Mola wake (ni sawa na asiyefanya hayo) sema; "Jee! wanaweza kuwa sawa wale wanaojua na wale wasiojua?"
Az - Zumar -9
MwenyeziMungu akatoa wasfu wa wasioamini aliposema:-
"Na ambao wanaiogopa adhabu itokayo kwa Mola wao hakika adhabu ya Mola si ya kusalimika nayo mtu (mbaya)."
Al - Maarij - 27-28
Huenda mtu akawa na hofu juu ya baadhi ya mambo ya kidunia, lakini hofu hii sio ibada juu ya yale anayoyaogopa, maana hofu hiyo ni ya kimaumbile ambayo mwenye kuamini anaamini kuwa MwenyeziMungu ndiye aliyemkadiria, na hofu hiyo haifikii daraja ile ya kumuogopa Mola wake, maana anaamini ya kuwa MwenyeziMungu anaweza kumuepusha na kila ovu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na kama MwenyeziMungu akikugusisha madhara (taabu) basi hakuna yeyote awezaye kuyaondoa ila Yeye; na kama akikugusisha kheri (hakuna awezaye kuiondoa ila Yeye tu  peke Yake ) Yeye ndiye mwenye uwezo wa juu ya kila kitu"    
Al - Anam -17

4)            Kurejea Kwa MwenyeziMungu:
Nako ni kukimbilia kufanya yanayomridhisha MwenyeziMungu na kurudi kwake na kuomba maghufira na kutubia.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na rejeeni kwa Mola wenu na mnyenyekeeni kwake kabla ya kukujieni adhabu kisha hamtanusurika. Na fuateni yaliyo bora katika yale yaliyoteremshwa kwenu kutoka  kwa Mola wenu kabla ya kukujieni adhabu kwa ghafla na hali hamtambui."
Az Zummar -54-55
Katika kuelezea wasfu wa Waislamu, MwenyeziMungu pia anasema:-
"Na ambao wanapofanya uchafu (kufanya dhambi kubwa) au kudhulumu nafsi zao (kwa kufanya dhambi ndogo) hukumbuka MwenyeziMungu na kuomba msamaha kwa dhambi zao. Na nani anayeghufiria dhambi isipokuwa MwenyeziMungu? Na hawaendelei na (maovu) waliyoyafanya hali wanajua (kuwa hayo ni maovu)".
Aali - Imran –135



5)            Kumtegemea MwenyeziMungu Na Kumuomba Msaada:
Uhakika wa kutegemea: Ni ukweli wa moyo unaomtegemea MwenyeziMungu katika kutafuta yenye manufaa na kujiepusha na madhara katika mambo ya kidunia na ya akhera.
MwenyeziMungu amekadiria na akauwekea ulimwengu nidhamu kwa kukadiria kila kitu, akauwekea mwenendo maalum na akaziwekea sababu zake,  ili tumuabudu kwa kuzifuata hizo sababu.
Miongoni mwa sababu kubwa kabisa ni kumtegemea MwenyeziMungu:

MwenyeziMungu anasema:
"Na anayemtegemea MwenyeziMungu, yeye humtoshea. Kwa yakini MwenyeziMungu anatimiza kusudi lake (lolote alitakalo; hakuna wa kumpinga). Hakika MwenyeziMungu amekwisha kiwekea kila kitu kipimo chake ".
At Talaq -3
Na anasema:-
"Ikiwa nynyi mumemuamini MwenyeziMungu, basi mtegemeeni yeye kama nyinyi ni Waislamu kweli."
Yunus - 84
Na anasema:-
"Na Waislamu wamtegemee MwenyeziMungu tu".
At Taghabun -13
MwenyeziMungu akawafaradhishia waja wake katika kila Sala waseme:
"Wewe tu ndie tunayekuabudu na Wewe tu ndie tunayekuomba  msaada".
Fatiha -5)
Na Mtume (SAW) akasema:
<< Ukitaka kuomba msaada muombe MwenyeziMungu >>.
(Sehemu ya hadithi sahihi iliyotolewa na Ahmad na Al Tirmidhy ilopokelewa kutoka kwa Ibn Abbas)
     

IBADA ZA MATAMSHI


1) Kuzitamka Shahada Mbili
Hauwi sahihi Uislamu  wa mtu iwapo hajazitamka shahada mbili, isipokuwa bubu ambaye vinatosheleza vitendo vyake vitakavyoonyesha dalili ya imani yake.
 Mtume (SAW)amesema:
<<Nimeamrishwa nipigane vita mpaka watu washuhudie kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa isipokuwa Allah na kwamba Muhammad ni Mtume wa MwenyeziMungu na wasimamishe Sala na Watoe Zaka. Watakapotimiza hayo watakuwa wamezuilika kwangu damu zao na mali zao ila kwa haki ya Uislamu [6]na  hesabu yao itakuwa kwa MwenyeziMungu>>.
(Bukhari na Muslim). 
  
1)     Kumdhukuru(kumtaja) MwenyeziMungu, Kumsabihi(kumtukuza) na Kumwomba Maghufira
MwenyeziMungu anasema:
"Enyi mlioamini! Mkumbukeni MwenyeziMungu kwa wingi na mtukuzeni asubuhi na jioni".
(Al - Ahzab -41 -42)

Na akasema:-
"Na ili muombe msamaha kwa Mola wenu, kisha mtubie(mrejee) kwake.  Atakustarehesheni kwa starehe nzuri mpaka mda maalum (mtapoondoka ulimwenguni).  Na atampa (akhera) kila mwenye fadhila, fadhila yake, na kama mtakengeuka basi nakukhofieni adhabu  ya (hiyo) siku kubwa."
(Hud-3)
   Na akasema:
"Basi (hapo) mtakase Mola wako pamoja na kumsifu na umuombe maghfira (msamaha) ; hakika Yeye ndiye Apokeaye toba ".
(Nasr -3)

   3) Dua  Na Kuomba Msaada
Atakayeomba dua, au msaada, hatokuwa mwenye akili (iwapo atamwomba asiyemsikia) isipokuwa huyo anayemuomba awe ni mwenye kumsikia na kuwasikia wengine kila wakati, kila mahali na kwa kila lugha.
Hatokuwa mwenye akili isipokuwa awe na yakini kwamba yule anayemuomba anao uwezo kwa njia za ghaibu wa kulijibu ombi lake na kumfariji dhiki zake, na awe na uwezo wa kimiujiza unaoweza kufanya jambo lolote katika ulimwengu huu.
Mwenye uwezo  huu  hawezi  kuwa  mwingine  isipokuwa MwenyeziMungu. Hawezi kuyafanya  haya kiumbe chake chochote, aliye hai au aliyekwisha kufa.
Mwenye kuamini kwamba asiyekuwa MwenyeziMungu anao uwezo wa kufanya lolote katika hayo, kisha akamulekezea dua yake, basi atakuwa amefanya   kiendo cha Shirki.
MwenyeziMungu anasema:-
"Huyo ndiye MwenyeziMungu, Mola wenu, Mwenye ufalme, na wale mnaowaabudu kinyume chake, wao hawamiliki hata utando (ngozi) wa kokwa ya tende, kama mkiwaomba hawatakujibuni na siku ya kiyama watakataa ushirika wenu wala hatakuambia kama (akuambiavyo MwenyeziMungu) Mjuzi wa kweli kweli".
(Fatir - 13 - 14)
Na anasema:-
"Na Mola wenu akasema "Niombeni nitakujibuni”. Kwa hakika wale wajivunao kufanya ibada yangu bila shaka wataingia Jahannam, wadhalilike".
(Al - Muumin - Ghafir- 60).
Na akasema:-
"Na waja wangu watakapokuuliza hakika yangu Mimi niko karibu nao. Naitikia maombi ya muombaji anaponiomba. Basi waniitikie na waniamini ili wapate kuongoka".
Al - Baqarah - 186
Iwapo mjinga yeyote ataelekeza dua yake kwa mwengine asiyekuwa MwenyeziMungu, basi ni wajibu wa anayeelewa kumbainishia, na anapaswa huyo asiyeelewa kufuata na kuiokoa nafsi yake isiingie katika Shirki.

4) Kuapa Kwa Jina La MwenyeziMungu
   Mwislamu hali kiapo isipokuwa kwa jina la MwenyeziMungu, kwa sababu ya kumtukuza na kumheshimu.
Mtume wa MwenyeziMungu (SAW) amesema:
<<Atakae kula kiapo, ale kiapo kwa jina la MwenyeziMungu au anyamaze.>>
Bukhari, Muslim, Ahmad na Annasai
Atakaekula kiapo kwa asiyekuwa MwenyeziMungu, akamtukuza kama anavyotukuzwa MwenyeziMungu na akamwogopa kama anavyomuogopa MweyeziMungu basi atakuwa amefanya kitendo cha Shirki.
Mtume (SAW) amesema:-
<<Atakaekula kiapo kwa asiyekuwa MwenyeziMungu anakuwa keshafanya (kitendo cha) Shirk>>.
Attirmdhiy, Ibn Majah, Ahmad, Annasai, na Addarimy
Pia haijuzu mtu kuapa kwa 'Amana'.
Mtume (SAW) amesema:
<<Atakayeapa kwa Amana hayupo pamoja nasi>>.
Ahmad na Abu Daud.

5) Kulingania Watu Katika Njia Ya MwenyeziMungu, Kuamrisha Mema Na Kukataza Mabaya
   MwenyeziMungu anasema:-
"Ni nani asemaye kauli bora zaidi kuliko aitaye viumbe (viumbe) kwa MwenyeziMungu na (mwenyewe) akafanya vitendo vizuri na kusema: "Hakika mimi ni miongoni mwa Waislamu".
Haa - Miym - Sajdah (Fussilat -33 )
Na anasema:-
"Sema": Hii ndio njia yangu; ninaita (ninalingania) kwa MwenyeziMungu kwa ujuzi wa kweli; mimi (nafanya hivi) na (kila) wanaonifuata. Na MwenyeziMungu ametakasika na kila upungufu, wala mimi simo miongoni mwa wanaomshirikisha (MwenyeziMungu)".
(Yusuf - 108).
Na anasema;
"Na wawepo katika nyinyi watu wanaolingania kheri (Uislamu) na wanaoamrisha mema na wakakataza maovu na hao ndio watakaotengenekewa".
(Aal - Imran -104)

IBADA ZA VITENDO

1)       Kusimamisha Sala
MwenyeziMungu anasema:
 "Wala hawakuamrishwa ila kumwabudu MwenyeziMungu kwa kumtakasia dini, wawache dini za upotofu (upotevu) na wasimamishe Sala na kutoa Zaka, hiyo ndio dini iliyo sawa .
 (Suratul - Bayyinah - 5)
Na anasema katika kuelezea wasfu wa walioamini:
"Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi (hakuwasahaulishi) kumkumbuka MwenyeziMungu na kusimamisha Sala na kutoa Zaka, wanaiogopa siku ambayo nyoyo zitadahadari na macho pia",
(An - Nur -37).
Na anasema:
"Wale ambao tukiwamakinisha (tukiwaweka uzuri) katika ardhi, husimamisha Sala na wakatoa Zaka na Wakaamrisha yalio mema na Wakakataza yalio mabaya. Na marejeo ya mambo ni kwa MwenyeziMungu".
(Al - Hajj - 41).
Na anasema:-
"Na waamrishe watu wako kusali na uendelee mwenyewe kwa hayo. Hatukuombi riziki bali Sisi ndio tunaokuruzuku na mwisho mwema utawathubutukia wamchao Mungu."
(Taha - 132)

2) Kutoa Zaka
MwenyeziMungu anasema:-
"Wala hawakuamrishwa ila kumuabudu MwenyeziMungu kwa kumtakasia dini, wawache dini za upotofu(upotevu) wasimamishe Sala na watoe Zaka hiyo ndiyo dini iliyo sawa .
(Suratul - Bayyinah -5).
Na anasema:-
"Na simamisha Sala na toeni Zaka na kheri mtakazozitanguliza kwa ajili ya nafsi zenu mtazikuta kwa MwenyeziMungu  ………"
(Al Baqarah - 110)


Na anasema:-
"Lakini wale waliozama barabara katika elimu miongoni mwao (hawa waliopewa kitabu) na Waislamu (ambao wote hao) wanaamini yaliyoteremshwa kwako na yaliyoteremshwa kabla yako, na (wale) wanaodumisha Sala na kutoa Zaka na wanaomwamini MwenyeziMungu  na (wanaamini) Siku ya mwisho. Hao tutawapa malipo makubwa ".
(An - Nisaa -162)

2)       Kufunga mwezi wa Ramadhani
    MwenyeziMungu anasema:-
"Enyi mlioamini mmelazimishwa kufunga (Saumu) kama walivyolazimishwa waliokuja kabla yenu ili mpate kumcha Mungu".
(Al - Baqarah -183).
Na anasema:-
"(Mwezi huu mlioambiwa mfunge)  ni mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa katika (mwezi) huo hii Qurani ili iwe uwongozi kwa watu na hoja zilizo wazi wa uwongozi na upambanuzi (wa baina ya haki na batil) atakae kuwa katika mji katika huu mwezi (wa Ramadhani) afunge."
(Al - Baqarah - 185)
Na Mtume (SAW) amesema:-
<<Atakae funga Ramadhan kwa Imani na kwa (nia ya) kutaka Ridhaa za Mwenyezi Mungu, anasamehewa madhambi yake yaliotangulia >>.
Bukhari, Muslim, Abu Daud, Attirmdhyna, Ibni Majah,na Ahmad

4) Kuhiji Makka (Kaaba) Kwa Mwenye Uwezo
MwenyeziMungu anasema:-
"Na MwenyeziMungu amewawajibishia watu wafanye Hijja katika nyumba hiyo; yule awezaye kufunga safari kwenda huko na atakae kanusha (asende na hali ya kuwa anaweza ) basi MwenyeziMungu si mhitaji kuwahitajia walimwengu "
Aal - Imran -97).
Na anasema :-
"Na (tukamwambia) "Utangaze kwa watu habari za Hijja watakujia (wengine) kwa miguu na wengine juu ya kila mnyama aliyekonda (kwa machofu ya njiani) wakija kutoka njia ya mbali".
(Al - Hajj - 27).
Na Mtume (SAW) akasema :-
<<Uislamu umejengeka juu ya nguzo tano; kubaini kwa moyo na kutamka kwa ulimi kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa isipokuwa Allah, na Muhammad ni Mtume wa MwenyeziMungu, Kusimamisha Sala. Kutoa Zaka, Kuhiji Makka na Kufunga mwezi wa Ramadhani>>.
Bukhari na Muslim

2)        Kuhukumu Kwa Sheria Iliyoteremshwa na MwenyeziMungu
 Hana haki mtu yeyote ya kuwawekea wanadamu sheria, isipokuwa yule Aliyewaumba - Subhanahu wa Taala.
MwenyeziMungu anasema:-
"Fahamuni kuumba (ni kwake tu MwenyeziMungu) na amri zote ni zake (MwenyeziMungu) ametukuka kabisa MwenyeziMungu Mola wa walimwengu wote".
(Al -Aaraf 54).
Kwa hivyo mwenye kujipa yeye mwenyewe, au kumpa mtu mwengine haki ya kuwatungia wanadamu sheria na nidhamu ambazo MwenyeziMungu hajazitolea amri yake, atakuwa ametenda kitendo cha shirki na atakuwa amewalingania watu wamwabudu asiyekuwa MwenyeziMungu.

MwenyeziMungu anasema:-
"Oh! Wana washirika wa (MwenyeziMungu) waliowawekea dini asiyoitolea MwenyeziMungu  ruhusa (yake)?"
(Ashuraa - 21)
Na anasema:-
"Haikuwa hukumu ila hii ya MwenyeziMungu tu; ameamrisha msimuabudu yeyote yule isipokuwa Yeye tu".
Yussuf -40
     Kwa hivyo Mwislamu anatakiwa asalimu amri mbele ya sheria ya MwenyeziMungu na aitii sheria hiyo kwa nafsi iliyoridhika. 
MwenyeziMungu anasema:-
"Naapa kwa haki ya Mola wako, wao hawawi wenye kuamini (kweli kweli) mpaka wakufanye (wewe ndie) hakimu (mwamuzi) katika yale wanayokhitilafiania kisha wasione uzito nyoyoni mwa juu ya hukumu uliyoitoa, na wanyenyekee kabisa."
    (AN - Nisaa -65)
3)        Kuipigania Dini Ya MwenyeziMungu
"Enyi mlioamini! Jee! nikujulisheni juu ya biashara itakayokuokoeni na adhabu iumizayo?
(Basi biashara yenyewe ni hii): Muamini MwenyeziMungu na Mtume wake piganieni dini ya MwenyeziMungu kwa hali zenu na nafsi zenu, haya ni bora kwenu ikiwa mnajua (kuwa ni bora basi fanyeni)".
(As - Saff -10 11)
Na anasema:
"Jee! Mnadhani mtaingia Peponi hali MwenyeziMungu hajapambanua wale waliopigania dini ya MwenyeziMungu miongoni mwenu, na kuwapambanua wale walofanya subira?”
(Aal - Imran - 142)

4)        Kuweka Nadhiri Kwa Ajili Ya MwenyeziMungu.
MwenyeziMungu anasema:
"Wanaotimiza wajibu (wao) (Nadhiri walizoziweka) na wanaoigopa siku ambayo shari yake itaenea (sana)".
(Ad - Dahr -7)
Na Mtume (SAW) amesema:-
<<Aliyeweka nadhiri ya kumtii MwenyeziMungu, basi amtii,  ama aliyeweka nadhiri ya kumuasi MwenyeziMungu) basi asimuasi>>.
(Bukhari, Ahmad, Attirmdhy na wengine na imepokewa kutoka kwa Bibi Aisha (RA).

5)        Kutufu Nyumba Tukufu Ya MwenyeziMungu:
MwenyeziMungu anasema:-
"Na tulimuusia Ibrahim na Ismail (tukawaambia): "Itakaseni (isafisheni) nyumba yangu kwa ajili ya wale wanaozunguka kwa ajili ya kutufu  na wanaokaa hapo na (kwa ajili ya) wanaorukuu na kusujudu hapo pia".
(Al - Baqarah - 125)
Na anasema:-
"Na waizunguke nyumba ya kale (Nyumba kongwe Al-Kaaba)”.
(Al - Hajj -29)

6)        Kuchinja Kwa Ajili Ya MwenyeziMungu
MwenyeziMungu anasema:-
"Sema hakika Sala zangu na Ibada zangu (zote nyengine) na uzima wangu na kufa kwangu (zote) ni kwa MwenyeziMungu. Mwumba wa walimwengu wote. (Likinisibu jambo limenisibu kwa kutaka MwenyeziMungu. Si kwa kutaka viumbe vyake, na yote ninayofanya nafanya kwa ajili yake) Hana mshirika wake, na haya ndiyo niliyoamrishwa na mimi ni wa kwanza wa waliojisalimisha (kwa MwenyeziMungu)”.
(Al - Anam -162-163)
Na kuchinja ni miongoni mwa ibada maana MwenyeziMungu anasema:-
"Basi Sali kwa ajili ya Mola wako na Uchinje (kwa ajili ya Mola wako).
(Na kila utakalolifanya lifanye kwa ajili ya Mola wako siyo mizimu wala mapango wala makaburi )."
(Suratul - Kawthar - 2)
        Ameeleza Imam Ali ibn Abi Talib(RA),  kwamba Mtume (SAW) amesema:-
<<MwenyeziMungu amemlani (kila) anayechinja kwa (ajili ya mwengine) asiyekuwa MwenyeziMungu)>>.
(Muslim, Ahmad, Annasai)


KWANZA - UKWELI WA AZMA YA KUTAKA KUFANYA IBADA

Mwenye kutaka kumuabudu Mola wake anahitaji azma ya kweli, yenye kuweza kuushinda uvivu na kuishinda tabia ya kupuuza, ili azma hiyo imwezeshe kufanya juhudi katika kumtii MwenyeziMungu na ili kauli yake isadikishe vitendo vyake (afanye vitendo na sio kusema tu).
MwenyeziMungu anasema:-
"Enyi mlioamini! Mbona (kwa nini) mnasema msiyoyatenda?"
(As - Saff-2)
Kwa anayetaka msaada kwa ajili ya kuiongeza nguvu azma yake basi inampasa kufuatana na watu wanaopenda kukaa katika vikao vya kheri.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na siku hiyo dhalimu atajiuma mikono yake (vidole) na huku akisema: "Laiti ningelishika njia (ya haki) pamoja na Mtume! " "Eee ole wangu , (adhabu yangu) Laiti nisingelimfanya fulani kuwa rafiki. Amenipoteza nikaacha mawaidha baada ya kunijia. Na kweli shetani anamtupa mwanaadamu".
Surat Al Furqan - 27-29

PILI -  KUAMINI KUWEPO KWA MALAIKA

 Kuamini kuwepo kwa Malaika ni nguzo katika nguzo za Imani, na hii inatokana na kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola wake na Waislamu, (pia wameamini hayo): Wote wamemuamini MwenyeziMungu na Malaika wake".
(Al - Baqarah - 285)
Na anasema:-
"Na Malaika wanamtukuza Mola wao na kumshukuru na kuwaombea msamaha walio katika ardhi".
(Ash -Shuraa -5)
Na anasema:-
"Wale walioko kwa Mola wako (nao ni Malaika) hawajivuni (wakaacha) kumuabudu (Mola wao kwa kuwa ni wakubwa la; bali) na wanamtukuza na kumsujudia".
(Al - Aaraf - 206)

Na anasema:-
"Anayemfanyia ushinde MwenyeziMungu na Malaika wake na Mitume wake na Jibrili na Mikail (anatafuta kuangamia) kwani MwenyeziMungu atakuwa mshinde wa makafiri hao".
(Al -Baqarah - 98)

Ushahidi upo mwingi katika Qurani na katika Mafundisho ya Mtume(SAW) juu ya kuwajibika kuwaamini (Malaika), na kwamba MwenyeziMungu amewaumba kwa Nuru.
 Na Imani juu ya kuwepo Malaika: Ni kukiri na kutokuwa na shaka yoyote juu ya kuwepo kwao, na kwamba wao ni viumbe na watumwa wa MwenyeziMungu, wanaamrishwa na wamekirimiwa.
MwenyeziMungu anasema:-
"Hawamtangulii kwa neno (Lake analosema) Nao wanafanya kwa amri Zake (zote)".
(Al - Tahriym - 6)
Na anasema :-
"Na walioko kwake (Malaika) hawatakabari na kumuabudu wala hawachoki (hawapumziki) Wanamtukuza usiku na mchana hawanyong'onyei  (hawafanyi uvivu)."
(Al - Anbiyaa - 19- 20)

MwenyeziMungu amewagawa Malaika makundi mbali mbali:
Miongoni mwao wamo wenye kazi ya  kuwapelekea Wahyi Mitume naye ni Mhuyisha sheria Mwaminifu Jibrili (AS), yupo mwenye kutoa roho, naye ni (Malak al Maut) Malaika wa kifo na wasaidizi wake, yupo aliyepewa kazi ya kupiga baragumu (Siku ya Kiama), naye ni Israfiyl na aliyepewa kazi ya kuleta mvua Mikail, na wapo Malaika wanaosimamia amali za viumbe nao ni Malaika wanaoandika mema na maovu tutendayo, na wamo waliopewa kazi ya kumlinda kiumbe mbele na nyuma yake, nao ni Walinzi.
MwenyeziMungu anasema:-
"Ana (kila mtu) kundi (la Malaika) mbele yake na nyuma yake; wanamlinda kwa amri ya MwenyeziMungu".
(Ar - Raad -11)

Wamo pia walinzi wa Pepo na neema zake, nao ni Radhwan na wenzake, na wamo waliopewa kazi ya motoni (Jahannam) na adhabu zake, nao  ni Malik na wenzake, na miongoni mwa Malaika wa motoni wapo pamoja na viongozi wao kumi na tisa.
Wamo pia wenye kazi ya adhabu za kaburini nao ni Munkar na Nakir na wamo wabebaji Arshi, na wamo wenye kazi ya kushughulikia manii katika matumbo ya uzazi,  kuanzia kuingia kwake (Manii hiyo) hadi kufikia wakati wa kuandikiwa kheri na shari ya kizazi kipya.
Katika hao wamo wanaoingia katika Nyumba inayozuriwa daima, (Baitul Maamur), wanaingia humo kila siku Malaika elfu sabiini kisha hawarudi tena mahali hapo, na wamo Malaika wanaotembea na kufuatilia vikao vya wenye kumtaja (Kumdhukuru) Mola wao, na wamo waliopangwa wakiwa wamesimama wala hawainami na wengine wanaorukuu na kusujudu na wala hawainuki na wamo wanaofaya mengi yasiyotajwa humu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Wala hapana yoyote ajuaye majeshi ya Mola wake ila Yeye tu; na wala haikuwa ila ukumbusho wa viumbe."
( Al -Mudathir - 31)
Ushahidi juu ya ugawaji huu (wa kazi za Malaika) ni mwingi, na umeelezewa katika Qurani na Sunnah, na ni maarufu miongoni mwa Maulamaa.


TATU – KUVIAMINI VITABU VILIVYOTANGULIA

Imani juu ya vitabu maana yake ni kuamini bila ya kuwa na shaka yoyote kwamba vitabu vyote (Taurat, Injili, Zaburi na Qurani) vimeteremshwa kutoka kwa MwenyeziMungu na kwamba MwenyeziMungu amevitaja kwa uhakika.
Mwenyezi Mungu anasema:-
"Enyi mliamini muaminini MwenyeziMungu na Mtume wake na kitabu alicho kiteremsha juu ya Mtume wake na vitabu alivoteremsha zamani. Na mwenye kumkanusha MwenyeziMungu na  Malaika wake na vitabu vyake na Mitume wake na Siku ya mwisho basi bila ya shaka amepotea (upotevu) ulio mbali(na haki)".
(AN - Nisaa -136)
       Miongoni mwa vitabu hivyo (asili yake) vilitokana na maneno ya MwenyeziMungu  kwa Mitume yake moja kwa moja bila kupitia kwa mwakilishi (Jibril AS), na mengine ni kupitia kwa Malaika (Jibrili AS) na yapo aliyoyaandika MwenyeziMungu mwenyewe "Subhanahu wa taala."
MwenyeziMu;ngu anasema:-
"Na haikuwa kwa mtu kwamba MwenyeziMungu anasema naye ila kwa ilhamu (anayotiwa moyoni mwake) au kwa nyuma ya pazia la (kumsikilizisha sauti inayotokana na MwenyeziMungu pasi na kumwona) au humtuma mjumbe (Jibril) naye hufunulia (humletea wahyi ) kiasi anachotaka kwa idhini yake.”
(Ashu - araa -51).
Na akamwambia Musa(AS)
“Akasema(MwenyeziMungu) "Ewe Musa! mimi nimekuchagua juu ya watu wote kwa ujumbe wangu na kwa kusema nawe kwangu. Basi pokea haya niliyokupa na uwe miongoni mwa wanaoshukuru."
(Al -Aarar-144)
Na anasema pia:-
"Na MwenyeziMungu akamsemeza Musa.”
(An - Nisaa -164)
Ama kuhusu Taurat MwenyeziMungu anasema:-
"Na tukamuandikia katika mbao kila kitu mauidha (ya kila namna) na maelezo ya kila jambo".
(Al - Aaraf -145)
Na akasema juu ya Issa (AS)
"Na tukampa Injili".
(Al - Hadiyd - 27)
Na akasema:-
"Na Daud tukampa Zaburi".
(An - Nisaa -163)
Na juu ya Qurani akasema;
"Lakini MwenyeziMungu anayashuhudia aliyokuteremshia (kuwa ni haki) ameyateremsha kwa ilimu yake na Malaika pia wanashuhudia. Na MwenyeziMungu anatosha kuwa shahidi".
(An - Nisaa -166)
Na pia akasema:
"Na Qurani imegawanywa sehemu mbali mbali (kwa kuiteremsha kidogo kidogo) ili uwasomee watu kwa kituo; na tumeiteremsha kidogo kidogo (ili iwe nyepesi kuhifadhika)".
BANI ISRAIL (Israa -106)
Na akasema:
"Na bila ya shaka hii Qurani ni uteremsho wa Mola wa walimwengu wote. Ameteremsha haya Mhuyisha sheria mwaminifu (Jibrli(AS)) juu ya moyo wako ili uwe miongoni mwa waonyaji kwa lugha ya kiarabu wazi wazi (fasihi)."
(Ash - Shuraa - 192 -195)
Na MwenyeziMungu pia akasema:-
"Haitaifikia batili mbele yake wala nyuma yake; kimeteremshwa na mwenye hekima ahimidiwaye".
HAA MYM SAJDAH (Fusilat - 42).
    
Vitabu alivyovitaja MwenyeziMungu katika Qurani ni:
Qurani, Taurat, Injili, Zaburi na vitabu (sahifa) za Nabii Ibrahim na Musa (AS).
MwenyeziMungu anasema:-
"MwenyeziMungu hakuna aabudiwaye kwa haki isipokuwa Yeye - Mwenye uhai wa milele na Mwendeshaji wa mambo yote Amekuteremshia kitabu kwa haki, kinachosadikisha yaliyokuwa kabla yake na aliteremsha Taurat na Injili".
(Aal - Imrani -2 - 3)
Na akasema:
"Na Daud tukampa Zaburi ".
(An - Nisaa -36- 37)
Na pia akasema:-
"Au hakuambiwa yaliyomo katika vitabu vya Musa? Na vya Ibrahim aliyetimiza ahadi (ya MwenyeziMungu )".
(An - Najim -36 - 37)
Akavitaja vyengine kwa pamoja akasema:-
"Kwa hakika tuliwapeleka Mitume wetu kwa dalili wazi wazi na tukaviteremsha vitabu na uadilifu pamoja nao ili watu wasimamishe uadilifu".
(Al - Hadiyd -25)


QURANI TUKUFU


DARAJA YAKE KATIKA VITABU VILIVYOTANGULIA

MwenyeziMungu anasema:-
"Na tumekuteremshia kitabu kwa ajili ya kubainisha haki kinachosadikisha vitabu vilivyokuwa kabla yake na kuvihukumia(Wa Muhayminan) kama haya ndiyo yaliyoharibiwa au ndiyo yaliyosalimika".
(Al - Maidah -48).
Na akasema:-
"Na haiwezekani kuwa hii Qurani imetungwa haitoki kwa MwenyeziMungu (kama mnavyodai). Bali imetokana na MwenyeziMungu inayasadikisha yaliyo mbele yake na ni maelezo ya vitabu (vilivyopita) Haina shaka kuwa imetokana kwa Mola wa walimwengu (wote)".
Yunus - 37)
Neno "Wa muhaiyminan" na maana yake ni "Kuvihukumia", na maana yake ni kuwa Qurani imepewa jukumu la kutoa hukmu juu ya vitabu vilivyokuja kabla yake. Na neno “Kuvisadikisha”, maana yake ni kusadikisha yaliyomo, yale ya kweli na kukanusha yaliyoongezwa, yaliyobadilishwa au kugeuzwa pamoja na kuyaamulia kufutwa na pia  kuyathibitisha yaliyo sahihi.
Haya ndiyo anayotakiwa kufuata kila anayeshikamana na vitabu vilivyotangulia, yule ambaye hataki kurudi nyuma akawa kafiri.
Kama alivyosema MwenyeziMungu:-
"Wale tuliowapa kitabu kabla ya hii (Qurani‎) baadhi yao wanaiamini hii (Qurani) na wanaposomewa husema; ‘tunaiamini bila ya shaka hii ni haki itokayo kwa Mola wetu; kwa yakini kabla ya haya tulikuwa wenye kujisalimisha (kwa MwenyeziMungu).”
(Al - Qasas -52)

UMMA WOTE UNAWAJIBIKA KUKIFUATA

Watu wote wanawajibika kukifuata kitabu hiki kwa dhahiri na kwa siri na kushikamana nacho na kukisimamia kama ipasavyo.
MwenyeziMungu anasema:-
“Na hii (Qurani) ni kitabu tulichokiteremsha (kwenu) kilicho na baraka nyingi basi kifuateni na muwe wacha Mungu ili Mrehemiwe".
(Al - An - Am - 155)
Na akasema:-
"Fuateni mliyoteremshiwa kutoka kwa Mola wenu wala msifuate (hao mnaowaitakidi) kuwa walinzi badala yake".
(Al - Aaraf -3)
Na pia akasema:-
"Na wale wanaokishika kitabu (cha MwenyeziMungu kweli kweli) na wakasimamisha Sala (tutawalipa mema) Hakika sisi hatupotezi malipo ya wafanyao mema.”
(Al - Aaraf -170)
Aya zinazoelezea haya ni nyingi, na Mtume (SAW) ameusia juu ya kushikamana na kitabu cha MwenyeziMungu akasema:-
<<Kikamateni kitabu cha MwenyeziMungu na mshikamane nacho>>.
Na katika hadithi iliyoelezwa na Sayiduna Ali(RA) aliyoinyanyua kwa Mtume(SAW), alisema kuwa Mtume (SAW) alisema:-
“Zitakuwa fitina nyingi”.
Nikasema:
“Tufanye nini ili tuepukane nazo ewe Mtume wa MwenyeziMungu?”
Akasema:
“Kitabu cha MwenyeziMungu”.
(Imetolewa na Attirmidhy).

KUSHIKAMANA NACHO NA KUKISIMAMIA KAMA KINAVYOSTAHIKI

Uislamu umeshurutisha wafuasi wake kukihifadhi, kukisoma na kukisimamia vilivyo kitabu hiki (Qurani tukufu) usiku na mchana. Kuzizingatia aya zake, kuhalalisha yale yaliyohalalisha kitabu hiki, kuharamisha yaliyoharamisha pamoja  na kuzifuata amri zake, kujiepusha na makatazo yake, kujifunza kutokana na mifano yake, kuwaidhika na visa vyake, kuzifuata vilivyo aya zake zile zilizo wazi maana yake na kusalimu amri juu ya zile zinazotatanisha maana yake (kwa kujiepusha na kuzifasiri kwa matamanio yetu), kutoivuka mipaka yake, kukilinda kutokana na wabadilishaji na waongezaji (wazidishaji mambo yasiyokuwemo ndani yake) walaghai waongo, na kunasihi kutokana nacho kama ipasavyo na kuilingania kwa ujuzi wa kweli.

WAADI WA MWENYEZIMUNGU WA KUIHIFADHI(Qurani).

MwenyeziMungu amekwishadhamini kuihifadhi Qurani isifikiwe na mikono ya uongezaji na upunguzaji na ubadilishaji.
MwenyeziMungu anasema:-
"Hakika sisi ndio tulioteremsha mauidha haya (Qurani); na hakika sisi ndio tutakayoyalinda".
(Hijr- 9)
MwenyeziMungu ametaka iwe hivyo ili kuidumisha hoja yake kwa watu na kuifanikisha mpaka hapo atakapoirithi ardhi pamoja vilivyo juu yake (siku ya Kama).
Na hoja hiyo haitoweza kudumu isipokuwa kwa kuendelea kuwepo kwa Qurani hii baina ya watu, huku ikiwa imehifadhika mpaka siku ya Kiama na ili iwe marejeo yao katika mambo ya Itikadi zao za Dini, Misingi yake, Chimbuko lake, Lengo lake na ili tuweze kuzijuwa Sheria za MwenyeziMungu na kubainika kwa wajibu wa yale yanayobainisha(Qurani) na maharamisho yanayokataza na ili kuzijuwa fadhila za kibinadamu pamoja na ukamilifu wa tabia inayofundisha kitabu hiki na kuyaamrisha katika hayo pamoja na kufaidika kutokana na yaliyomo ndani yake katika mongozo ya sheria na kwa kila lililo muhimu katika maisha ya wanadamu.
Tunatakiwa pia kuyasoma mawaidha yake (Qurani), nasaha zake, mifano yake, na mafudisho yake pamoja na yote yaliyomo yenye bishara njema, maonyo, makemeo na njia zote za mafunzo ya malezi ya kila namna inayotuongoza kuelekea njia iliyonyooka.

USHAHIDI WA KUHIFADHIKA KWAKE.

Inampasa kila mwenye akili timamu aamini na awe na uhakika kuwa Qurani anayoisoma leo, ndiyo ile ile aliyoteremshiwa Muhammad(SAW), na iwapo mtu atachukua aya yoyote ile katika aya za Qurani akaenda nayo London, Paris, Moscow, Washington, Peking au Tel aviv na akatembea nayo katika miji ya Afrika, Australia kisha akenda Makka au Madina au akachukua msahafu kutoka kila mji miongoni mwa miji hiyo na akafungua sura ambazo aya hizo zimetolewa, atagundua kwamba Qurani zote ni moja, na kwamba aya alizozitoa ndani yake ni moja, bali atagundua kwamba kila kilicho ndani ya msahafu wowote ule ni maneno yale yale, hayakugeuzwa wala kubadilika.
MwenyeziMungu amesadikisha aliposema:-
"Hakika sisi ndio tulioteremsha mawaidha haya (hii Qurani) na hakika sisi ndio tutakayoyalinda".
(Al - Hijri 9)

 

 

SUNNAH, INAYOIBAINISHA QURANI NA KUIHIFADHI

MwenyeziMungu anasema:-
"Na tumekuteremshieni mauidha ili uwabainishie watu yaliyoteremshwa kwao na ili wapate kufikiri."
(An - Nahl-44)
Mtume(SAW) amekibainisha kitabu cha Mola wake kwa watu kwa kauli zake, matendo yake na kukubali kwake.
MwenyeziMungu ameuhifadhi ubainisho huu wa kinabii katika yale yalioandikwa na watu ndani ya vitabu vya Sunnah za Mtume (SAW), na MwenyeziMungu amezihifadhi Sunnah hizo kwa kuwajaalia wengi wa viumbe vyake kuzihifadhi hadithi za Mtume(SAW) kwa moyo wakiziwekea vikao vya elimu ili kumuelimisha kila asiyezijua, hata wakapatikana miongoni mwa umma wa Muhammad(SAW) wanaohifadhi kwa moyo maelfu ya hadithi pamoja na milolongo ya majina ya wapokezi wa hadithi hizo pamoja na daraja zake,  mfano wa Al Bukhari, Muslim na wale Maimamu sita, ambao kila mmoja wao ameandika kitabu cha hadithi za Mtume (SAW) na wengineo.
Hii ni kwa sababu hadithi za Mtume (SAW) zinabainisha mafundisho yaliyomo katika Qurani, na ni sehemu ya dini inayomfundisha Muislamu kwa ukamilifu mwenendo wake wa kila siku katika Sala zake, Funga zake, Hija yake, kuuza na kununua kwake, kuoa na kuacha kwake, pamoja na uhusiano wake na ukoo wake na jirani zake n.k. Na pia Sunnah ya Mtume(SAW) inamfundisha Mwislamu yale yanayompasa mbele ya Mola wake na mbele ya Umma wake na yote hayo yameandikwa na kudhibitiwa na kuhifadhiwa.

MWENYEZIMUNGU AMEUCHAGUA UMMA ULIO BORA KUKIHIFADHI KITABU CHAKE NA SUNNA ZA MTUME WAKE (SAW).

Kwa vile Mtume wa Mwenyezi Mungu(SAW) ni Mtume wa mwisho, kwa hivyo MwenyeziMungu amechukuwa dhamana ya kuihifadhi dini aliyokuja nayo kutokana na kubadilishwa, kuongezwa au kupunguzwa mpaka siku ya Kiama.
MwenyeziMungu akawaandaa kwa kazi hiyo Masahaba wa Mtume(SAW) na akasema juu yao:
"Nyinyi ndio Umma bora kuliko Umma zote zilizodhihirishiwa watu".
Aal - Imran -110).
Na akasema juu yao:-
"Na vivyo hivyo tumekufanyeni Umati bora, ili muwe mashahidi juu ya watu na Mtume awe shahidi juu yenu".
(Al - Baqarah -143).
Na Mtume (SAW) amewaelezea Masahaba wake (kwa kuwapa sifa ya) kuwa ni:
‘Karne iliyo bora kupita zote’.

Kwa vile sababu kubwa ya kuongeza, kupunguza au kubadilisha ni kufuata matamanio ya nafsi, MwenyeziMungu aliwaandaa masahaba wa Mtume (SAW) mwandao mahsusi ili waisimamie dini na kuihifadhi kwa ajili ya walimwengu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na jueni ya kwamba Mtume wa MwenyeziMungu yuko pamoja na nyinyi (basi msikilizeni anavyokwambieni) Lau yeye angekutiini katika mambo mengi (mnayoyasema) bila shaka mngetaabika lakini MwenyeziMungu ameupendezesha kwenu Uislamu na ameupamba nyoyoni mwenu na amekufanyieni muuchukie ukafiri na ufasiki na uasi".
(Al - Hujurat -7)

Kwa uandalizi huu walistahiki kusifiwa na MwenyeziMungu kwa sifa zifuatazo;

MwenyeziMungu anasema:-
"(Basi) wapewe (mali hayo ) mafakiri wakimuhajiri ambao walifukuzwa katika nyumba zao na mali zao (wakahiari kuacha hayo) kwa ajili ya (kutafuta) fadhila za MwenyeziMungu na radhi (yake) na kuinusuru (dini ya) MwenyeziMungu na Mtume wake. Basi hao ndio Waislamu wa kweli. Na (pia wapewe) wale waliofanya maskani yao hapa (Madina ) na wakautakasa Uislamu (wao barabara) kabla ya (kuja) hao (Muhajiri huko Madina) na wakawapenda hao waliohamia kwao wala hawapati (hawaoni) dhiki nyoyoni mwao (Muhajiri) na wanawapendelea kuliko nafsi zao, hao ndio wenye kufaulu kweli kweli.
(Al - Hashr -8 - 9)

MwenyeziMungu anasema:-
"Na walioamini wakahama (kuja Madina na wakaipigania dini ya MwenyeziMungu (nao ni Muhajiri). Na wale waliowapa Muhajiri mahali pa kukaa na wakainusuru (dini ya MwenyeziMungu na Mtume wake) (Nao ni Ansari) Hao ndio Waislamu wa kweli. Watapata msamaha (wa MwenyeziMungu) na kuruzukiwa kuzuri (kabisa huko akhera)".
(Al - Anfal -74).

MwenyeziMungu anasema:-
"Na kama wakitaka kukuhadaa basi MweyeziMungu atakutosheleza, Yeye ndiye aliyekusaidia kwa nusura yake na kwa waliokuamini".
(Al - Anfal -62).




MwenyeziMungu anasema:-
Muhammad ni Mtume wa MwenyeziMungu, na walio pamoja nae ni wenye nyoyo thabiti mbele ya makafiri na wenye kuhurumiana wao kwa wao, utawaona wakiinama kwa kurukuu na kusujudu (pamoja) wakitafuta fadhila za MwenyeziMungu na radhi (yake). Alama zao zi katika nyuso zao kwa taathira (athari) ya kusujudu".
(Al - Fath -79)

"Kwa hakika MwenyeziMungu amewapa radhi Waislamu walipofungamana nawe chini ya mti; na Alijua yaliyomo nyoyoni mwao. Basi akateremsha utulivu juu yao na akawapa kushinda kwa zama za karibu".
(Al - Fath -18).

SIFA ZA MASAHABA ZILIZOWAFANYA WATEULIWE KUWA NI MAIMAMU (VIONGOZI) WA DINI NA DUNIA.

Aya zilizotajwa kabla zimeelezea kwamba Masahaba (RA) wanasifika na sifa zifuatazo:
Umma ulio bora kuliko umma zote zilizodhihirishiwa watu.
Umati bora  uliochaguliwa kuwa mashahidi juu ya watu.
MwenyeziMungu aliupendezesha kwao Uislamu, akaupamba nyoyoni mwao na akawafanya wauchukie ukafiri na ufasiki na uasi.
Wao ni wasema kweli waliofaulu na walioamini kikweli.
Wenye nyoyo thabiti kwa makafiri, wenye kuhurumiana wao kwa wao.
Wanaorukuu na kusujudu ambao MwenyeziMungu alitizama yaliyo ndani ya nyoyo zao na akawa radhi nao.

Kwa ajili ya yote hayo, wakastahiki kufanywa na MwenyeziMungu kuwa Makhalifa katika ardhi na kuwatimizia yale aliyowaahidi na hayo yalipatikana wakati wa utawala wa Makhalifa walioongoka – Al Khulafaa Al Rashidiyn(RA)[7].
MwenyeziMungu anasema:-
"MwenyeziMungu amewaahidi wale walioamini miongoni mwenu na kufanya vitendo vizuri, kuwa atawafanya makhalifa katika ardhi kama alivyowafanya makhalifa wale waliokuwako kabla yao. Na kwa yakini atawasimamishia dini yao aliyowapendelea na atawabadilishia amani baada ya hofu yao, wawe wananiabudu, hawanishirikishi na chochote. Na watakaokufuru baada ya hayo basi hao ndio wavunjao amri zetu".
(Annur -55)
Kama walivyostahiki kuwa Maimamu – Viongozi - katika mambo ya kidunia na kwa kupitia mikononi mwao kuweza kuisimamisha dini aliyoridhika nayo MwenyeziMungu, basi walistahiki pia kuwa Maimamu wa dini, ili MwenyeziMungu awe radhi nao pamoja na watakaowafuata kwa wema.
MwenyeziMungu anasema:
"Na wale waliotangulia wakawa wa kwanza katika (Waislamu), Muhajiri na Ansari na wale waliofuata kwa mwenendo mzuri “MwenyeziMungu atawapa radhi nao wamridhie MwenyeziMungu kwa hayo atakayowapa”, na amewaandalia mabustani yapitayo mito mbele yake wakae humo milele, huku ndiko kufuzu kukubwa."
(At-Tawba -100)
 Huu ndio Umma ambao kwao MwenyeziMungu ameihifadhi dini, akaridhika nao na Umma zote na mataifa mbali mbali pia yakaridhika nao, wakawafuata na kuwapenda juu yahitilafu ya utaifa, rangi na lugha zao.

Nne - KUIAMINI MITUME (Alayhimu Salaam)

Kuamini Mitume ni nguzo katika nguzo za Akida (Itikadi ya dini) kwa ajili hiyo inamwajibikia kila mtu kuiamini Mitume ya MwenyeziMungu yote bila ya kutofautisha baina yao.
MwenyeziMungu anasema:-
"Semeni nyinyi (Waislamu): "Tumemwamini MwenyeziMungu na yale tuliyoteremshiwa na yale yaliyoteremshwa kwa Ibrahim na Ismail na Is haqa na Yakubu na kizazi (chake Yakubu) na waliyopewa Musa na Issa na pia yale waliyopewa Manabii (wengine)kutoka kwa Mola wao; hatutafautishi baina ya yeyote katika hao (wote tunawaamini) Na sisi tumenyenyekea kwake."
(Al - Baqarah - 136).
MwenyeziMungu akabainisha pia kuwa hii ndiyo imani ya Waislamu, akasema:-
"Mtume ameamini yaliyoteremshwa kwake kutoka kwa Mola wake, na pia Waislamu (pia wameamini hao) Wote wamemwamini MwenyeziMungu na Malaika wake na vitabu vyake na Mitume yake (Na husema Waislamu na Mtume wao husema); Hatutofautishi baina ya yeyote katika Mitume yake (wote tunawaamini)." Na husema "Tumesikia na tumetii (tunakuomba) msamaha Mola wetu! Na marejeo ni kwako."
(Al - Baqarah - 285)

 MwenyeziMungu akatujulisha pia kuwa wema umo katika imani hii, akasema:-
"Sio wema (tu huo peke yake) kuwa mnaelekeza nyuso zenu upande wa Mashariki na Magharibi (katika kusali. Yako na mema mengine.) Bali wema (hasa) ni (wa wale) wanaomwamini MwenyeziMungu na siku ya mwisho na Malaika na Kitabu na Manabii …."
(Al - Baqarah -177)
Kwa hivyo mtu anapoamini baadhi ya Mitume na asiwaamini wengine na akawabagua katika kuwaamini basi anakuwa kafiri.
MwenyeziMungu amesema:-
"Hakika wale wanaomkanusha MwenyeziMungu na mitume yake na wanataka kutenga baina ya MwenyeziMungu na Mitume yake kwa kusema; "Wengine tunawaamini na wengine tunawakataa" na wanataka kushika njia iliyo kati kati ya haya (si ya kiislamu khasa wala ya kikafiri) Hao ndio makafiri kweli. Na tumewaandalia adhabu idhalilishayo. Na waliomwamini MwenyeziMungu na Mitume yake wala wasimfarikishe yeyote katika wao, hao atawapa ujira wao na MwenyeziMungu ni mwingi wa kurehemu."
(An - Nisaa -150- 152)

HEKIMA YA KULETWA MITUME.

1)     MWENYEZIMUNGU AMELETA MITUME ILI WAWAJULISHE WATU JUU YA MOLA WAO NA MUUMMBA WAO, NA PIA ILI KUWALINGANIA WATU WAMWABUDU MWENYEZIMUNGU MMOJA TU, NA KUIKANUSHA MIUNGU YA UWONGO
MwenyeziMungu anasema:-
"Bila shaka tumempeleka Mtume katika kila umma (awaambie) ya kwamba "Mwabuduni MwenyeziMungu na muepukeni (Iblis) muovu".
(An - Nahl -36)

Na akasema:-
"Na kawaulize Mitume wetu tuliowaleta kabla yako; “Jee! Tulifanya miungu mengine iabudiwe badala ya Mwingi wa rehema?"
(Az - Zukhruf 45)
Na akasema:-
"Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia ya kwamba hakuna aabudiwae ila mimi basi niabuduni".
(Al - Anbiyaa -25)

2)     MWENYEZI MUNGU AMEWALETA MITUME ILI KUISIMAMISHA DINI, KUIHIFADHI, KUKATAZA MFARAKANO, NA ILI IHUKUMIWE KWA HUKMU ALIYOITEREMSHA MWENYEZI MUNGU;
MwenyeziMungu anasema:-
"Amekupeni Sharia ya dini ile ile aliyomuusia Nuhu na tuliyokufunulia wewe na tuliowausia Ibrahim na Musa na Isa, kwamba simamisha dini wala msifarikiane kwayo”.
(Ash - Shuraa -14).
Na akasema:-
"Hakika tumekuteremshia kitabu(hiki) hali ya  kuwa kimeshikamana na haki ili upate kuhukumu baina ya watu kama alivyokufahamisha MwenyeziMungu wala usiwe mwenye kuwatetea wafanyao hiyana."
(An - Nisaa -105).

3)     AMEWATUMA KWA AJILI YA KUWAPA HABARI NJEMA WAISLAMU JUU YA YALE ALIYOWAANDALIA KATIKA NEEMA ZA MILELE, JAZAA YA UTIIFU WAO, NA ILI KUWAONYA MAKAFIRI JUU YA ADHABU WATAKAYOPATA ILI IWE JAZAA YA KUKANUSHA KWAO, NA ILI KUONDOA UDHURU KWA  WATU NA KUWASIMAMISHIA HOJA KUTOKA KWA MOLA WAO
MwenyeziMungu anasema:-
"(Hao ni) Mitume waliotoa habari nzuri kwa (watu wema), wakawaonya (wabaya) ili watu wasiwe na hoja juu ya MwenyeziMungu baada ya (kuletwa hawa) Mitume. Na MwenyeziMungu ni Mwenye nguvu na Mwenye hikma."
(An - Nisaa -165)

4)     AMEWATUMA ILI WAWAFUNDISHE WATU NA KUWA MFANO MWEMA KATIKA MWENENDO WAO, IKHLAQI NJEMA, KUWAFUNDISHA KUMWABUDU MOLA WAO KWA NJIA ZILIZO SAHIHI NA ILI KUWAONGOZA KATIKA NJIA YA MWEYEZIMUNGU ILIYONYOKA.
MwenyeziMungu anasema juu ya Mtume wetu(SAW):-
"Bila ya shaka mnao mfano mwema(Ruwaza nzuri) kwa Mtume wa MwenyeziMungu kwa mwenye kumuogopa MwenyeziMungu na Siku ya mwisho, na kumtaja MwenyeziMungu sana".
(Al - Ahzab -21).

5)     MWENYEZIMUNGU AMEWALETA ILI KUWAOKOA WATU WASIKHITILAFIANE KATIKA MAMBO MUHIMU YA MAISHA YAO NA KUWAONGOZA KATIKA HAKI AITAKAYO MUUMBA WAO.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na hatukukuteremshia kitabu (hiki) ispokuwa uwabainishie yale ambayo wanakhitalifiana, na pia (kiwe) uongozi wa rehma kwa watu wanaoamini."
(An - Naha 64)

6)     AMEWALETA ILI WABAINISHE AMALI NJEMA ZINAZOITAKASA NAFSI YA BINAADAMU NA KUITAHIRISHA NA KUPANDA NDANI YAKE MBEGU ZA KHERI.
MwenyeziMungu anasema:-
"Yeye ndie aliyeleta Mtume katika watu wasiojua kusoma, anayetokana na wao awasomee Aya zake na  kuwatakasa na kuwafunza Kitabu (Qurani) na Hikima (ilimu nyenginezo). Na kabla ya haya walikuwa katika upotofu (upotevu) ulio dhahiri".
(Al - Jumua -2)


SIFA ZA MITUME (AS)

Kila Mtume Lazima awe mkamilifu wa sifa za kimaumbile, awe na tabia njema za hali ya juu kabisa, awe na akili timamu na awe msema kweli, awe mwaminifu katika kuyafikisha aliyokalifishwa kuyafikisha, aepukane na kila sifa mbaya, awe na ukamilifu wa kiwiliwili (asiwe na kilema), na awe na nguvu ya kiroho ili isiwezakane kwa nafsi ya mwanadamu au jinni kuitawala mtawalo wa kiroho, na hii ni kwa sababu MwenyeziMungu anamnyoshea msaada kutoka kwake.
Lazima kila Mtume awe na sifa hizi kwa sababu sifa zao zikiwa duni kuliko za wengine walioishi wakati wao, au akili zao zikiwa na udhaifu fulani au kuwa na udhaifu wa kiroho hata waweze kutawaliwa na nguvu za kiroho za watu wengine, au udhaifu wa nafsi, udhaifu wa azma hata washindwe kutekeleza amri za Mwenyezi Mungu, makatazo Yake, pamoja na kushindwa kutii kikamilifu au kushindwa kuyafikisha kikamilifu yale waliyokalifishwa kuyafikisha kwa sababu ya hofu, tamaa, kusahau au kwa sababu nyengine zozote zisizokuwa hizo.
Wangelikuwa na upungufu wa lolote miongoni mwa hayo, wasingefaa kwa kazi ya MwenyeziMungu makhsusi kama hii ya kuchaguliwa kuwa Watume na kupokea Wahyi pamoja na kuonyeshwa siri za elimu ya  MwenyeziMungu walizofunuliwa.
Wasingefaa kuchaguliwa na Mwenyezi Mungu kwa kazi hii pia ingelikuwa miili yao ina vilema vinavyoweza kuwafanya watu wajiepushe nao, na kwa njia hiyo makafiri wangepata hoja za kuwatia ila katika ulinganio wao.
Ama kinyume na hayo Mitume ni wanadamu kama wanadamu wengine, huwasibu yote yanayowasibu wanadamu wenzao na hufanya kama wanavyofanya, wanakula na kunywa, wanalala, wanaowa, wanaumwa na huenda wakasahau baadhi ya mambo yale yasiyohusiana na ujumbe waloamrishwa na MwenyeziMungu kuufikisha na huenda wakakosea katika baadhi ya mambo ya kibinadamu waliyoruhusiwa kufanya kwa jitihada zao katika kuyaamua.
Lakini wao hukumbushwa na kujulishwa makosa yao kwa njia ya Wahyi ili makosa hayo yasije kuonekana kuwa ndiyo sahihi inayotakiwa.
Na huenda mikono ya madhalimu ikawafikia na wakakumbana na mateso na adhabu na huenda hata wakauwawa, hasa kwa wale Mitume wasioamrishwa kupigana jihadi.

MITUME ILIYOTANGULIA

Wamo miongoni mwao wale alotuhadithia MwenyeziMungu juu yao na kuyataja majina yao na wengine hukutuhadithia  habari zao.
MweyeziMungu anasema:-
"Na (tuliwapa wahyi) Mitume tuliokuhadithia (habari zao) zamani na Mitume ambao hatukukuhadithia (habari zao) na MwenyeziMungu akamsemeza Musa".
(An - Nisaa -164)
Kwa hivyo sisi tunawaamini Mitume wote, mmoja mmoja, pale alipowataja MwenyeziMungu kwa kuwachambua au kwa ujumla pale alipowajumuisha.

Ama wale alotuhadithia habari zao ni wale waliotajwa katika kauli ya MwenyeziMungu:-
"Na hizi ndizo (baadhi ya) hoja zetu tulizompa Ibrahim juu ya watu wake.Tunamyanyua katika vyeo yule tumtakaye (kwa kuwa anakwenda mwendo tunaoutaka). Hakika Mola wako ndiye Mwenye hekima na ndiye Ajuaye.
Na tukampa (Ibrahim mtoto anayeitwa Is-haqa na (mjukuu anayeitwa) Yakubu wote tukawaongoa. Na Nuhu tulimwongoa zamani na katika kizazi chake (Nuhu tulimwongoa) Daudi na Suleiman na Ayub na Yusuf na Musa na Harun. Na hivi ndivyo tulipavyo wafanyao wema Na (tukamwongoa) Ismail na Al Yasaa (Ilisha) na Yunus na Luti Na wote tukawafadhilisha juu ya walimwengu (wote katika zama zao)".
(Al - An - Am -83- 86).
Na akasema:-
“Hakika Mwenyezi Mungu alimchagua Adamu na  Nuhu na kizazi cha Ibrahimu na kizazi cha Imrani (Babake Musa na Imrani mwengine aliye babake Maryamu) juu ya walimwengu wote (wa zama zao)”.
Aali Imran - 33
Na akasema:-
"Na kwa Adi tuliwapelekea ndugu yao Hud".
(Huud -50)      
 Na akasema:-
"Na (mtaje) Ismail na Idris na Dhul Kifli wote walikuwa miongoni mwa wanaosubiri".
(Al - Anbiyaa -85)
"Na kwa Thamud tukampeleka ndugu yao Saleh".
(Huud -61)
Na akasema:-
"Muhammad si baba wa yeyote katika wanaume wenu bali yeye ni Mtume wa Mungu na mwisho wa Mitume".
(Al - Ahzab -40)
Mitume hii imeletwa na MwenyeziMungu katika zama zote zilizopita, na hakukuwa na Umma uliokosa Mtume aliyekuwa akiwalingania katika njia ya MwenyeziMungu na kuwaongoza katika njia iliyo sawa.
MwenyeziMungu anasema:-
"Wallahi sisi tulituma (Mitume) kwa Umma zilizokuwa kabla yako".
(Al - Nahl -63).
Na akasema:-
"Na hakuna taifa lolote ila alipita humo muonyaji (Mtume kuwaonya)".
(Fatir -24)
Na kasema:-
"Na kila kaumu ina muongozaji."
(Ar - Raad -7)

MUHAMMAD (SAW)

Hapo mwanzo, Mitume ilikuwa ikitumwa kwa ajili ya kaumu zao tu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na kila kaumu ina muongozaji."
(Ar - Raad -7)
Lakini Muhammad (SAW) ametumwa kwa ajili ya watu wote .
MwenyeziMungu anasema:-
"Nasi hatukukutuma (hatukukuleta) ila uwe rehema  kwa walimwengu wote".
(An - Biyaa - 107)
Na akasema:-
"Ni mwenye kuleta baraka (kweli kweli) yule aliyeteremsha Qurani kwa mja wake ili awe muonyaji kwa walimwengu (wote)".
(Furqan -1)
Miujiza ya Mitume iliyotangulia ilikuwa ikitendeka na kuonekana mbele ya macho ya watu waliokuwa wakiiona, ama wengine waliobaki walikuwa wakihadithiwa tu na wenzao wengi waliyoiona miujiza hiyo ikitendeka. Lakini MwenyeziMungu amejaalia Dalili na Muujiza wa Muhammad (SAW), yenye kuusadikisha ujumbe wake kuwa ni thabiti na isiyokonga mpaka Siku ya kiama ili iwe hoja juu ya watu wote.
Muhammad (SAW) ni Nabii na Mtume wa mwisho; hapana mtume baada yake. Ndiyo maana MwenyeziMungu akaihifadhi dini aliyokuja nayo na akaihifadhi Miujiza yake inayosadikisha Utume wake (SAW).


TANO – IMANI JUU YA SIKU YA KIAMA.

Imani juu ya Siku ya mwisho ni  nguzo mojawapo katika nguzo za imani, ni wajibu kuiamini, pamoja na kuziamini alama za kukaribia kwa Siku ya kiama pamoja na ishara zake zitakazo onekana kabla ya kufika siku hiyo, na pia imani juu ya kufa na yale yanayofuatia baada yake katika misukosuko ya kaburini na adhabu zake pamoja na neema zake,  na juu ya kupulizwa kwa baragumu na watu kutoka makaburini, na juu ya vitisho vya Siku ya Kiama na kukusanywa kwa watu na kugawiwa kwa madaftari (yaliyoandikwa ndani yake mema na maovu) na kuwekwa kwa mizani na Sirati (njia) na Hodhi na Shafaa kwa wale watakaoruhusiwa na MwenyeziMungu, na juu ya Pepo na neema zake, na Moto na adhabu zake, na mengi mengineyo yaliyotajwa katika Qurani na katika hadithi za Mtume (SAW) zilizo sahihi.


DALILI ZA IMANI JUU YA SIKU YA MWISHO (KIAMA)


1) USHAHIDI WA KUNUKUU:-

MwenyeziMungu ametujulisha juu ya Siku ya Kiama katika kauli Yake:
“Alif Lam Mim.
Hiki ni Kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake; ni uwongofu kwa wachamungu.
Ambao huyaamini ya ghaibu na hushika Sala, na hutoa katika tuliyowapa.
Na ambao wanayaamini yaliyo teremshwa kwako, na yaliyo teremshwa kabla yako; na Akhera wana yakini nayo”.
(Al - Baqarah -1 - 4)
Na katika kauli Yake:-
"Na mwenye kumkanusha MwenyeziMungu na Malaika wake na vitabu vyake na Mitume  yake na Siku ya mwisho basi bila ya shaka amepotea upotofu (upotevu) ulio mbali(na haki)".
(An - Nisaa -136)
Na katika Kauli yake:-
"Hakika wale wasiotaraji kukutana nasi na wakawa radhi na maisha ya dunia na wakapoa moyo kwa hayo, na wale wanaoghafilika na Aya zetu. Wote hao makazi yao ni Motoni kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma".
(Yunus - 7 - 8)
Na akasema:-
"Bila shaka mnayoahidiwa ni ya kweli na kwa hakika malipo bila ya shaka yatatokea".
(Ad - Dhariyat -5-6)
Na akasema:-
"Na kwamba Kiama kitakuja, hapana shaka ndani yake na kwa hakika MwenyeziMungu atawafufua walio makaburini."
(Al - Hajj -7)
Na akasema:-
"Waliokufuru wanadai kuwa hawatofufuliwa. Sema; "Kwa nini? Kwa haki ya Mola wangu nyinyi lazima mtafufuliwa; kisha lazima mtajulishwa mliyoyatenda na (mlipwe kwayo). Na hayo ni sahali (mepesi) kwa MwenyeziMungu".
(Attaghabun -7)
Na katika kauli Yake:
"Jee! wao hawafikiri ya kwamba watafufuliwa katika siku hiyo iliyo kuu siku watakaposimama watu wote mbele ya Mola wa walimwengu wote".
(Al -Mutafifin -5)
Na katika kauli yake:
"Naapa kwa Siku ya Kiama. Tena naapa kwa nafsi inayojilaumu; (kuwa mtafufuliwa na mtalipwa) anadhani mtu kuwa sisi hatutaikusanya mifupa yake? Kwanini! Sisi tunaweza (hata)kuzisawazisha ncha za vidole vyake".
 (Al - Kiyama - 1-4)
MwenyeziMungu akasema pia:-
"Nao (wakaapa) kwa jina la MwenyeziMungu kwa kiapo chao cha nguvu (kwamba)   
MwenyeziMungu hatawafufua wafao. (kwa nini asiwafufue?) Ni ahadi iliyolazimika kwake (kuwafufua na kuwalipa), lakini watu wengi hawajui.
Atawafufua ili kuwabainishia yale waliokhitilafiana, na ili wajue waliokufuru kwamba wao walikuwa waongo.
Kauli yetu kwa kitu tunachokitaka (kiwe) ni kukiambia "Kuwa ". Basi kinakuwa tu".
(An - Nahl 38- 40)
Na Aya kama hizo zipo nyingi sana.


2) Kujulishwa na Mtume (SAW) kama pale alipoulizwa na Jibrli (AS) 
 "Nijulishe juu ya Imani”
Mtume(SAW) akajibu;
"Kumwamini MwenyeziMungu na Malaika wake na vitabu vyake na Mitume wake, na Siku ya Kiama na kwa Qadari, kheri yake na shari yake".
(Bukhari na Muslim)
Hadithi za mfano huo zipo nyingi sana.

1.      Kukubaliana kwa dini zote zenye asili ya kushushiwa Wahyi, pamoja na imani ya mamilioni ya viumbe wakiwemo Mitume, Manabii, watu wenye Hekima, Maulamaa na Wacha Mungu, wote wakiamini kuwepo kwa Siku ya Kiama pamoja na yote yaliyoelezewa kuwa yatatokea siku hiyo na kuwa na imani isiyokuwa na shaka juu ya hayo.

2.      Uwezo wa MwenyeziMungu aliyeumba wa kuwarejesha tena viumbe vyake baada ya kuwafanya watoweke, kwa sababu kuwarudisha tena, si kazi ngumu kuliko kuumba mara ya mwanzo, pale alipoweza kuumba pasipo na mfano wake.

3.      Tunapata uhakika juu ya haya pia, kutokana na ukweli wa Mtume (SAW), "Msema kweli" mwenye miujiza na dalili zinazoilazimisha akili kuukubali ukweli wa ujumbe wake. Tumejulishwa pia kuwa MwenyeziMungu alimpandisha Mtume wake mbinguni na akaiona Pepo na Moto, na akatuletea maneno ya MwenyeziMungu aliyeumba uhai wa dunia na uhai mwingine na akatujulisha pia juu ya uhai unaotusubiri baada ya kufa kwetu.
4.      Kwa hivyo elimu yetu juu ya makazi ya akhera imetujia kutokana na asili zenye kuaminika kabisa. Kutoka kwa Yule aliyeumba dunia na akhera, na kutoka kwa Mtume wake aliyeziona Pepo na Moto.
5.      Hiyo ni ahadi ya mwenyeziMungu na MwenyeziMungu havunji miadi yake

6.      Mtume (SAW) ametuelezea pia juu ya ishara zitakazoonekana duniani, zikiwa ni alama za kukaribia kwa saa, na tukazishuhudia nyingi katika alama hizo, jambo linalotuhakikishia ukweli wa yale aliyotueleza Mtume(SAW) juu ya Siku ya Kiama.
7.      Kwa hivyo kama tulivyoziona alama hizo hapa duniani kweli kweli baada ya kupita miaka elfu moja na mia nne (tokea alipokuja Mtume(SAW)),  basi tutaziona pia Pepo na Moto kweli kweli.
8.      MwenyeziMungu anasema:-
9.      "Na watu wa Peponi watawaita watu wa motoni (waseme) "Sisi tumekuta aliyotuahidi Mola wetu kuwa ni kweli. Jee na nyinyi (Pia) mmekuta aliyokuahidini Mola wenu kuwa ni kweli?”
10. Wakasema (watu wa motoni) "Ndiyo" Basi mtangazaji atatangaza baina yao (aseme); "Laana ya MwenyeziMungu iko juu ya Madhalimu (waliodhulumu nafsi zao)".
11. (Al - Aaraf -44). 

1)       Aliyemuumba mwanadamu bila shaka atakuwa mkamilifu kuliko mwanadamu, na mwanadamu kwa kawaida hupenda  uadilifu. Bila shaka MwenyeziMungu ndie aliyeumba mapenzi hayo ya uadilifu ndani ya nafsi za binadamu waliotangulia na watakaokuja. Na uadilifu wa binaadmu wote pamoja, ni sawa na cheche ndogo tu ukilinganisha na uadilifu wa MwenyeziMungu. Kwani MwenyeziMungu ndiye Muadilifu Mwenye Hikima.

 Na katika uadilifu ni kulipwa mema kila atendae mema na kutiwa adabu mwenye kufanya maovu, lakini hapa duniani hapawezi kupatikana uadilifu huo kwa ukamilifu. Kwa vile tumekwishauelewa uadilifu wa MwenyeziMungu, kwa hivyo akili inahakikisha kwamba Mwenyezi Mungu lazima ataisimamisha mizani za uadilifu katika uhai ujao.
MwenyeziMungu anasema:-
"Jee!Tuwafanye wanaotii sawa na waasi? Mmekuwaje! Mnahukumu namna gani?".
(Al -Qalam -35 - 36)
Na akasema:-
"Nasi tutaweka mizani za udadilifu Siku ya Kiama, na nafsi yoyote haitadhulumiwa hata kidogo".
(Al - Anbiyaa - 47)
2)       Tukizingatia jinsi mbingu na ardhi zilivyoumbwa tunaona kuwa kila kitu kimewekwa mahali panaponasibiana napo sawa sawa. Mbingu na vilivyomo ndani yake kama vile nyota na sayari, usiku na mchana. Ardhi na vilivyomo ndani yake pia kama vile mimea na wanyama na wanaadamu na vitu visivyo na uhai, kila kitu kipo mahali panapostahiki kuwepo sawa sawa.
Moyo upo mahali pake na jicho lipo mahali pake na jani lipo mahali pake juu ya mti, na ua lipo mahali pake na hivi ndivyo ilivyo, hapana kitu chochote kilichohalifu amri  na kisiwe mahali pake kama kinavyotakiwa isipokuwa katika hali za wanadamu.
Tunamuona dhalimu yupo mahali asipostahili kuwepo, na utamuona Nabii aliyetumwa akifukuzwa na kuudhiwa na masafihi.
    Kwa nini basi hatuioni haki ikisimama katika maisha ya wanaadamu kama ilivyosimama katika kila kilichokuwemo ardhini na mbinguni?
Akili inatujulisha kuwa Aliyeumba mbingu na ardhi kwa haki, lazima siku moja ataisimamisha haki kwa ajili ya watu pia. Na iwapo haya hayawezi kutimia hapa duniani kwa vile hapa ni mahali pa majaribio na mitihani, basi hapana budi haki itasimama Siku ya Kiama.
"Jee! Wanafikiri wale waliofanya maovu kuwa tutawafanya kama wale walioamini na kutenda mema kwamba maisha yao yawe sawa sawa? Ni hukumu mbaya wanayoihukumu (ya kuwa wote watakuwa sawa) Na MwenyeziMungu ameziumba mbingu na ardhi kwa haki na ili kila nafsi ilipwe yale iliyoyachuma; nao hawatadhulumiwa”.
(Al - Jathiya - 21 22)
      Mwanadamu akitafakari namna gani MwenyeziMungu alivyomhifadhi na asimpoteze tokea pale alipokuwa tone la maji yaliyo dhalili (Manii) au pale alipokuwa kidonge cha damu, na pia namna gani MwenyeziMungu alivyochukuwa jukumu la kumhifadhi katika maisha yake yote.
Atakayetafakari juu ya yote haya, atakuwa na uhakika kwamba MwenyeziMungu hatompoteza mwanadamu kwa njia ya kifo na kumfanya apotee bure. Kwa sababu Mwenye Hikima anayezihifadhi sehemu ndogo ndogo za mwili, hatokipoteza kile alichokiumba kwa ukamilifu (ambaye ni mwanadamu aliye kamili).
MwenyeziMungu amesema:-
"Jee! anafikiri binaadamu kuwa ataachwa bure? Jee hakuwa tone la manii lililotonwa kisha akawa kidonge cha damu kisha akaumba na akamsawazisha (mwanadamu kamili)? Kisha akamfanya namna mbili, mwanaume na mwanamke. Jee! Hakuwa huyo ni muweza wa kuhuisha waliokufa ?
(Al - Qiyama -36 - 40).

MAISHA YA BARZAKH (BAADA YA KUFA)

Mwislamu anaamini kwamba Neema za kaburini na Adhabu zake pamoja na masuala atakayoulizwa na Malaika wawili kaburini mwake, ni haki na kweli kutokana na ushahidi ufuatao:-
MwenyeziMungu anasema:
"Hapana! Hakika hili ni neno tu analolisema yeye (aliye mwovu anapofikiwa na mauti) na mbele yao kuna maisha ya baada ya kufa (ya taabu kwa wabaya na ya raha kwa wazuri) mpaka siku watakapofufuliwa!".
(Al - Muminun - 100)
Na akasema:
"Na adhabu mbaya ikawazunguka hao watu wa Firauni pamoja naye. Adhabu ya Motoni wanadhihirishiwa (makaburini mwao) asubuhi na jioni na siku ile kitakapotokea Kiama (kutasemwa); "Waingizeni watu wa Firauni katika adhabu kali zaidi".
(Al - Muminun - 45 - 46)
Na pia akasema:-
"MwenyeziMungu huwathubutisha wale walioamini kwa kauli thabiti katika maisha ya dunia na katika akhera."
(Ibrahim - 27)
Na Mtume (SAW) amesema:
<<Hakika mja baada ya kuwekwa kaburini mwake, pale watu wake wanapoondoka huwa anasikia vishindo vya viatu vyao. Basi hujiwa na Malaika wawili wakakaa naye na kumuuliza: "Ulikuwa ukisema nini juu ya mtu huyu (aitwae) Muhammad (SAW)?"
Muislamu hujibu:
"Ninashuhudia kwamba yeye ni mjumbe wa MwenyeziMungu na Mtume wake."
Ndipo atakapoambiwa;
"Yaangalie (yaliyokuwa) makazi yako ya Motoni, MwenyeziMungu amekupa badala yake makazi ya Peponi".
Kisha atayaona makazi yote mawili, na kaburi litapanuliwa ili pawe na nafasi kubwa.
Ama mnafiki au kafiri anapoulizwa;
"Ulikuwa ukisema nini juu ya mtu huyu?”
Yeye hujibu;
"Sijui! Nilikuwa nikisema kama wasemavyo watu."
Basi huambiwa;
"Hukujua wala hukusoma"
Kisha anapigwa kwa nyundo ya chuma pigo moja, na hupiga ukelele unaosikika na viumbe vyote waliokuwa naye isipokuwa wanadamu na majini>>.
Na Mtume (SAW) pia akasema:
<<Mmoja wenu anapokufa huonyeshwa makazi yake mchana na usiku.  Akiwa katika watu wa Peponi basi (huonyeshwa) ya Peponi na akiwa katika watu wa Motoni  basi (huonyeshwa) ya Motoni, kisha huambiwa;
"Haya ndiyo makazi yako atakapokufufua MwenyeziMungu Siku ya Kiama>>.

Siku moja Mtume(SAW) alipokuwa akipita baina ya makaburi mawili alisema:
(1)<<Hawa wanaadhibiwa, na wala hawaadhibiwi kwa makubwa, (bali hivyo) bali mmoja wao alikuwa akifanya Namima (na maana yake ni ‘kuchukua maneno ya huku na kuyapeleka kule) ama mwengine alikuwa hajikingi na mkojo wake>>[8].
Na katika dua zake, Mtume (SAW) alikuwa akisema:
<<MwenyeziMungu najikinga kwako kutokana na Adhabu ya Kaburini na Adhabu ya Motoni na kutokana na mitihani ya maisha na ya kifo>>.
Zipo hadithi nyingi kama hizo za kuaminika kabisa zilizofikia daraja la ‘Tawatur’.

USHAHIDI WA KIAKILI.

1)         Imani juu ya MwenyeziMungu na Malaika wake na Vitabu vyake na Mitume yake na juu ya Siku ya Kiama, inamlazimisha mtu kuamini pia juu ya adhabu za kaburini na neema zake na kila kinachotendeka humo, na hii ni kwa sababu vyote hivyo ni katika Elimu ya Ghaibu.
Kwa hivyo anayeamini baadhi ya hayo, akitumia akili yake ataona kwamba hana budi kuyaamini yote yaliyobaki.
2)         Adhabu na neema za kaburini pamoja na masuali yanayoulizwa na Malaika wawili si katika mambo ambayo akili haiwezi kuyakubali na wala si jambo lisilowezekana kuwa, bali kinyume cha hivyo, akili inayakubali na kuyashuhudia hayo.
Mtu anapolala (kwa mfano), huota na kuyaona mambo anayoyapenda na akayaonea raha, yakamfurahisha nafsini mwake, jambo ambalo humfanya ahuzunike pale anapoamka na kukatika utamu wa  ndoto yake.
Wakati huo huo mtu anaweza kuota ndoto asiyoipenda, ikamhuzunisha na kumfanya amshukuru yule aliyekuja kumwamsha.
Hizi ni Neema au Adhabu za usingizini tu, huingia katika roho kwa uhakika, na roho huathirika nazo; na haya ni matukio ambayo hatuyahisi wala kuyashuhudia kwa uhakika, lakini hakuna anayeyakanusha.
Vipi basi mtu anakanusha adhabu za kaburini na neema zake?

VITISHO VYA SIKU YA KIAMA

Tunavishuhudia vitisho vya Siku ya Kiama katika aya mbali mbali za Qurani.
Miongoni mwa aya hizo ni kauli yake MwenyeziMungu isemayo:
"Jua litakapokunjwakunjwa.
Na nyota zitakapopukutika.
Na milima itakapoendeshwa (angani kama vumbi).
Na ngamia wenye mimba pevu watakapokusanywa.
Na bahari zitakapowashwa moto.
Na roho zitakapounganishwa (na viwiliwili vyake).
Na mtoto mwanamke aliyezikwa hali ya kuwa yu hai atakapoulizwa kwa makosa gani aliuawa?
Na madaftari ya amali yatakapoenezwa (kila mtu apewe lake).
Na utando wa mbingu utakapotanduliwa.
Na Jehannam itakapochochewa.
Na Pepo itakaposogezwa".
(At - Takwiyr -1 - 13).
Na katika kauli Yake:-
"(Wakumbusheni) Litakapotokea tokeo (hilo la Kiama).
Ambalo kutokea kwake si uwongo.
Lifedheheshalo (wabaya). Litukuzalo (wazuri).
Ardhi itakapotetemeshwa mtetemeko mkubwa.
Na milima itakaposagwa sagwa.
Iwe mavumbi yanayopeperushwa".
(Al - Waqiah - 1 - 6)

Na katika kauli Yake:-
"Enyi watu! Mcheni Mola wenu, hakika utetemeko wa Kiama ni jambo kubwa (kabisa).
Siku mtakapokiona (hicho Kiama) kila mwanamke anyonyeshaye atamsahau amnyonyeshaye na kila mwenye mimba ataizaa mimba yake (kabla ya wakati kufika).
Na utawaona watu wamelewa kumbe hawakulewa.
Lakini ni adhabu tu ya MwenyeziMungu (hiyo) iliyo kali."
(Al - Hajj - 1 - 2)

Na katika kauli Yake:
"Basi itakapokuja sauti kali iumizayo masikio(sauti ya baragumu la Kiama).
Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye na mamaye na babaye.
Na mkewe na wanawe.
Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na hali itakayomtosha mwenyewe (hana haja ya wenziwe)".
ABASA  - 33 - 37

 

 

 

 

 

PEPO NA MOTO


PEPO

   Ni makazi ya wanaomuabudu Mungu mmoja tu, na makazi ya walioamini na kutenda mema, na ya waliomcha Mungu wao, na ya waja wa Mungu waliosafishwa, na ni makazi ya wale wanaomuogopa Mungu wao na ya wanaotimiza ahadi ya Mwenyezi Mungu wanapoahidi, na ya wapiganao Jihadi katika njia ya MwenyeziMugnu kwa nafsi zao na mali zao,  na wanaotubu, wanaomuabudu MwenyeziMungu na kumshukuru, wanaomsujudia na ya wenye kuamrisha mema na kukataza maovu.
   Na Mwenyezi Mungu Subhanahau wa Taala amekwisha bainisha wazi katika kitabu chake kitukufu juu ya Pepo na neema zake na Mito yake na Miti yake na Matunda yake na Vyakula na Vinywaji vyake, na juu ya Nguo na Mavazi na Mapambo yake, na juu ya Nyumba zake na Vyumba vyake, Wanawake wake walio wazuri. Akaeleza kwamba neema zake hazifanani hata kidogo na neema za hapa duniani.
MwenyeziMungu anasema:-
"Nafsi yoyote haijui waliyofichiwa katika hayo yanayofurahisha macho (huko Peponi); ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyafanya.
(As - Sajdah - 17)


Na Mtume (SAW) katika hadith ya Al Qudusiy akasema:-
MwenyeziMungu anasema;
<<Nimewatayarishia waja wangu walio wema yale ambayo hapana jicho lililowahi kuyaona wala sikio kuyasikia, na wala hayakupata kumpitikia mtu yeyote (akilini mwake)>>.

MOTO.

1 ya makafiri na wanaotakabari katika kumtii MwenyeziMungu na katika kumuabudu.  MwenyeziMungu ametujulisha juu ya wasfu wa kuni zake na moto wake unaowaka vikali kabisa, na akaelezea juu ya vyakula na vinywaji vya watu wa Motoni, na akaelezea pia adhabu zake kwa ajili ya kuingiza hofu katika nyoyo za wahalifu, na ili kumtisha kila mwenye kutakabari na kujifanya kuwa ni jabari muovu, ili ayaache maovu anayoyafanya.
Mwenye kupata adhabu hafifu kabisa katika watu wa motoni ni yule atakayekewa viatu viwili au nyuzi za viatu za moto chini yake vinamuunguza mpaka ubongoni mwake kama inavyoungua sufuria ya kuchemshia maji, na hujiona kama kwamba yeye ndiye anayeadhibiwa kupita wote Siku ya Kiama.
Kwa atakae maelezo zaidi juu ya wasfu wa Pepo na Moto basi asome Qurani na hadithi za Mtume (SAW) na atapata mengi yakutosheleza humo.



FAIDA YA KUAMINI SIKU YA KIAMA.

Kuwa na Imani juu ya Siku  ya Kiama kunayafanya maisha yetu yawe na maana na yawe na lengo lililo bora, lengo ambalo linamfanya mtu apende kufanya yaliyo mema na kuacha maovu, kujipamba kwa fadhila na kujiepusha na maovu yanayodhuru miili na kuidhuru dini na heshima na yanayodhuru akili na mali.


VIPI TUTAFUFULIWA


ASILI TATU ALIZOUMBIWA MWANADAMU

Mwanadamu ameumbwa kutokana na Asili Tatu:-
1)     Asili ambayo ameirithi kutoka kwa Adam (AS) ambayo imekuja pamoja na tone la manii (mbegu).
2)     Udongo, ulioingia mwilini kwa njia ya chakula, mwili ukakuwa na kujengeka pamoja na asili ya mwanzo aliyoirithi kutoka kwa Adam (ambayo ni mbegu).
3)     Roho, iliyopulizwa katika mwili wa kiumbe akiwa bado yumo tumboni mwa mamake.

WAKATI WA MTIHANI NA MWISHO WAKE

Kutokana na mchanganyiko wa vitu hivyo vitatu (asili hizo tatu) na kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu, anapatikana mwanadamu aliye hai mwenye kupitisha wakati wake wa mtihani hapa duniani.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Ambaye ameumba mauti na uhai ili kukujaribuni (kukufanyieni mtihani) ni nani miongoni mwenu mwenye vitendo vizuri zaidi".
 Al Mulk - 2
Muda wa mtihani utakapomalizika, na wakati wa kutoka na kwenda kwenye makazi ya malipo utapofika, ndipo mauti yanapokuja.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Utakapowafikia muda wao hawatakawia (hata) saa moja wala hawatatangulia (kabla haujafika)".
Al Aaraf -34

Na anasema:
"Lakini Mwenyezi Mungu hataiakhirisha nafsi yo yote inapokuja ajali yake"
Al Munafiqun - 11

MTU ANAPOKUFA, ZILE ASILI TATU KILA MOJA INARUDI MAHALA PAKE PA ASILI

Kwa kifo, udongo ambao kwao ndio mwili ulijengeka, unarudi mahala pake pa asili napo ni ardhini.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Kwa hakika tunajua kiasi cha kila kinachopunguzwa na ardhi katika miili yao (wakati wanapooza huko makaburini) Na kwetu kiko kitabu kinachohifadhi (kila kitu)".
Qaf -4
Kinachobaki katika mwili wa mwanadamu ni kitu kidogo kinachoitwa "Ajabu dhanab" (kilichoingia pamoja na mbegu). Hii ni sehemu ambayo ndani yake mtu aliumbiwa, na kitu hiki asili yake kilikuwa katika uti wa mgongo wa Baba yetu Adamu(AS), kwa vile kitu hiki ni kidogo sana (Hakiwezi kuonekana ila kwa kutumia microscope zenye nguvu sana), ndiyo maana uti wa mgongo wa Baba yetu Adamu(AS) uliweza kuzibeba asili hizi zote za wanawe.
Na sehemu hii iitwayo "Ajabu dhanab" haiozi wala haivurugiki.
Mtume(SAW) amesema:-
<<Mwili wote wa mwanaadamu unaoza isipokuwa "Ajabu dhanab", kutokana nayo ameumbwa na kutokana nayo atakusanywa tena >>.
Bukhari – Muslim – An Nasai, Malik katika Muwata a na Abu Daud.

Ama Roho itarudi mahali anapopataka MwenyeziMungu (katika Barzakh) mpaka Siku ya Kiama.

SIKU YA KUFUFULIWA ZILE SEHEMU TATU ZINAKUSANYIKA TENA

Unapofika wakati wa kufufuliwa, MwenyeziMungu atateremsha mvua na kuifanya ile mbegu isiyooza "Ajabu dhanab”, imee tena.
Mtume (SAW) amesema:-
<<Kisha inateremshwa mvua na watamea kama imeavyo mboga, na hapana katika mwili wa mwanadamu kisicholiwa na ardhi isipokuwa fupa moja nalo ni "Ajabu dhanab" ndani yake humo watakusanywa viumbe Siku ya Kiama>>.
(Bukhari, Muslim, Imam Malik, Abu Daud na AnNasaiy)

Yaliyofanana na haya yanatokea duniani kila siku. Panapotokea ukame, tunaona miti ikianguka na kufa (na kutoweka). Hauonekani mti wowote wala mmea. Lakini Mwenyezi Mungu amejaalia ndani ya ardhi au ndani ya mawe kuwemo mbegu, na mbegu hizo hazionekani kwa macho, isipokuwa mvua inaponyesha ndipo hupasuka na kuchipua miti na mimea mbali mbali.
MwenyeziMungu anasema:-
"Hukitoa kilicho hai katika kilichokufa na hukitoa kilicho kufa katika kilicho hai na huihuisha ardhi baada ya kufa kwake na hivyo ndivyo mtakavyofufuliwa".
(Al - Rum - 19).
Mtu mmoja alimuuliza Mtume (SAW):-
"Ewe Mtume wa MwenyeziMungu, namna gani MwenyeziMungu atawarudisha tena viumbe, na nini dalili yake?”
 Mtume (SAW) akamjibu;
"Uliwahi kupita bondeni kijijini kwenu wakati wa ukame (miti yote ikiwa imekufa), kisha ukapita tena wakati miti (imeota tena na) imejaa na ardhi ikageuka (na kuwa) rangi ya kijani?
Akasema:- "Naam".
Mtume(SAW) akamjibu:
"Basi hiyo ndiyo dalili ya MwenyeziMungu katika kuumba kwake na hivyo ndivyo atakavyowafufuwa wafu".
(Imam Ahmad )

(Siku ya Kiama), Pale Ajab dhanab itakapochipua na kutoka ndani ya ardhi na mwili ukarudi tena, ndipo zitakapokuja roho na kuingia kila moja katika mwili wake.
Ndio sababu MwenyeziMungu akasema:
"Na nafsi zitakapounganishwa (na viwiliwili vyake)."
(At - Takwiyr - 7)
Na hivi ndivyo watakavyorudi viumbe mara ya pili kama walivyoanzishwa hapo mwanzo.

MwenyeziMungu anasema:-
"Kama tulivyoanza umbo la awali tutalirudisha tena, ni ahadi ilio juu yetu, bila shaka sisi ni wenye kufanya (tusemavyo).”
(Al - Anbiyaa -104).

JIBU KWA WANAOIKADHIBISHA SIKU YA KIAMA.

Inatosha kuwajibu wanayoikanusha Siku ya Kiama kama walivyojibiwa na MwenyeziMungu, katika kauli yake:-
"Enyi watu! Kama mumo katika shaka juu ya ufufuo; (mnaona haimkiniki kufufuliwa) basi (tazameni namna tulivyokuumbeni) Kwa hakika tulikuumbeni kwa udongo (Mzee wenu Nabii Adam), kisha (tukawa tunakuumbeni nyinyi) kwa manii (mbegu ya uhai) kisha (yanageuka) kuwa kipande cha damu, kisha huwa kipande cha nyama kinachoumbika (kinachofanyika sura) na kisichoumbika ili tukubainishieni (Kudra yetu). Nasi tunakikalisha matumboni tunachokitaka mpaka muda uliowekwa, kisha tunakutoweni kwa hali ya utoto, kisha (tunakuleeni) ili mfike baleghe yenu. Na kuna wanaokufa (kabla ya kufikia hali hii). Na katika nyinyi wako wanorudishwa katika umri dhalili; asijue chochote baada ya kule kujua kwake; na unaiona ardhi imetulia kimya lakini tunapoyateremsha maji juu yake, inataharaki na kukua na kuotesha kila namna ya mimea mizuri.
Hayo ni kwa sababu MwenyeziMungu yuko, na kwamba Yeye huwahuisha wafu, na kwamba Yeye ndiye Mwenye uweza juu ya kila kitu.
Na kwamba kiyama kitakuja, hapana shaka ndani yake; na kwa hakika MwenyeziMungu atawafufua walio makaburini".
(Al - Hajj - 5 - 7)
Na katika kauli Yake:-
"Jee! Mwanaadamu hatambui ya kwamba tumeemuumba kwa tone la manii. Amekuwa hasimu yetu aliye dhahiri (sasa)?
Na akatupigia mfano na akasahau kuumbwa kwake(kwa manii) akasema: "Nani atakaeihuisha mifupa na hali imesagika?"
Sema: “Ataihuisha yule aliyeumba mara ya kwanza naye ni Mjuzi wa kila (namna ya) kuumba”. Ambaye amekufanyieni moto katika mti mbichi, (nanyi) mkawa kwa (mti) huo mnauwasha.
Jee yule aliyeziumba mbingu na ardhi (mnaona) hana uwezo wa kuumba (mara ya pili) mfano wao (wanadamu)? Kwa nini? Naye ni muumbaji mkuu, Mjuzi wa kila jambo.
Hakika amri yake anapotaka chochote (kile kitokee) ni kukiambia "Kuwa," basi mara huwa. Ametukuka yule ambaye mkononi mwake umo ufalme wa kila kitu; na kwake mtarejezwa nyote."
(Yaasin -77 -84)

Na kauli Yake MwenyeziMungu;
"Qaf. Naapa kwa hii Qurani tukufu (kuwa mtafufuliwa).
Bali wanastaajabu ya kwamba amewajia muonyaji kutoka miongoni mwao (Wanataka awe Malaika). Na wakasema makafiri "Hili jambo la ajabu!"
Kuwa tutakapokufa na tukawa udongo (kuwa tutafufuliwa)?
Marejeo hayo ni ya mbali kabisa (hayawezi kuwa).
Kwa hakika tunajua kiasi cha kila kinachopunguzwa na ardhi katika miili yao (wakati wanapooza makaburini). Na kwetu kiko kitabu kinachohifadhi (kila kitu).
Lakini waliikadhibisha haki ilipowajia na wamo katika jambo la mkorogeko.
Jee! hawazioni mbingu zilizo juu yao! tumezijengaje na tumezipambaje wala hazina nyufa".
(Qaf - 1- 6)


SITA: IMANI JUU YA QADAR "KUDRA" (Majaliwa- YALIYOKWISHA ANDIKWA)

 

MAANA YA KUDRA

MwenyeziMungu alitaka kuumba viumbe(akaumba), kisha akavipangia ajali zake na kuvipa viumbe hivyo vipimo maalum.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na ameumba kila kitu na akakikadiria kipimo (chake)".
(Furqan - 7)
Kwa vile Yeye ni Mwenye kujua kila kitakachowatokezea viumbe vyake, akaiamrisha kalamu iandike katika ubao uliohifadhiwa (Lauhi l Mahfudh) yote yatakayo tokea hadi Siku ya Kiama.
MwenyeziMungu anasema:-
"Jee! Hujui ya kwamba MwenyeziMungu anajua yaliyoko mbinguni na ardhini? Bila ya shaka (yote) hayo yamo Kitabuni (mwake); Hakika (kudhibutu) hayo kwa MwenyeziMungu ni sahali".
(Al - Hajj - 70)
     Na kila kilichokuwepo ulimwenguni katika vinavyotaharaki na vilivyotulia, vyote  hivyo huwa kama apendavyo MwenyeziMungu na kwa uwezo wake Subhanahu Wa taala.
MwenyezMungu anasema:-
"Anaumba apendavyo; Naye ni Mjuzi Mwenye uweza."
(Ar - Rum - 54)
Wala hakitendeki chochote ila kwa uwezo wa MwenyeziMungu na kama apendavyo.
MwenyeziMungu anasema:-
"Wala usiseme kamwe kwa lolote lile kuwa "Nitalifanya kesho" Isipokuwa uongeze "Inshaallah" (MwenyeziMungu akipenda)."
(Al - Kahf - 23 - 24)
Kwa hivyo atakacho MwenyeziMungu kinakuwa, na asichotaka hakiwi.

IMANI JUU YA QADAR “KUDRA’.

Imani juu ya Kudra (Majaliwa) ni nguzo mojawapo katika nguzo za Imani kama alivyotubainishia Mtume (SAW) katika hadithi ya Jibril(AS), aliposema:-
Na uamini juu ya Kudra, kheri yake na shari yake.
Mwanadamu yeyote hawezi kuzizunguka kwa kuzijua siri za MwenyeziMungu isipokuwa labda elimu yake iwe sawa na ilimu ya MwenyeziMungu - na hili ni jambo lisilowezekana.
Huoni basi mfano wa kazi wanazofanya madaktari na wenye ujuzi na wahandisi katika kazi ambazo wengine wasiokuwa wao hawazijui sawa sawa, isipokuwa yule ambaye elimu yake imefikia daraja ya elimu zao?
Kwa mfano mtu mjinga, asiyeijua kazi ya madaktari anapomwona daktari anapasua tumbo la mgonjwa na kuanza kukata matumbo yake, hatokubali, na huenda  akafanya zogo, lakini mara atakapoelewa kwamba daktari ni mtu mwenye hekima na kwamba anaijua kazi yake vizuri, mtu huyo ataacha ubishi wake huku akikiri juu ya ujinga wake na kusalimu amri mbele ya elimu ya Daktari.
Mwislamu anauelewa vizuri ukamilifu mkubwa kabisa wa Mola wake, ndio maana anaamini kwamba lolote linalotokea, basi haliwi isipokuwa lina hekima ya MwenyeziMungu ndani yake.
Na iwapo hajaielewa hekima ya MwenyeziMungu katika jambo lolote lile, huutambua ujinga wake mbele ya elimu ya MwenyeziMungu, na kwa ajili hiyo huacha kubisha kwake na kujisalimisha mbele ya Mwenye Hekima, Mwenye Ujuzi, Mwenye Ilimu anayesema:-
"Haulizwi (MwenyeziMungu) anayoyafanya (Kwani yote ni ya haki) lakini wao viumbe wataulizwa".
(Al Anbiyaa - 23)
 

KATIKA MATUNDA YA KUAMINI KUDRA (KUDRA)

Mwenye kuamini kwamba MwenyeziMungu ameumba kila kitu kwa kukikadiria, utamwona anajitahidi sana katika kutafuta mambo yaliyokadiriwa ya kheri ili apate kuyasukumizia mbali yale ya shari.
Anaondoa Kudra(majaaliwa) ya njaa kwa kutumilia kudra(majaaliwa) ya chakula, na kudra ya ugonjwa kwa kutumia kudra ya dawa na kudra ya ufakiri anaiondoa kwa kutumia kudra ya kutafuta riziki.
Kwa yule mwenye Imani kamili juu ya kudra, utamwona hahuzuniki kwa jambo lolote lile alolikosa au kumpotea, na wala havunjiki moyo anapopatwa na masaibu, wala hajifakharishi au kutakabari anapofanikiwa au kubahatika na jambo lolote lile,  siku zote anaiamini kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"Hautokei msiba katika ardhi wala katika nafsi zenu ila umekwisha andikwa katika kitabu (cha MwenyeziMungu) kabla hatujauumba. Kwa yakini hilo ni sahali kwa MwenyeziMungu. Ili msihuzunike sana juu ya kitu kilichokupoteeni wala msifurahi sana kwa alichokupeni na MwenyeziMungu hampendi kila ajivunae na ajifakharishae."
(Al - Hadid -22-23).
Mwenye kuamini Kudra ya MwenyeziMungu na uwezo Wake na matakwa Yake kisha akaujua udhaifu wake(mwanadamu huyo) na jinsi anavyomuhitajia Muumba wake, utamwona siku zote ni mkweli katika kumtegemea Mola wake.
Anakubali kwamba kila kinachomfikia au kumsibu kuna sababu ambayo MwenyeziMungu keshazikadiria, na humuomba Mola wake msaada kwa yale asiyomuwezeshea.
Kila wakati huikariri kwa yakini kauli ya MwenyeziMungu isemayo:-
"Sema 'Halitatusibu ila alilotuandikia MwenyeziMungu, Yeye ni Mola wetu', basi Waislamu wamtegemee MwenyeziMungu tu".
(At - Tawba -21)

MAMBO MAWILI YANAYOBABAISHA WATU

La kwanza:

Baadhi wa wajinga wanadai kwamba MwenyeziMungu ndiye aliyewafanya wao wapotee na kuwafanya wasisali wala kufunga wala kutii amri nyengine zozote za dini, na akawaongoza wengine. Kisingizio chao kikiwa ni katika kauli ya MwenyeziMungu alipomwambia Mtume wake (SAW):-
"Kwa hakika wewe huwezi kumuongoza umpendae, lakini MwenyeziMungu humuongoza amtakaye, naye anawajua waongokao (kwa hivyo anawaongoa, na anawajua wasiotaka kuongoka kwa hivyo anawachilia mbali)".
(Al - Qasas -56).
     Wale wanaopenda kuzungumza juu ya mambo haya yanayobabaisha, hawaelewi kwamba hidaya  imegawika sehemu mbili;
1)     Hidaya ya Kuongoza.
2)     Hidaya ya Msaada.
Hidaya ya Kuongoza, ni mfano wa mtu anayekuonyesha njia ya kukufikisha nyumba uitakayo kisha akakuacha baada ya kukuongoza na kukufikisha penye njia itakayokupeleka huko.
Mitume ya MwenyeziMungu(AS), kazi yao ndio hii ya kuongoza wanaadamu na kuwaonyesha njia itakayowafikisha Peponi.
MwenyeziMungu akimwambia Mtume wake(SAW) anasema:-
"Na kwa yakini wewe unaongoza katika njia iliyonyooka".
(A- Shuraa -52)
Ama hidaya ya Msaada, mfano wake ni mfano wa mtu aliye karimu, mwenye huruma, mpole, unapomuuliza njia ya kukufikisha nyumba uitakayo, akakuonyesha njia hiyo, kisha ukamuomba akusaidie zaidi, akakuchukua katika gari lake na akakushika mkono mpaka akakufikisha pale unapotaka kwenda.
Hii ndiyo hidaya ya Msaada, na hidaya hii haipati isipokuwa yule aliyeikubali kwanza hidaya ya kuongozwa, kisha akaomba msaada wa kufikishwa.
Kwa vile Mitume ya Mwenyezi Mungu(AS), kazi yao ni kuwapa watu hidaya ya Kuongoza, wao hawana uwezo wa kuwapa watu hidaya ya Mafanikio au ya Msaada, kwa sababu mwenye kutoa hidaya hii ni  Mwenyezi Mungu aliyetukuka, na hampi isipokuwa yule tu anayemjua kuwa anastahiki kupewa.
MwenyeziMungu akimuambia Mtume wake(SAW) anasema:-
"Kwa hakika wewe huwezi kumuongoza umpendaye, lakini MwenyeziMungu humuongoza amtakaye, naye anawajua waongokao (kwa hivyo anawaongoa na anawajua wasiotaka, kwa hivyo anawachilia mbali)".
(Al - Qasas -56)
Kwa hivyo Mwenyezi Mungu ambaye ni Muadilifu, anawaahidi wale waliyoikubali hidaya ya Kuongozwa na kuwapa hidaya ya Mafanikio na Msaada.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na wale wanaokubali kuongoka anawazidishia uongofu na anawapa (jaza) ya ucha Mungu wao".
(Muhammad - 17)
Kwa hivyo MwenyeziMungu hamuachi kupotea isipokuwa yule tu anayestahiki kuachwa kwa kuikataa hidaya ya Kuongozwa na kuendelea kwenda mbali na njia ya haki.

MwenyeziMungu anasema:-
"Basi walivyoendelea na uovu wao, MwenyeziMungu aliziachilia nyoyo zao zipotoke (kama walivyotaka wenyewe) na MwenyeziMungu hawaongoi watu waovu (wenye kutoka katika utiifu wake".
(As  - Saaf -5)

La Pili:

Baadhi ya wajinga wanasema;
"Kwa vile MwenyeziMungu keshaandika kila kitu juu ya ubao (Lauhu l mahfudh) ndio maana ikawafanya wasiosali wasisali  na wanaosali wawe wanasali".
Haya ni mawazo ya kipuuzi kwani anayesali huwa anasali kwa hiari yake mwenyewe bila ya kulazimishwa, na asiyesali huacha kusali kwa hiari yake mwenyewe pia bila ya kulazimishwa wala kuambiwa.
Kila mtu anayaelewa haya vizuri kabisa, kwa sababu MwenyeziMungu ametaka aumbe mwanaadamu (na akamuumba) akiwa amempa uhuru na hiari ya kujichagulia alipendalo.
Mtu huenda akauliza:-
"Kwanini basi isiwe yale yaliyokwisha andikwa katika ubao ndiyo yanayomlazimisha mtu afanye hayo, kwa sababu yameandikwa tokea dunia ilipoumbwa".
Tunasema hivi;
Jibu lake ni rahisi, na tutalifafanua kwa mfano huu:
Huoni kwamba mwalimu aliye hodari anayewajua vizuri wanafunzi wake, anapotoa masuali ya mtihani, iwapo ataandika katika karatasi majina ya wanafunzi ambao ana hakika kuwa watafeli katika mtihani huo, na akaandika majina ya wale ambao ana hakika kwamba watapasi, kisha mtihani ukafanywa na matokeo yakajulikana, kisha wakaja wale waliofeli wakamlaumu mwalimu wakisema:
"Kwa vile mwalimu keshaandika majina yetu kwenye karatasi yake kwamba tutafeli basi yeye ndiye sababu ya kufeli kwetu".
Jee! udhuru wao utakubalika? Ama wataambiwa kwamba:
"Alivyoandika mwalimu katika karatasi kunaambatana na kukujueni vizuri nyinyi wanafunzi wake, na kufeli kwenu kunatokana na uzembe wenu, kwa hivyo msiutafutie uzembe wenu kisingizio na kumlaumu mwalimu wenu kwa sababu ya kukujueni vizuri (yupi katika yenu anayejitahidi na yupi mchezaji)".
MwenyeziMungu ndie mwenye sifa Tukufu zaidi, kwani Yeye Aliyetukuka Muumba wa viumbe ndie anayewajua vizuri viumbe wake.
MwenyeziMungu anasema:-
"Oh! Asijue aliyeumba! Naye ndie avijuaye visivyojulikana na vinavyojulikana".
(Al - Mulk 14)

MwenyeziMungu Mtukufu ametuumba ili tupitishe wakati wa kufanyiwa mtihani hapa duniani akiwa Yeye Mwenye Shani ya juu kabisa anajua matokeo ya mtihani huo,  akawaandikia (kuwa watatenda) maovu wale waovu na akaandika yaliyo mema kwa walio wema, kutokana na  elimu Yake iliyokizunguka kila kitu. Kwani Yeye ndiye anayejua yaliyokuwa na yatakayokuwa.
Huenda Mwalimu akakosea katika kukadiria matokeo ya mtihani wa mwanafunzi wake, lakini MwenyeziMungu hawezi kukosea katika kukadiria amali za viumbe vyake, na maandishi yaliyo katika ubao (Lauhul Mahfudh) yanaambatana na elimu ya MwenyeziMungu iliyokitangulia kila kitu.
Kwa hivyo kutokusali, ni jambo lililoambatana na uasi na uzembe wa yule aliyeacha kusali.
Wajinga wanataka kuutafutia udhuru upotevu wao huo na maasi yao hayo, kwa kuisingizia ilimu ya MwenyeziMungu na Ukamilifu wake.
Elimu ya MwenyeziMungu imetangulia kuvijua vitendo, lakini haimlazimishi mtu kutenda (kila mtu ana hiari ya kutii au kuasi), na MwenyeziMungu amekwishamjulisha Mtume wake (SAW) yale yatakayotokea hadi Siku ya Kiama na tumeona hapo mwanzoni katika Dalili za Kiama kwamba mengi ya yale aliyoyataja Mtume(SAW) kuwa yatatokea yale ambayo Waislamu waliyaandika katika vitabu vya hadithi za Mtume(SAW), tunayaona yakitokea hivi sasa.
Jee anaweza mtu kudai kwamba kwa vile Waislamu waliyaandika katika vitabu vyao, ndio sababu yakatokea?
Sivyo. Bali elimu ya MwenyeziMungu juu ya matokeo hayo imetangulia kwa kujua ni nani atakayeyaleta hayo matokeo, lakini hayakumlazimisha mtu kuyatenda.


MATENDO YANAYOIJENGA YA IMANI

1-  KUYAKUBALI NA KUYASADIKI YOTE YALIYOKUJA KUTOKA KWA MWENYEZIMUNGU

Mwislamu anatakiwa ayakubali yote aliyotujulisha MwenyeziMungu katika kitabu chake, pamoja na yote aliyotamka Mtume wake mkarimu(SAW).  Ayakubali na kuyasadiki usadikisho wa kweli usio na shaka yoyote ndani yake.
Mwislamu anatakiwa pia aamini kwamba lolote lile lililopingana au linalopingana na yale aliyotujulisha MwenyeziMungu ni batil na halifai hata wakilipambaje wenye hilo jambo au kuligeuza geuza.
Hii ni kwa sababu itikadi yake ni kuwa Dini inatoka kwake Mwenye Kujua, Mwenye Hikima, Aliyekizunguka kila kitu kwa ilimu yake.
MwenyeziMungu anasema:-
"Basi ni lipi likupalo kukadhibisha Malipo baada (ya kuona hayo)?
Jee! MwenyeziMungu si Hakimu Muadilifu kuliko mahakimu wote?(basi si lazima atawalipa kwa mema yao na mabaya kwa mabaya yao?)”
At Tiyn- 7-8
    

2-  KUMTII MWENYEZIMUNGU NA KUMTII MTUME WAKE(SAW)

Hii ni kwa sababu anayemwamini MwenyeziMungu na akamwamini Mtume wake, kisha akawa na yakini kwamba waadi wa MwenyeziMungu ni wa kweli na kwamba MwenyeziMungu keshatayarisha malipo na thawabu kwa yule atakaemtii Yeye na akamtii Mtume wake(SAW) kisha akafuata amri Zake na amri za Mtume wake(SAW).
Kwa Imani yake hiyo, atalazimika ajisalimishe kwa kuzifuata amri za MwenyeziMungu na za Mtume wake(SAW), na hii ni kwa sababu Mwislamu anatakiwa awe anachunga kila alitendalo likubaliane na mafundisho ya kitabu cha MwenyeziMungu pamoja na Sunnah (mafundisho) ya Mtume wake (SAW).
MwenyeziMungu anasema:-
"Na wenye kumtii MwenyeziMungu na Mtume, basi hao watakuwa pamoja na wale aliowaneemesha MwenyeziMungu; Manabii na Masidiki na Mashahidi na Masalih (watu wema). Na uzuri ulioje (kwa mtu) watu hao kuwa rafiki (zake).”
(An - Nisaa -69)
Na akasema:-
"Mwenye kumtii Mtume (basi) amemtii MwenyeziMungu (kwani anayoamrisha Mtume yanatoka kwa MwenyeziMungu) Na anayekengeuka (anajidhuru mwenyewe). Hatukukupeleka wewe kuwa mlinzi juu yao (wakipotea ulaumiwe wewe, la hatukufanya hivyo)".
(An - Nisaa - 80)
Na Mtume (SAW) amesema:-
<<Umma wangu wote utaingia Peponi isipokuwa waliokataa>>.
Akaulizwa "Ni nani hao waliokataa?"
Akasema;
<<Atakayenitii ataingia Peponi na atakayeniasi basi amekataa>>>
Bukhari katika sahihi yake na imepokelewa kutoka kwa Abu Hurairah

3-  KUTEKELEZA FARADHI

Imani inapoingia na kujaa moyoni, itavifanya viungo vya mwili vifanye amali njema inayolingana na Imani hiyo  na kumfanya mwenye Imani hiyo kujitahidi kuyatekeleza yale aliyofaradhishiwa.
Ama yule asiyetekeleza faradhi zake huku akijidai kuwa yeye ni Mwislamu, bila shaka ni mwongo aliyedanganywa na shetani akampambia amali zake mbovu hizo azione nzuri.
Lau kama moyo wake ungetengenea kwa Imani kikweli, basi kiwiliwili chake chote kingetengenea na kutekeleza faradhi zake.
 Mtume (SAW) amesema:-
<<Hakika katika mwili kuna kipande cha nyama, kikitengenea hutengenea mwili wote na kinapoharibika huharibika mwili wote, kwa hakika (eleweni kuwa) kipande chenyewe ni Moyo>>.
(Bukhari na Muslim)

4)-  KUTIMIZA YALIYOWAJIBISHWA NA KUYAACHA YALIYO HARAMISHWA.

Imani ya mtu haiwi kamilifu bila kutimiza yale aliyowajibishiwa na MwenyeziMungu na kuyaacha yale aliyoharamishiwa, kama alivyotufundisha Mtume wa MwenyeziMungu (SAW).
Mwenyezi Mungu anasema;
“Na anachokupeni  Mtume basi pokeeni na anachokukatazeni jiepusheni nacho. Na muogopeni MwenyeziMungu. Kwa yakini MwenyeziMungu ni mkali wa kuadhibu”.
(Al - Hashr - 7)

5-  TOBA NA KUOMBA MAGHUFIRA:

Mwislamu anapotelezeshwa na shetani akatenda katika yale yaliyoyaharamisha na MwenyeziMungu, hufanya haraka sana kutubu na kujuta juu ya yale aliyoyapunguza katika haki ya MwenyeziMungu, na wala haendelei kumuasi Mola wake, bali huomba maghufira kutoka Kwake.
MwenyeziMungu anasema akitoa wasfu wa waja wake walioamini:-
“Na ambao wanapofanya uchafu (kufanya dhambi kubwa) au kudhulumu nafsi zao (kwa dhambi ndogo ndogo) humkumbuka MwenyeziMungu na kuomba msamaha kwa dhambi zao. Na ni nani anyeghufuria dhambi isipokuwa MwenyeziMungu? Na hawaendelei na (maovu) waliyoyafanya hali wanajua (kuwa hayo ni maovu).”
(Aal - Imran - 53)
Na akasema:-
"Sema "Enyi waja wangu mliojidhulumu nafsi zenu! Msikate tamaa na rehema za MwenyeziMungu; bila shaka MwenyeziMungu husamehe dhambi zote; hakika Yeye ni Mwingi wa kurehemu".
(Az - Zummar - 53)

 KUAMRISHA MEMA NA KUKATAZA MABAYA.

Kuamrisha mema na kukataza mabaya ni katika dalili za ukamilifu wa Imani na ni moja katika sifa za Mwislamu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na wanaoamini wanaume na wanaoamini wanawake, ni marafiki wao kwa wao. Huyaamrisha yaliyo mema na kuyakataza yaliyo mabaya”.
(At - Tawba - 71).
Uhusiano uliopo baina ya nguvu ya Imani katika moyo wa Mwislamu na katika kuifanya kazi ya kukataza mabaya na kuamrisha mema, ni uhusiano ulio thabiti (Madhubuti)


Mtume SAW) amesema:-
<<Atakayeona miongoni mwenu jambo baya basi alizuie kwa mkono wake, asipoweza basi kwa ulimi wake, asipoweza basi kwa moyo wake na huo ni udhaifu wa imani >>.
Na katika hadithi nyengine:
<<Hapana katika kufanya hivyo (katika kuzuwia mabaya kwa moyo) Imani hata iliyo na ukubwa wa chembe  ya hardali >>.
(Imetolewa na Muslim , Abu Daud, Al Tirmidhy na Ibn Majah Na imepokewa kutoka kwa Abu Saeed Al Khudry).
Mwislamu asiiache kazi hii ya kuamrisha mema na kukataza mabaya, kwa sababu anapoiacha,  matokeo  yake ni kula hasara na kwenda mbali na  njia ya Waislamu wa kweli.
MwenyeziMungu anasema:-
"Naapa kwa zama (zako ewe nabii Muhammad ).
Kuwa binaadamu yuko katika hasara.
Isipokuwa wale walioamini na wakafanya mema.Wakausiana (kufuata) haki na wakausiana (kushikamana) na subira (kustahamiliana)".
(Asri - 1-3)

 KULINGANIA WATU KATIKA DINI YA MWENYEZMUNGU NA KUWAPIGA VITA WANAOZUIA WATU KATIKA NJIA YA MWENYEZIMUNGU

Mja akeshaonja utamu wa Imani, na mapenzi ya Mwenyezi Mungu yakaingia moyoni mwake, hufanya jitihada kubwa ili ajiepushe yeye, jamii yake, pamoja na watu wote kutokana na kiza cha kufru, kutoamini Mungu na kughafilika, na atafanya jitihada apate kuwaingiza watu katika Nuru ya Imani na Qurani na uongofu.
Huwalingania watu katika dini ya MwenyeziMungu huku akistahamili udhia wao, akitegemea ujira na thawabu kutoka kwa MwenyeziMungu aliyetukuka.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na ni nani  asemaye kauli zaidi kuliko aitaye (viumbe) kwa MwenyeziMungu na (mwenyewe) akafanya vitendo vizuri na kusema "Hakika mimi ni miongoni mwa Waislamu".
Haam - mym Sajdah (fusilat - 33)
Na akasema:-
"Sema hii ndio njia yangu; ninaita (ninalingania) kwa Mwenyezi Mungu kwa ujuzi wa kweli; mimi (nafanya hivi) na (kila) wanaonifuata. Na Mwenyezi Mungu ametakasika na kila upungufu; wala mimi simo miongoni mwa wanaomshirikisha (Mwenyezi Mungu)".
Yusuf _108
Na Mtume (SAW) amesema:
<<Atakayewalingania watu katika uongofu, atapata ujira wake sawa na watakaomfuata bila ya kupunguziwa kitu katika ujira wao>>.
Imetolewa na Muslim na wengineo na Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurairah (RA)

Ama kwa wale wanaozuwia watu katika njia ya Mwenyezi Mungu na wakasimama imara kuwazuwia wasiingie katika dini ya Mwenyezi Mungu, basi Waislamu wamefaridhishiwa kupigana nao Jihadi mpaka dini ya Mwenyezi Mungu iweze kuwafikia watu wote ili  aamini atakayeamini baada ya kubainishiwa na aangamie atakayeangamia baada ya kubainishiwa.

Mwenyezi Mungu anasema:
"Enyi mlioamini Je! Nikujulisheni biashara itakayokuokoeni na adhabu iumizayo? (Basi biashara hiyo ni hii) Muaminini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na piganieni dini ya Mwenyezi Mungu kwa mali zenu na nafsi zenu, haya ni bora kwenu; ikiwa mnajua (kuwa ni bora basi fanyeni). (Mkifanya haya):-  Atakusameheni dhambi zenu na atakuingizeni katika Mabustani yapitayo mito mbele yake na (atakupeni) maskani mazuri mazuri katika Bustani za milele; huku ndiko kufuzu kukubwa. Na (atakupeni) kingine mnachokipenda; nayo ni Nusura itokayo kwa Mwenyezi Mungu na ushindi ulio karibu. Na wapashe habari njema Waislamu".
Al Anfal - 39

8-  KUWAPENDA (KUWANUSURU) WAISLAMU NA KUJITENGA NA MAKAFIRI

   Kunusuru (wilaa) ni kupenda, kusahibiana na kusaidiana baina ya Waislamu. Na katika masharti ya Imani ni kwa Mwislamu kuwanusuru Waislamu wenzake.
Mwislamu hatakiwi kukipa utiifu wake kwa kukinusuru kisichokuwa na msingi wa Imani ya Kiislamu.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Rafiki yenu khasa (wa kumsafishia nia) ni Mwenyezi Mungu na Mtume wake na walioamini ambao husimamisha Sala na hutoa Zaka, na hali ya kuwa wananyenyekea. Na atakayefanya urafiki na Mwenyezi Mungu na Mtume wake na walioamini (atafuzu) kwani (watu wa) kundi la Mwenyezi Mungu ndio watakaoshinda".
Al Maidah - 55-56
Na akasema:
"Na wanaoamini wanaume na wanoamini wanawake, ni marafiki wao kwa wao. Huyaamrisha yaliyo mema na kuyakataza yaliyo mabaya, na husimamisha Sala na hutoa Zaka na humtii Mwenyezi Mungu na Mtume. Hao ndio ambao Mwenyezi Mungu atawarehemu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye Nguvu na Mwenye Hikima".
At Tawba - 71

Mwenyezi amewapa Waislamu mfano bora katika kujitenga na makafiri.
Mwenyezi Mungu anasema;
"Hakika nyinyi mnao mfano mzuri kwa (Nabii) Ibrahimu na wale waliokuwa pamoja naye, walipowaambia jamaa zao (makafiri); "Kwa yakini sisi tu mbali nanyi, na mbali na hayo mnayoyaabudu kinyume cha Mwenyezi Mungu, tunakukataeni umekwisha dhihiri uadui na bughudha ya daima baina yetu na nyinyi mpaka mtakapomwamini Mwenyezi Mungu peke yake".
Mumtahinah – 4

MATENDO YANAYOIHARIBU IMANI - KWANZA - KUFRU NA AINA ZAKE

a-  KUFRU YA KUKADHIBISHA

Nako ni kukadhibisha chochote katika aliyokuja nayo Mtume (SAW).
Mwenyezi Mungu anasema:
"Na kama wanakukadhibisha, basi walikwisha kadhibisha wale wa kabla yao. Mitume wao waliwajia kwa dalili wazi wazi na kwa madaftari na kwa vitabu vyenye nuru (wakakadhibisha). Kisha niliwakamata (niliwatia mkononi) wale waliokufuru; basi adhabu ilikuwa (kali) namna gani".
Fatir - 25-26

b-  KUFURU YA KUTOTII NA KUTAKABARI

Mfano wake ni mfano wa kufru ya Ibilisi, maana yeye hajaikanusha amri ya Mwenyezi Mungu pale alipotakiwa asujudu wala hakuikataa, (alikuwa akijua kuwa aliyetoa amri hiyo ni Mwenyezi Mungu), lakini aliikabili amri hiyo kwa kutokutii na kwa kutakabari. Yeye ni mfano wa yule ajuwae kwamba dini ya Kiislamu ni dini ya haki itakayomfaa hapa duniani na akhera, lakini akaiacha na kufuata dini au madhehebu yaliotungwa na mwanadamu.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Na (wakumbushe watu habari hii) Tulipowaambia Malaika: "Msujudieni Adam", wakamsujudia wote isipokuwa Iblisi akakataa na akajivuna; na (tokea hapo) alikuwa katika makafiri".
Al Baqarah - 35

c-  KUFRU YA KUKATAA KUFUATA

Nako ni kukataa kuyafuata yale aliyokuja nayo Mtume (SAW), hata kama hakuyakubali wala hakuyakanusha, isipokuwa awe amekataa tu kuyafuata.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Na ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule anayekumbushwa aya za Mola wake akazikataa? Hakika sisi ni wenye kuchukua kisasi kwa wale wabaya".
Sajda _22

d- KUFRU YA KUTIA SHAKA

Nako ni kutia shaka katika yale alokuja nayo Mtume wa Mwenyezi Mungu (SAW) hata bila kutoa uamuzi wa kusadikisha wala kukadhibisha.
Mwenyezi Mungu anasema;
"Na wakasema 'Hakika sisi tunakataa mliyotumwa nayo na hakika sisi tunayo shaka ituhangaishayo kwa hayo mnayotuita' (Ya kumwabudu Mungu mmoja)".
Ibrahim _9

e-  KUFRU YA KUKANUSHA

Yote sawa ikiwa kukanusha mengi katika aliyoteremsha Mwenyezi Mungu au kukanusha jambo moja tu katika yale yajulikanayo kuwa ni ya lazima kuyaamini katika Uislamu.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Na wakazikanusha, na hali ya kuwa nafsi zao zina yakini nazo; kwa dhuluma na kujivuna. Basi angalia ulikuwaje mwisho wa wafanyao ufisadi".
An Naml -14
Na akasema:
"Tunajuwa ya kwamba yanakuhuzunisha yale wanayoyasema (katika kukutukana na kukukadhibisha). Basi wao hawakukadhibishi wewe lakini madhalimu hao wanakanusha hoja za Mwenyezi Mungu (Mungu atawalipa)".
Al An Aam  - 33

PILI -  SHIRKI NA AINA ZAKE

Mwenyezi Mungu anasema:
“Na kwa yakini yamefunuliwa kwako na kwa wale waliokuwa kabla yako (maneno haya); ‘Kama ukimshirikisha (Mwenyezi Mungu) bila shaka amali zako zitaruka patupu, (hutazipatia thawabu japo ni amali njema); na lazima utakuwa miongoni mwa wenye hasara”.
Azumar – 65
Na akasema;
"Hakika Yeye hasamehe kushirikishwa; na husamehe yasiyokuwa haya kwa amtakaye na anayemshirikisha Mwenyezi Mungu bila shaka amebuni dhambi kubwa".
An Nisaa - 48
Shirki haikubaliani na Imani, nayo ipo aina nyingi:

a-  SHIRKI YA ANAYEMWAMINI MWENYEZI MUNGU LAKINI ANAMSHIRIKISHA NA MWENGINE KATIKA UFALME, KATIKA UWEZO WA KUFANYA ALITAKALO JUU YA VIUMBE, KATIKA KUUMBA, KUTOA MAISHA, RIZIKI, MAUTI, MADHARA NA MANUFAA

Shirki hii ni sawa na ile ya Manasara (Wakristo) na  Wamajusi, maana Manasara wanaamini kwamba Mwenyezi Mungu amegawika sehemu tatu- Mwenyezi Mungu ametakasika na kuepukana na hayo wayasemayo uepukano mkubwa kabisa - na Wamajusi wanaamini kwamba Yeye ni wawili - Mwenyezi Mungu ametakasika na hayo wayasemayo.
Mwenyezi Mungu aliyetakasika anasema:
"(Mwenyezi Mungu) ambaye ni wake (peke yake) ufalme wa mbingu na ardhi, wala hakuzaa mtoto wala hana mshirika katika ufalme (Wake) na ameumba kila kitu na akakikadiria kipimo (chake)".
Al Furqan- 2

b-  SHIRKI YA MTU KUJISIFIA MWENYEWE AU KUMSIFIA MTU MWENGINE KWA SIFA ZA UKAMILIFU

Hizi ni sifa ambazo hana mwengine isipokuwa Mwenyezi Mungu peke Yake. Mfano wake ni mfano wa kauli ya Firauni aliposema:
"Mimi ndie Mola wenu mkuu (huyo Mola wa Nabii Musa ni mdogo)".
An Naziat -24
Au kwa yule anayekanusha moja wapo ya sifa za ukamilifu wa Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, mfano wa kauli ya Firauni:
"Na nani huyo Mola wa ulimwengu".
Ash Shuaraa -23
 Au kauli ya makafiri wa Kiquraishi kama alivyosema Mwenyezi Mungu:
"Na wanapoambiwa 'Msujudieni Rahmani’; husema: ‘Ni nani Rahmani? Je! Tumsujudie unayetuamrisha wewe tu? 'Na maneno namna hii yanawazidisha chuki".
Al Furqan - 60



Na akasema:
"Na wao wanamkufuru (Mwenyezi Mungu) Rahmani.Sema: 'Yeye ndiye Mola wangu, hakuna aabudiwaye (kwa haki) ila Yeye; nimemtegemea Yeye na marejeo yangu ni kwake”.
Ar Raad - 31

c-  SHIRKI YA KUMUABUDU ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU KWA NAMNA YO YOTE YA IBADA

Mwenyezi Mungu anasema:
"Mwabuduni Mwenyezi Mungu wala msimshirikishe na cho chote".
An Nisaa - 36
Na akasema:
"Sema: 'Je! Mnaniamrisha niabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu enyi wajinga!".
Az Zumar - 64
Na akasema:
"Kwa yakini yamefunuliwa kwako na kwa wale waliokuwa kabla yako (maneno haya): 'Kama ukimshirikisha (Mwenyezi Mungu) bila shaka amali zako zitaruka patupu (hutazipatia thawabu japo ni amali njema) Na lazima utakuwa miongoni mwa wenye hasara. Bali mwabudu Mwenyezi Mungu tu na uwe miongoni mwa wenye kushukuru".
Az Zumar - 65-66

TATU - KUTOKA KATIKA DINI -"KUR-TADI"

MwenyeziMungu anasema:-
"Wala hawataacha kupigana nanyi, mpaka wakutoeni katika dini yenu, kama wakiweza. Na watakaotoka dini yao katika nyinyi, kisha wakafa hali ya kuwa makafiri, basi hao ndio ambao amali zao zimeharibika katika dunia na akhera. Nao ndio watu wa Motoni. Humo watakaa milele."
(Al - Baqarah  -217).

Na "Murtadi" ni yule aliyeiacha dini ya Kiislamu akiwa na akili timamu, amejiamulia mwenyewe bila kulazimishwa na mtu kuingia katika dini nyingine kama vile Ukristo  au dini ya Kiyahudi au kutokuwa na dini kama vile Ukoministi au hata akakanusha jambo lolote lile lijulikanalo kama ni la lazima katika dini kama vile kuwajibika Kusali, Kutoa zaka au akafanya jambo dhidi ya Uislamu au dhidi ya sheria zake zilizo dhahiri au akatamka kauli ambayo haina tafsiri nyengine isipokuwa kukufuru.

NAMNA GANI HUPATIKANA KUR-TADDI (KUTOKA KATIKA DINI)


A - KUR-TADDI KWA ITIKADI NAYO NI KAMA IFUATAVYO:-

1-  Maulamaa wote wa Kiislamu wamekubaliana kwamba yeyote anayemshirikisha MwenyeziMungu au kumpinga au akakanusha moja wapo ya sifa zilizothibitika katika sifa Zake ikijulikana wazi kuwa mtu huyo lazima anazielewa vizuri sifa hizo, au amsingizie Mwenyezi Mungu jambo ambalo Yeye mwenyewe amelikanusha, mfano; kuwa na mtoto, au kukanusha kuwepo kwa Malaika au vitabu au Mitume au kuikanusha Siku ya Kiama au Qadari kheri yake na shari yake au akatae jambo lolote lijulikanalo kwamba ni la lazima katika dini,  basi mtu huyu huwa ni Murtadi, kafiri (ametoka katika dini).

2-  Inajulikana kwamba anahesabika kuwa Murtadi, Muislamu yeyote anayeipinga au kuikanusha Qurani yote, au sehemu yoyote ya Qurani au hata aya moja katika aya za Qurani. Huhesabiwa kuwa amertadi pia, yule mwenye itikadi kwamba Qurani inakhitalifiana yenyewe kwa yenyewe au ina khitilafu ndani yake au kuwa na shaka katika miujiza yake au kujigamba kuwa ana uwezo wa kuleta mfano wake, na pia mwenye kuivunjia heshima yake(Qurani), au kuongeza au kupunguza ndani yake.

3-  Anahesabiwa kuwa kafiri Aliyertadi, mwenye kuitakidi kwamba Mtume (SAW) amesema uwongo katika baadhi ya aliyokuja nayo, na pia yule anayeitakidi kuwa ni halali jambo lolote liloharamishwa kama vile kuzini kunywa pombe n.k.

B-  KURTADI KWA MATAMSHI, KAMA IFUATAVYO:

1-  Anayeapa kwa mila nyengine isiyokuwa ya Kiislam.
 Ameelezea Thabit bin Dha-Haak kwamba Mtume (SAW) amesema:-
"Atakaekula kiapo kwa mila isiyokuwa ya Kiislamu (kwa mfano akadai kwamba yeye ni mkristo ilihali uwongo) basi anakuwa kama alivyosema".
(Mfano wake ni baadhi ya watu wanaopenda kuwaiga wazungu katika kula kiapo kwa kusema; ‘Yesu kristo’ au kwa lugha yoyote ile, viapo vya aina hiyo).
(Imetolewa na wote isipokuwa Abu Daud).
Na kutoka kwa Buraida(RA), ameeleza kuwa Mtume (SAW) amesema:-
"Atakayesema; ‘Mimi  si Muislam’, ikiwa anasema uwongo basi kama alivyosema na ikiwa anasema kweli basi hatorudi katika Uislamu akiwa amesalimika".
(Abu Daud , Annasai na Ibn Majah ).

2-  Atakae mtukana Mwenyezi Mungu au akaitukana Qurani au akamtukana Mtume (SAW) au moja wapo wa Mitume ya Mwenyezi Mungu, basi anakuwa amekufuru japo kuwa amesema kwa mzaha au kweli au kwa istihizai.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na kama ukiwauliza (kwa nini wanaifanyia mzaha dini)? Wanasema; "Sisi tulikuwa tukizungumza zungumza na kucheza tu."  Sema; "Mlikuwa mkimfanyia mzaha MwenyeziMungu na Aya zake na Mtume wake?
"Msitoe udhuru (wa uwongo) umekwisha kudhihiri ukafiri wenu (mlokuwa mkiuficha) baada ya kule kuamini kwenu (kwa uwongo)."
(At - Tawba - 65 - 66)

3-  Maulamaa wote wamekubaliana kuwa kila atakaemsingizia uwongo bibi Aisha (RA) katika kile kisa cha uwongo alichozuliwa (hadithi ya "Al-Ifki") wakati MwenyeziMungu kishamtakasa basi anakuwa si Muislamu tena.
MwenyeziMungu anasema:-
"Hakika wale walioleta uwongo huo (wa kumsingizia bibi Aisha(RA) mkewe Mtume(SAW) kuwa amezini)) Ni kundi miongoni mwenu (ni jamaa zenu) msifikiri ni shari kwenu bali hiyo ni kheri kwenu. Kila mtu katika wao atapata aloyachuma katika madhambi yao na yule aliyejitwika sehemu yake kubwa miongoni mwao atapata adhabu kubwa (zaidi).
Kwa nini mlipo sikia khabari hii, wanaume Waumini na wanawake Waumini hawakuwadhania wenzao mema, na kusema: Huu ni uzushi dhaahiri?
Kwa nini hawakuleta mashahidi wane? Na ilivyo kuwa hawakuleta mashahidi wane basi hao mbele ya Mwenyezi Mungu ni waongo.
Na lau kuwa si fadhila ya Mwenyezi Mungu juu yenu na rehema yake katika dunia na
Akhera, bila ya shaka ingeli kupateni adhabu kubwa kwa sababu ya yale mliyo jiingiza.
Mlipoupokea (uwongo huo mkawa mnautangaza) kwa ndimi zenu na mkasema kwa vinywa vyenu msiyo yajua, na mlifikiri ni jambo dogo, kumbe mbele ya Mwenyezi Mungu ni kubwa.
Na kwa nini mlipo yasikia msiseme: Haitufalii kuzungumza haya. Subhaanaka (Mola wetu) Umetakasika! Huu ni uzushi mkubwa!?
Mwenyezi Mungu anakuonyeni msirudi kabisa (msirejee tena) kufanya kama haya, ikiwa nyinyi ni Waumini! (Waislamu) kweli.”
An Nur– 11-17
Kwa hivyo atakaerudia kueneza uwongo huo hatakuwa Muislamu tena.

4-  KUITUKANA DINI

Yeyote atakayeituhumu, kuishambulia au kuitukana dini ya MwenyeziMungu au kuwataka watu wafuatae siasa ya kutoamini Mungu au kuwataka wakufuru basi anakuwa Murtadi.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na kama wakivunja viapo vyao baada ya kuahidi kwao na wakatukana dini yenu, basi wapigeni vita viongozi wa ukafiri. Hakika viapo vyao havina maana wauweni (piganeni nao) ili wapate kujizuia (na kufanya ubaya wao).”
(At - Tawba -12)

"KUR-TADI" KWA VITENDO, NAYO NI KAMA IFUATAVYO:

1-  Maulamaa wa Kiislamu wote wamekubaliana kuwa amefanya kitendo cha kurtaddi Muislamu yeyote atakayeutupa msahafu mahala panapotupwa taka, au kuuchafua (kwa kukusudia) kwa kuumwagia taka, na pia kuvifanyia hivyo hivyo vitabu vya hadithi za Al Qudusiy au vya hadithi za Mtume (SAW) na pia atakayeufanyia dharau msahafu.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na kama ukiwauliza (kwa nini?) Wanasema; "Sisi tulikuwa tukizungumza zungumza na kucheza tu, Sema; "Mlikuwa mkimfanyia mzaha MwenyeziMungu na aya zake na Mtume wake?".
(At - Tawba -65)

2-     Wamekubaliana Maulamaa kwamba Mwislamu yeyote akilisujudia sanamu, juwa au mwezi au akasema neno au kufanya kitendo kinachoonesha wazi kuwa kaifanyia istihizai dini, basi anakuwa ametoka katika dini ‘Amertadi’.

3-  Mwislamu yeyote atakayekimbilia nchi ya makafiri wanaowapiga vita Waislamu na akaungana nao katika kupigana vita hivyo dhidi ya Waislamu, basi kesha kuwa kafiri, na hii ni kutokana na kauli ya MwenyeziMungu isemayo:
"Na miongoni mwenu atakayefanya urafiki huo nao,  basi huyo atakuwa pamoja nao. Hakika MwenyeziMungu hawaongozi (njia ya kheri  watu madhalimu)."
(Al - Maidah -51).
Mtume(SAW) pia amekataza kufanya hivyo na akajiweka mbali na aina hiyo ya watu.

4-  Mwislam yeyote atakayeipiga vita sheria ya Kiislamu na akaibadilisha kwa kanuni za wanadamu kwa nia ya kuizuia sheria ya Kiislamu isitumike, basi amekuwa kafiri.
MwenyeziMungu anasema:-
"Na wasiohukumu kwa yale aliyoyateremsha MwenyeziMungu basi hao ndio  makafiri".
(Al - Maidah - 44)

NNE-  UNAFIKI

Unafiki ni mtu kujidhihirisha mbele ya Waislamu kuwa na Imani kama yao, na kujifanya kama mwenzao, wakati moyoni mwake ni kafiri anayeukadhibisha Uislam.
Katika itikadi ya Kiisilamu, Unafiki ni kufru, isipokuwa mnafiki hatendewi kama anavyotendewa kafiri kwa sababu ya kutoudhihirisha ukafiri wake.
MwenyeziMungu anasema:
“Wanapokujia wanafiki, husema; "Tumeshuhudia kwa yakini wewe ni Mtume wa MwenyeziMungu". Na MwenyeziMungu anajua kuwa wewe ni Mtume wake na MwenyeziMungu anashuhudia ya kuwa hakika wanafiki ni waongo. (wanasema wasiyoyasadiki)."
Al - Munafiqoun - 1
Na anasema:
“Na hayo ni kwa kuwa waliamini kisha wakakufuru; kwa hivyo muhuri umepigwa juu ya nyoyo zao; kwa hivyo hawafahamu lolote".
Al - Munafiqoun - 3
Na upo Unafiki wa Vitendo ulio tofauti na ule wa Unafiki wa Imani, kwa mfano;
Kufanya khiyana katika amana, kusema uongo au kutotekeleza ahadi (kuvunja ahadi).
Huyu mnafiki wa vitendo hahisabiwi kuwa ni kafiri, lakini huhisabiwa kuwa ni "fasiki” mtenda maasi na anayo sehemu ya unafiki moyoni mwake.

SIFA ZA WANAFIKI

Miongoni mwa sifa maarufu za wanafiki ni hizi zifuatazo:

A-  KUFANYA UFISADI ULIMWENGUNI KWA KUIPIGA VITA SHERIA YA MWENYEZIMUNGU NA KUWATUHUMU WAISLAMU KUWA NI WAPUMBAVU

 MwenyeziMungu akiuelezea wasfu wa wanafiki wa aina hii anasema:
“Na wanapoambiwa "Msifanye uharibifu ulimwenguni”, Husema; "Sisi ni watengenezaji”. Hakika wao ndio waharibifu, lakini hawatambui, na wanapoambiwa;  "Aminini kama walivyoamini watu", Husema; "Oh! tuamini kama walivyoamini wapumbavu?" Hakika wao ndio wapumbavu lakini hawajui."
Al Baqarah 11-13

B-  KUWAFANYIA HADAA WAISLAMU KWA KUJIONESHA MBELE YAO KUWA WAO NI WAISLAMU KISHA KUUDHHIRISHA UKAFIRI WAO MBELE YA MABWANA ZAO

MwenyeziMungu anasema:
“Na wanapokutana na walioamini husema; "Tumeamini", na wanapokuwa peke yao kwa mashetani wao husema; "Hakika tu pamoja nanyi, tunawacheza shere tu".
Al - Baqarah – 14

KUPINGA KUHUKUMU KWA SHERIA YA MWENYEZIMUNGU NA KUWAZUIA WATU WASIZITUMIE SHERIA ALOZITEREMSHA MWENYEZI MUNGU

MwenyeziMungu anasema:
“Huwaoni wale wanaodai kwamba wameamini yale yaliyoteremshwa kwako na yaliyoteremshwa kabla yako? Nao wanataka wakahukumiwe kwa njia isiyowafiki sheria; na hali wameamrishwa kukataa  njia hiyo. Na shetani anataka kuwapoteza upotofu (upotevu) ulio mbali (na haki). Na  wanapoambiwa; "Njooni katika yale aliyoyateremsha MwenyeziMungu na (njooni) kwa Mtume", utawaona wanafiki wanajiweka mbali nawe kabisa".
An - Nisaa -60 - 61


D-  KUAMRISHA MAOVU NA KUKATAZA MEMA

MwenyeziMungu anasema:
“Wanaume wanafiki na wanawake wanafiki wote ni hali moja, huamrisha yaliyo mabaya na kukataza yaliyo mazuri  na kuizuilia mikono yao (hawasaidii mambo ya kheri). Wamemsahau MwenyeziMungu (wamepuuza amri zake) na Yeye pia amewasahau (amewapuuza). Hakika wanafiki ndio wavunjao amri".
At - Tawba -67

E-  KUWAFANYA MAKAFIRI KUWA MARAFIKI BADALA YA WAISLAMU

MwenyeziMungu anasema :
“Waambie wanafiki kwamba watapata adhabu inayo umiza, (wanafiki) ambao huwafanya makafiri kuwa marafiki badala ya Waislamu,.. Jee! wanataka wapate utukufu kwao? Basi utukufu wote ni wa MweyeziMungu.(hauko katika mkono wa mtu)."
An - Nisaa -138 - 139

F-  KUWAFANYIA UADUI WAISLAMU KWA AJILI YA IMANI YAO NA KUFANYA URAFIKI NA MAKAFIRI KWA UKAFIRI WAO

Anayefanya urafiki na makafiri akawapenda na kuzitetea itikadi zao za kikafiri, huyo atakuwa amekwishaiharibu imani yake:
MwenyeziMungu anasema:
“Huwapati (huwaoni) watu wanaoamini MwenyeziMungu na Siku ya mwisho, kuwa wanawapenda wale wanaompinga  MwenyeziMungu na Mtume wake; hata wakawa ni baba zao au watoto wao au ndugu zao au jamaa zao."
Al - Mujadilah - 22
Anayewafanyia uadui Waislamu kwa kuwapiga vita, kuwachukia na akawanusuru maadui wao dhidi yao kwa ajili ya imani yao, basi amekwishavunja imani yake.
MwenyeziMungu anasema:
“Nao hawajaona baya lolote kwa (Waislamu) ila kumuamini MwenyeziMungu Mwenye kushinda (na) Mwenye kusifiwa.
Ambaye ni Mwenye Ufalme wa mbingu na ardhi, na MwenyeziMungu ni Mwenye kuona kila kitu.
Hakika wale waliowaadhibu Waislamu wanaume na Waislamu wanawake, kisha wasitubie basi watapata adhabu ya Jahannam na watapata adhabu ya kuungua (barabara)".
Al - Buruj - 8 – 10

Wanafiki hawa Siku ya kiama watakuja kujuta kwa sababu ya dharau yao na stihizai zao juu ya Waislamu.
MwenyeziMungu anasema:
“Bila shaka kulikuwa na kundi katika waja wangu likisema; "Mola wetu! Tumeamini, basi tusamehe na turehemu, nawe ndiwe Mbora wa wanaorehemu.”
Lakini nyinyi mliwafanyia stihizai hata wakakusahaulisheni kunikumbuka, na mlikuwa mkiwacheka.
Hakika leo ninawalipa (Pepo) kwa sababu ya kusubiri kwao bila shaka hao ndio wenye kufuzu.”
Al - Muuminun - 110 – 112


UJINGA WENYE HATARI

WAISLAMU LAKINI WAJINGA

Ujinga wa kutoijua dini ya MwenyeziMungu umeenea sana katika nchi za Kiislamu, hata anapatikana Mwislamu mwenye Kuishahidia shahada ya; Laa Ilaha illa Llah, Muhammad Rasulu Llah’, akasimamisha Sala na kutoa Zaka na kufunga mwezi wa Ramadhani, aka Hiji Maka na akaamini yote yaliyomo ndani ya Qurani na akampenda Mtume (SAW) na kumsadiki na Kuionea uchungu dini ya Kiislam, lakini juu ya yote hayo, utamuona anafanya vitendo na kusema maneno na kuwa na itikadi zinazomfanya awe katika Kufru au Shirki au Unafiki bila ya kuuelewa uhakika wake. Bali huenda akawa anadhani kuwa hali hiyo aliyokuwa nayo ya shirki au kufru au unafiki kuwa ni sawa na yenye kumridhisha Mwenyezi Mungu.
Yeye ni Mwislamu mwenye kuionea uchungu dini yake, lakini ameingia katika Kufru au Shirki kwa sababu ya ujinga wake ambao huenda ukamtia katika adhabu ya Moto.

MJINGA ANASAMEHEKA, LAKINI NI WAJIBU WAKE KUJIFUNZA NA KUIFUATA HAKI PALE ITAKAPOMBAINIKIA

Mtu akishaingia katika Uislamu na kumthibitikia Uislam, basi huendelea kuwa hivyo na hakimtowi katika Uislamu kitendo chochote isipokuwa akitenda moja wapo ya yale mambo yenye kuiondoa sifa ya Imani (yaliyokwishatajwa hapo mwanzo) tena atende jambo hilo kwa kusudi akiwa na nia ya Kurtadi. Kwa sababu Nia ni sharti muhimu ili kitendo chochote kikubaliwe na kuhesabiwa.
Kwa hivyo mtu anapotenda kitendo chochote cha shirki au cha kufru kinachomuodolea sifa za mwenye Imani, akiwa hakusudii kuibatilisha imani hiyo, basi mtu huyo anasameheka, lakini inamwajibikia kujifunza yaliyo sahihi na kutubia sana.
Wanafunzi wa Nabii Issa (AS) kutokana na ujinga wao walimuuliza Mtume wao huyo kama ilivyonukuliwa katika Qurani. Mwenyezi Mungu anasema:
"(Kumbuka) wanafunzi (wako) waliposema: "Ewe Issa mwana wa Maryam! Jee Mola wako anaweza kututeremshia chakula kutoka mbinguni?" (Nabii Issa) Akasema; "Mcheni MwenyeziMungu kama nyinyi ni wenye kuamini kweli."
(Al - Maidah - 112)
Kwa suala lao hilo, walionesha ujinga wao wa kutokujua kwamba MwenyeziMungu ni Muweza wa kila jambo, na Mwenye kukanusha uwezo wa MwenyeziMungu anakuwa kafiri, lakini kwa sababu ya ujinga wao huo, kumekuwa ni udhuru kwao mbele ya MwenyeziMungu na Mtume wake (AS).
Na Mtume (SAW) alipotoka pamoja na Sahaba zake(RA) kuelekea Khaybar, walipita mahali penye mti uliokuwa umetundikwa vitu vilivyo kama hirizi juu yake, mahala ambapo makafiri (Washirikina) walikuwa wakitundika panga zao wakati wa vita wakiwa wanaamini kwamba hirizi hizo zanawasaidia katika ushindi vitani. Baadhi ya Waislamu wakamuambia Mtume (SAW): "Tufanyie na sisi mti ulio na hirizi kama waliokuwa nao makafiri."
Mtume (SAW) akawambia:
<<Subhana Llah! Maneno haya ni kama yale waliyosema watu wa Nabii Musa:
"Tufanyie Mungu na sisi (yaani masanamu) kama wao walivyo na miungu>>.
(Al - Aaraf - 138)
Mtume (SAW) akaendelea kusema:
<<Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko mikononi mwake, mtakuja fuata mwenendo wa waliokuja kabla yenu.(Manasara na Mayahudi).>>
Imam Ahmed na Attirmidhy

Waliouliza masuala haya mawili kwa Musa na Muhammad (AS) kwa ujinga wao walifanya makosa yanayoingiza katika shiriki, lakini jawabu ya Mtume (SAW) lilikuwa;
"Mtakuja fuata mwenendo wa waliokuja kabla yenu"
Na jawabu ya Musa (AS) lilikuwa:-
"Hakika nyinyi ni watu mfanyao ujinga."
(Al - Aaraf - 138)

Hakusema yeyote kati ya Isa au Musa au Muhammad (Alayhimu Ssalaatu Wassalaam) kuwaambia watu wao hao waliokufuru kwa ujinga wao  pamoja na kumshirikisha kwao MwenyeziMungu (bila kukusudia), kuwa wao ni Makafiri au Washirikina.
MwenyeziMungu anasema:
"Wala si lawama juu yenu mkikosa, lakini (kuna lawama) katika yale ziliyoyafanya nyoyo zenu kwa kusudi, na MwenyeziMungu ni Mwingi wa kusamehe (na) Mwingi wa Kurehemu ."
Al - Ahzab – 5

HAPANA UDHURU KWA YEYOTE YULE BAADA YA KUELIMIKA

Ikiwa mambo yamekuwa ni ya hatari kiasi hiki, basi inawapasa Maulamaa kuwabainishia watu dini ya MwenyeziMungu na inampasa kila aliyefanya makosa katika Kukufuru au kufanya kitendo cha Ushirikina bila ya kujua, afanye juhudi ya kutubia.
MwenyeziMungu akitujulisha juu ya Maulamaa wanaoficha (mafundisho ya) dini ya MwenyeziMungu anasema:-
"Hakika wale wanaoficha tuliyoyateremsha - nazo ni hoja zetu zillizo wazi na uwongozi, baada ya sisi kuzibainisha kwa watu kitabuni - hao anawalani MwenyeziMungu, na anawalani (kila)  mwenye kulani.
Ila wale waliotubu na kutengeneza na kubainisha (yale waliokuwa wakiyaficha), basi hao nitawapokea, na mimi ni Mwenye kupokea toba na Mwenye rehema".
(Al - Baqarah - 159)
Kisha Mwenyezi Mungu akasema juu ya wale wanaoshikilia kwenda kinyume na dini ya Mwenyezi Mungu pamoja na kwenda kinyume na mafundisho ya Mtume wake(SAW), wakishikilia kufuata njia isiyokuwa ya Kiislamu hata baada ya kuwafikia uongofu:
"Na atakayemuasi Mtume baada ya kumdhihirikia uongofu na akafuata njia isiyokuwa ya Waislamu, tutamgeuza alikogeukia mwenyewe na tutamuingiza katika Jahannam; napo ni pahali pabaya kabisa kwa mtu kurudia".
An Nisaa - 115

AINA MBALI MBALI ZA SHIRKI

KUMSHIRIKISHA MWENYEZI MUNGU KATIKA KUZIENDESHA HALI ZA VIUMBE

Kila anayeamini kwamba yupo mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu mwenye uwezo wa kubadilisha hali yoyote ile katika dunia hii na kwamba ana uwezo wa kudhuru au kunufaisha kwa njia za ghaibu na sio kwa njia za kikawaida alizowakadiria Mwenyezi Mungu viumbe vyake. Kwa mfano akaamini kwamba mtu katika walio hai au waliokufa anao uwezo wa kumjaalia akapata watoto au anaweza kujibu dua ya mwenye dhiki au kuleta mvua au kuzilinda nyumba au wanyama au watoto au Bwana na Bibi arusi kwa nguvu zilizojificha zenye uwezo wa kudhuru, basi anakuwa amekwisha fanya kitendo cha Shirki.
Mwenyezi Mungu amesema akijielezea Mwenyewe:
"Ufalme wa mbingu na ardhi ni wa Mwenyezi Mungu, Anaumba Apendavyo, Anampa Amtakaye watoto wa kike na Anampa Amtakaye watoto wa kiume. Au huwachanganya (watoto) wa kiume na wa kike (kwa mtu mmoja), na Humfanya tasa Amtakaye; hakika Yeye ni Mjuzi, Muweza".
Ash - Shura -49-50
Na ana‎‎‎sema:
"Au Yule anayemjibu anayedhikika amwombapo na kuondoa dhiki (yake) na kukufanyeni wenye kuendesha dunia (siye bora?) Je, yuko Mungu pamoja na Mwenyezi Mungu? Ni kuchache kuwaidhika kwenu".
An Naml - 17
Na anasema:
"Na kama Mwenyezi Mungu akikugusisha madhara (taabu) basi hakuna ye yote awezaye kuyaondoa ila Yeye; na kama akikugusisha kheri (hakuna wa kuweza kuiondoa ila Yeye tu peke yake).Yeye ndiye Mwenye Uweza juu ya kila kitu".
Al An Am - 17          
Na pia Mwenyezi Mungu anasema:
"Sema 'Mwaonaje, kama maji yenu yakiwa yamezama, (yamedidimia chini) basi nani atakuleteeni maji (safi) yatiririkayo? (Ni Yeye tu Mwenyezi Mungu; basi muabuduni Yeye tu)".
Al Mulk - 30
Na pia anasema:
"Anauwingiza usiku katika mchana na kuuingiza mchana katika usiku, na amevitiisha jua na mwezi vyote (vinakwenda mchana na usiku) mpaka muda maalum ufike.Huyo ndiye Mwenyezi Mungu, Mola wenu, Mwenye Ufalme; na wale mnaowaabudu kinyume chake, wao hawamiliki hata utando (ngozi) wa kokwa ya  tende".
Fatir – 13

AINA MBALI MBALI ZA SHIRKI KATIKA IBADA

1- KUTOA SEHEMU YA RIZIKI KWA AJILI YA MWENGINE ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU

Yule anayetoa samli au asali au chembe chembe za nafaka kwa ajili ya baadhi ya miti au mawe au makaburi, na ye yote anayetoa nyama au maziwa kwa ajili ya majini, au ye yote ambaye huchinja mwana wa mwanzo wa ng'ombe wake au mbuzi, kama ni nadhiri kwa ajili ya mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Na Yule ambaye huvunja yai au kuchinja mnyama mbele ya bwana na bibi harusi kwa ajili ya kuwaridhisha majini, au kuchinja kondoo kila mwaka au hata mara moja ili kuilinda nyumba yake au kisima chake; ye yote afanyaye hayo anakuwa amefanya kitendo cha shirki, kutokana na kauli ya Mwenyezi Mungu isemayo:
"Na neema yo yote mliyonayo basi imetoka kwa Mwenyezi Mungu. (Na nyinyi hamumshukuru). Kisha inapokuguseni dhara mara Yeye mnamlilia (mnamlalamikia).
Kisha anapokuondoleeni hiyo dhara, mara kundi moja miongoni mwenu linamshirikisha (tena) Mola wao.
Wanazikataa zile neema tulizowapa. Basi stareheni kidogo. Karibuni hivi mtajua (ubaya wenu).
Na sehemu ya vile tulivyowaruzuku, wanawawekea (waungu wao) wasiofahamu (wanayofanyiwa). Wallahi! Bila shaka nyinyi mtaulizwa juu ya yale mliyokuwa mkiyazua".
An Nahl - 53-56
Na anasema:
"Na wamemfanyia Mwenyezi Mungu sehemu katika mimea aliyoiumba (mwenyewe) na katika wanyama aliowaumba (Mwenyewe) husema 'Hii ni sehemu ya Mwenyezi Mungu' Kwa madai yao (tu) 'Na hii ni ya (wale) tunaowashirikisha na Mungu', basi vile walivyowakusudia waungu wao havifiki kwa Mwenyezi Mungu na vilivyokuwa vya Mwenyezi Mungu hivyo hufika kwa waungu wao. Ni mabaya kabisa wanayoyahukumu".
Al An am - 136
Wanaingia katika kundi hili pia wale ambao yanapon’goka meno yao hulitaka jua au (kunguru) lichukuwe jino bovu na kumpa jino zuri badala yake.

KUCHINJA KWA AJILI YA ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU

Atakayechinja katika sehemu maalum kama vile chini ya mti, sokoni, kaburini n.k. (kwa nia ya kutaka kujikurubisha na miti, masoko au maiti ‘Mawalii’) ni sawa na uchinjaji  wa wakati wa Jahilia (kabla ya kuja kwa Mtume (SAW)) maana Mushrikina walikuwa wakichinja kwa ajili ya kafara walizokuwa wakiwatolea masanamu yao.
Na atakaejikurubisha kwa kuchinja kwa ajili ya mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu basi amekwisha fanya kitendo cha shirki, kwa sababu kuchinja ni ibada.

Mwenyezi Mungu anasema:
"Hakika tumekupa kheri nyingi. Basi Sali kwa ajili ya Mola wako na uchinje (kwa ajili ya Mola wako)”.
AL Kauthar - 1-2
Na akasema:
"Sema 'Hakika Sala yangu na ibada zangu (zote nyengine) na uzima wangu na kufa kwangu (zote) ni kwa Mwenyezi Mungu. Muumba wa walimwengu. Hana mshirika wake. Na haya ndio niliyoamrishwa, na mimi ni wa kwanza wa waliojisalimisha kwa (Mwenyezi Mungu)".
Al An Am - 162-163
Imelezwa na Imam Ali ibn Abi Talib(RA), kutoka kwa Mtume (SAW) kwamba:
<<Mwenyezi Mungu amemlaani kila anayechinja kwa ajili ya mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu>>.
Katika baadhi ya nchi, watu wanaostahiki kupewa sadaka hukusanyika mwahali maalum ambapo watu huamini kuwa ni patakatifu kwa ajili ya mzimu au Walii aliyezikwa hapo n.k. Basi inapombidi mtu kuchinja na kugawa nyama katika sehemu za mikusanyiko ya watu wa aina hiyo, (badala ya kwenda penye mizimu hiyo au makaburi hayo na kuchinja katika sehemu hizo) ni bora ampeleke mnyama huyo akiwa mzima na kuwapa wale wanaostahiki ili wachinje wenyewe, na kwa njia hii huwa kuchinja huko si kwa ajili ya  ye yote isipokuwa Mwenyezi Mungu. Na kwa vyo vyote vile haijuzu kukusanyika watu katika mikusanyiko kama hiyo.

3-  KUOMBA DUA KWA MWENGINE ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU

Mwenyezi Mungu Mtukufu amebainisha kwamba dua ni ibada, katika kauli yake:
"Na Mola wenu anasema 'Niombeni nitakujibuni. Kwa hakika wale wajivunao kufanya ibada Yangu bila shaka wataingia Jahannam wadhalilike".
Ghaafir - (Al Muumin - 60)
Na Mtume (SAW) pia alibainisha haya pale aliposema:
"Dua ndio ibada".
Imepokelewa na Ahmed na Attirmidhiy

Kwa hivyo ye yote yule atakayemuomba mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu awe ni Malaika aliyetukuzwa au Mtume aliyetumwa au Walii katika wacha Mungu au Jini katika mashetani au mtu ye yote aliye hai au aliyekufa, anakuwa ametenda kitendo cha shirki.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Na (nikaambiwa): 'Wala usiwaabudu badala ya Mwenyezi Mungu wale ambao hawakufai (unapowaabudu) wala hawakudhuru (unapowacha kuwaabudu) basi ukifanya utakuwa miongoni mwa madhalimu wa (nafsi zao).
Na kama Mwenyezi Mungu akikugusisha dhara basi hakuna ye yote awezaye kuiondoa isipokuwa Yeye (Mwenyewe). Na kama akikutakia fadhila zake (Mwenyezi Mungu) huzifikisha (fadhila hizo) kwa amtakaye katika waja wake. Naye ni Mwingi wa kusamehe (na Mwingi wa Kurehemu)".
Yunus - 106-107


Na akasema:
"Hakika wale mnaowaabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni waja (watumwa) kama nyinyi. Hebu waiteni, nao wakuitikieni ikiwa mnasema kweli".
Al Aaraf - 194
Na pia anasema:
"Sema 'Waiteni wale mnaodai (kuwa ni waungu) mkamwacha Yeye (ili akuondosheeni baa zinazokufikieni) hawataweza kukuondosheeni shari wala kubadilisha (kuwa kheri).
Hao wanaowaomba (wenyewe) wanatafuta ukaribiano na Mola wao; (hata) walio karibu sana miongoni mwao (kama Malaika) wanatumai rehema Zake na wanaogopa adhabu. Hakika adhabu ya Mola wako ni ya kuogopwa".
Israa (Bani Israil)  -56-57

4-  KUHUKUMU KWA SHERIA NYENGINE BADALA YA SHERIA YA MWENYEZI MUNGU

Atakayeiacha sheria ya Mwenyezi Mungu na kuikataa kwa ajili ya kufuata sheria iliyotungwa na binadamu au iliyopangwa na kukubaliwa na watu na ikapingana na sheria ya Mwenyezi Mungu basi anakuwa amemwabudu mwengine badala ya Mwenyezi Mungu kwa sababu kuhukumu ni ibada.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Haikuwa hukumu ila hii ya Mwenyezi Mungu, ameamrisha msimwabudu ye yote isipokuwa Yeye, hiyo ndiyo dini iliyonyooka, lakini watu wengi hawajui".
Yusuf - 40
Na kuhukumu huko (kinyume na sheria ya Mwenyezi Mungu), hugeuka kuwa ni kuhukumu kwa sheria ya shetani.
MwenyeziMungu anasema:-
"Huwaoni wale wanaodai kwamba wameamini yale yaliyoteremshwa kwako na yaliyoteremshwa kabla yako? Nao wanataka wakahukumiwe kwa njia isiyowafiki sheria; Na hali wameamrishwa kukataa njia hiyo. Na shetani anataka kuwapoteza upotofu (upotevu ) ulio mbali (na haki)".
(An - Nisaa - 60)
Na akasema Subhanahu Wataala :
"MweyeziMungu ni mlinzi wa wale walioamini. Huwatoa katika giza na kuwatia katika mwangaza. Lakini waliokufuru, walinzi wao ni mashetani. Huwatoa katika mwangaza na kuwaingiza katika giza. Hao ndio watu wa motoni humo watakaa milele".
(Al - Baqarah - 257)

5-  KUHALALISHA MAOVU NA KURIDHIKA KWA KUENEA KWAKE

Wale wanaoridhika waziwazi na (pia) wanaoridhika kwa kificho nyoyoni mwao juu ya kuenea kwa uovu, wakiuhalalisha uovu huo wanakuwa ni makafiri waliozipoteza imani zao, hata wakijigamba kuwa eti wao ni Waislamu.
Itakuwaje mtu ayakubali maovu (na maasi) na kuyapenda pamoja na kuyahalalisha kisha  ajinasibishe na Uislamu huku akiwa anaona ni halali akapenda pamoja na kuridhika kwa wanawake kutembea uchi (majiani), masokoni, na katika mikusanyiko mbali mbali ya pamoja.
Kisha aridhike kuwepo kwa mchanganyiko wa wanaume na wanawake katika sura hii huku akijistarehesha nafsi yake kwa (kutizama) yaliyo ya haramu.
Au mfano wa yule anaezitukana jamii za Kiislamu zinazojihifadhi kwa kufuata maamrisho ya Kiislamu, akawakejeli na kuwatuhumu kuwa ni watu wasiostaarabika na wasioendelea, na kuwapa kila sifa za upungufu, kisha akawa anaogopa kila wanapoelezwa watu juu ya wajibu wa kuhukumu kwa kitabu cha MwenyeziMungu Aliyetukuka, na hofu yake kubwa ni kuogopa yasije yakatoweka matamanio yake haya yaliyoharamishwa, au kupigwa vita pombe.

Kwa watu wa aina hii inasadikisha kauli ya Mtume wa MwenyeziMungu(SAW) aliposema:
<<Kila Mtume aliyeletwa na MwenyeziMungu katika umma kabla yangu, alikuwa nao (katika umma wake) Wanafunzi na Masahaba wanaoigiza mwenendo wake na kufuata amri zake. Kisha huzaa baada yao vizazi wanaosema wasiyotenda na wanatenda wasiyoamrishwa. Basi atakaepambana nao kwa mikono yake anakuwa ni mwenye Imani(Muislam wa kweli) na atakaye pambana nao kwa ulimi wake anakuwa ni Mwenye imani, na atakae pambana nao kwa moyo wake anakuwa ni Mwenye imani, na hakuna imani tena baada ya hayo hata yenye uzito wa punje ya Hardali>>.
Muslim na Ahmad na imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas

6-  KUJIGAMBA KUJUA ELIMU YA GHAIBU

Yeyote atayejigamba kuwa yeye au mwengine yeyote anajua elimu ya Ghaibu, basi atakuwa amefanya kitendo cha Shirki na cha Kufru.
MwenyeziMungu anasema:-
"Yeye ndie Mjuzi wa siri, wala hamdhihirishii yeyote siri yake isipokuwa Mtume wake aliyemridhia."
(Al - Jinn - 26 - 27)
Na akasema pia:
"Na ziko kwake (MwenyeziMungu tu) funguo za siri; hakuna azijuae ila Yeye”.
(Al - An - Am - 59)
MwenyeziMungu pia akasema kwa kumfundisha Mtume wake (SAW) aseme:
"Sema; "Sina mamlaka ya kujipa nafuu wala ya kujiondolea madhara ila apendavyo MwenyeziMungu; na lau kama ningelijua Ghaibu ningejizidishia mema mengi; Wala isingalinigusa dhara; mimi si chochote ila ni muonyaji na mtoaji wa habari njema kwa watu wanaoamini".
(Al - Aaraf - 188)

Huu ni mtihani mdogo MwenyeziMungu anawafedhehesha nao wale wanaojigamba kuwa wanajua Ghaibu, nao ni kuwataka waijue biashara yenye faida na waifanye biashara hiyo, ndipo watakapotajirika, au waelewe yale masaibu watakayopambana nayo ili wajiepushe nayo.
Wanaingia katika kundi hili wachawi na wapiga ramli kutokana na yale wanayoyafanya.
Mtume (SAW) amesema:
<<Atakayemuendea mchawi na kumsadiki ayasemayo, basi kesha yakufuru yale aliyoteremshiwa Muhammad>>.
Imetolewa na Ahmad na Al Tirmidhiy na Abu Daud na Al Nasai na Ibn Majah

Na katika baadhi chache ya habari za kweli wanazotamka wapigaji ramli na wachawi na mambo yenyewe ni nadra kutokea, huyapata kutoka kwa majini ambao huchanganya ukweli mmoja pamoja na uongo tisini na tisa.
Na wale wenye uwezo wa kuwasiliana na majini (na mashetani) ni watu wabaya kabisa.
MwenyeziMungu anasema:-
"Jee! Nikwambieni ambao mashetani wanawateremkia? Wanateremka juu ya kila mzushi mkubwa mwenye madhambi (shetani hawateremkii watu wazuri) wanawapelekea (hao wanaowafuga) yale wanayoyasikia (na wakaongeza yao ya uongo mtupu) na wengi katika hao ni waongo".
As - Shuaraa - 221 - 223

UCHAWI NA HADAA

Atakayefanya uchawi na kuomba kwa majina ya mashetani, akapiga mafundo na kuvaa au kutundika hirizi ambazo huandikwa majina ya majinni na akafanya uchawi ili mtu na mkewe wapendane au wachukiane basi anakuwa keshafanya kitendo cha kufru.
MwenyeziMungu anasema:
"Wakafuata yale waliyoyafuata mashetani (wakadai kuwa yalikuwa) katika ufalme wa (Nabii) Sulaiman; na Sulaiman hakukufuru bali mashetani ndio waliokufuru, wakiwafundisha watu uchawi (waliokuwa wakijua wenyewe tangu zamani) na (uchawi) ulioteremshwa kwa Malaika wawili, Haruta na Maruta, katika (mji wa) Babil. Wala (Malaika hao) Hawakumfundisha yeyote mpaka wamwambie hakika sisi ni mtihani (wa kutazamwa kutii kwenu); basi usikufuru. "Wakajifunza kwao ambayo kwa mambo hayo waliweza kumfarikisha mtu na mkewe (na mengineyo), wala hawakuwa wenye kumdhuru yeyote kwa hayo ila kwa idhini ya MwenyeziMungu. Na wanajifunza ambayo yatawadhuru wala hayatawafaa na kwa yakini wanajua kwamba aliyekhiari haya hatakuwa na sehemu yoyote katika akhera.
Na bila ya shaka ni kibaya kabisa walichuouzia (starehe za) nafsi zao (za akhera); laiti wangelijua (hakika wasingefanya hivi). Na lau wangeamini na kuogopa, bila ya shaka malipo yatokayo kwa MwenyeziMungu yangekuwa bora kwao. Laiti wangelijua”.
Al - Baqarah - 102- 103

Miongoni mwa mambo ya kichawi ni yale wafanyayo wenye kupandwa na jazba, wanaojipiga vichwani na kujichoma miili yao kwa mapanga na majambia, na yale wanayofanya wachawi wakaonekana kama kwamba wanatoa mawe matumboni mwa watu.
Mtume (SAW) amesema:-
<<Hayuko pamoja na sisi mwenye kupiga ramli au mwenye kupigiwa au (mwenye) kufanya uchawi au kufanyiwa au mwenye kufanya (1)Tatayyur au mwenye kufanyiwa>>.
(Imetolewa na Al - Bazaar)
(1)(Tatayyur ni kuamini kwamba baadhi ya ndege wakiruka au sauti zao zina leta madhara au nukhsi n.k.)

8-  MAKAURE, HIRIZI, KULA MICHANGA YA MAKABURINi AU KUJIPANGUSIA NAO MWILINI

Miongoni mwa ujinga, ni itikadi ya baadhi ya watu kuwa makaure yana uwezo wa kufukuza majini, wakawavisha wanyama wao au watoto wao kaure hizo. Wengine hutundika kamba na uzi au hutundika hirizi zenye majina ya majini na michoro isiyotambulika au kula michanga ya makaburi au kujipangusia miili yao michanga hiyo.
Yote hayo ni katika upotofu na ujinga ambao kila Muislamu lazima aepukane nao, maana hapana mwenye uwezo wa kudhuru au kufaa isipokuwa MwenyeziMungu tu, Subhanahu Wataala.

MwenyeziMungu amekwisha tukadiria yale yanayotudhuru tukayajua kwa akili zetu, kwa hivyo ni wajibu wetu kuziondoa kwa qudra zenye manufaa. Kwa hivyo tunaiondoa qadar ya njaa kwa qadar ya chakula na qadar ya maradhi kwa qadar ya dawa, tukishindwa basi tunamuomba Mwenye funguo za kila kitu (Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala).















MAENDELEO TULIYOYATUPA NYUMA

Mwenye kuzingatia hali za Waislamu atawaona kuwa wamekuwa ni wenye kutegemea mataifa mengine katika kuyaendesha mambo yao ya kidunia kama vile viwanda, ukulima, biashara na ujuzi wa kifundi.
Nini basi sababu za kuwa nyuma katika mambo haya ya Kidunia, bali hata katika mambo ya Kidini?
Baada ya kudhoofika kwa Imani ndani ya nafsi zetu, na kudhoofika uhusiano wetu na Mwenyezi Mungu, na kudhoofika tabia na mwenendo, ndipo ufisadi ukaanza kuenea kidogo kidogo hata vikapatikana vizazi vilivyoipoteza Sala na kufuata matamanio, Dhulma ikaenea baina ya watu na dhambi kuongezeka, ukaanza mvutano baina ya Waislamu, ujinga katika mambo ya kidini na kidunia ukaenea, uzushi katika mambo ya dini ukaongezeka pamoja na Ushirikina.
Waislamu wakaupoteza umoja wao na undugu wao, na kwa ajili hiyo nguvu zao zikatoweka, wakaanza kuanguka na kubadilika hali zao kutoka katika hali mbaya kuelekea katika hali mbaya zaidi.

UKOLONI UMEZAMISHA MIZIZI YA OPOTOFU (UPOTEVU) NA SISI TUKAKUBALI

Ikiwa Mwenyezi Mungu anasema:-
"Na Mwenyezi Mungu hatawajaalia makafiri njia ya kuwashinda Waislamu".
(An - Nisaa -141)
Kwa hivyo Waislamu baada ya kuipoteza imani iliyo sahihi na kuchukua nafasi yake ushirikina na Bid- aa, (uzushi wa mambo yasiyo na asili katika dini) isipokuwa kwa wale wachache aliowarehemu Mola wao,  Waislamu wakawa katika hali ya kuanza kuikubali sheria ya makafiri waliofanya juhudi kubwa ya kupiga vita kila kinachowaamsha Waislamu katika mambo yanayohusiana na Dini yao na ya kidunia.
Na kutokana na udhaifu wa imani, wakapatikana miongoni mwetu waliozikubali mbinu za makafiri, bali na kuwasaidia katika kufanikiwa kwa mbinu hizo dhidi ya Waislamu.

SABABU ZA MAENDELEO YA KIDINI NA YA KIDUNIA

Sababu zitakazo waendeleza mbele Waislamu katika dini yao ni kuizamisha imani katika nafsi zao, kuzidisha nguvu mawasiliano yao na Mola wao, kuzitakasa ibada zao ili ziwe halisi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, kufuata sheria zake, kufuata mwenendo wa Kiislamu pamoja na kuwalea watoto katika njia hizo zote.
Iwapo watatekeleza hayo, basi neno lao litakuwa moja, nguvu zao kuongezeka na Mwenyezi Mungu atawanusuru na adui zao.
Na sababu zitakazosababisha kunyanyuka hali zao katika mambo ya kidunia ni kuutumia uchumi na kheri aliyowapa Mwenyezi Mungu katika ardhi zao, kwa njia zilizo bora.

Ili Waislamu wafanikiwe katika mambo haya, zipo njia nyingi zinazohitajika kufuatwa, miongoni mwa njia hizo ni;
1-  Kupatikana kwa wataalamu wenye ujuzi na wafanyakazi waliopata mafunzo sawa sawa. 
2-  Kupatikana kwa mali pamoja na mali asili.
3- Kueneza viwanda pamoja na kutafuta masoko ya kununua bidhaa zitakazopatikana katika viwanda hivyo.
4-  Kuwepo kwa nidhamu yenye uadilifu itakayowapa moyo wafanyakazi ili waongeze juhudi, pamoja na kuwepo kwa nidhamu yenye uwezo wa kuzuwia dhulma na uvukaji mipaka (katika maonevu).

Bila shaka sababu hizi ni katika mema ambayo dini yetu inayatilia mkazo yafuatwe na kushirikiana kwa ajili ya kuyafikilia, maana haya ni katika mambo muhimu tunayoyahitajia sana. Ama sivyo siku zote Waislam watakuwa wakitegemea misaada kutoka katika nchi zisizokuwa za Kiislam,  na siku zote watadhalilika mbele yao.
Mwenyezi Mungu anasema:-
"Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika dini."
(A l - Hajj - 78)
Mwenyezi Mungu ametuamrisha kushirikiana katika mema yaliyo kama haya na mengineyo na ametukataza kushirikiana katika dhambi na uadui wa kila aina.
Mwenyezi Mungu anasema:-
"Na saidianeni katika wema na ucha Mungu na wala msisaidiane katika dhambi na uadui. Na mcheni Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni mkali wa kuadhibu."
(Al - Maidah - 2)

Ikiwa kila mtu atatoa mchango wa Shilingi mia kila mwezi, basi tunaweza kujenga kitivo cha Sheria au cha Uhandisi au cha Madawa (Pharmacology) au cha Sayansi au cha Ukulima au cha Tiba.
Na kutokana na vitivo hivi tutaweza kuutambua uwezo wetu na kufaidika nao na wakati huo huo tutaweza kupata waalimu wa kuwafundisha wenzao.
Ikiwa kila mtu ataweza kulipa shilingi mia tu, basi tutaweza kusimamisha mashirika au viwanda vitakavyofaa katika maendeleo yetu, itakuwaje basi ikiwa kila mwenye uwezo zaidi, atatoa kiasi cha uwezo wake?
Na kwa njia hii tutaifupisha njia ya kupata maendeleo ya kidunia na kupata mafanikio katika miaka michache tu.

Mwenyezi Mungu  amezijaalia nchi za Kiislamu kuwa na utajiri mkubwa, lakini kwa udhaifu wetu tumeshindwa kunufaika na kheri hizi sisi wenyewe isipokuwa tuwe chini ya watu wengine wasiokuwa Waislamu.

WAKOLONI WAMEZIPIGA VITA NJIA ZOTE AMBAZO ZINGEWAFANYA WAISLAMU WAPATE MAENDELEO

Nchi nyingi za Kiislamu na kwa miaka mingi zilikuwa chini ya utawala wa makafiri walioitumia kila fursa wanayoipata katika kuipiga vita dini ya Kiislamu.
Wakaipiga vita dini hii katika sehemu mbali mbali, kama vile:-
1-  Kuifuta sheria ya Kiislamu isitumike katika nchi za Kiislamu.
2-  Kupiga vita masomo ya dini katika skuli na vyuo vikuu.
3-  Kuwapiga vita Maulamaa wa Kiislamu wanaoifanyia kazi dini yao.
4- Kuanzisha vyama vya siasa visivyoamini Mungu na vinavyopiga vita dini.
5- Kutilia mkazo mambo ya Uzushi katika dini (Bida a) pamoja na Imani za kijinga na za ushirikina na kuifanyia biashara dini.
6- Kuwafisidi wanawake pamoja na kuufisidi ukoo na kuwaacha wanawake watembee uchi pamoja na kuufisidi mwenendo wa Waislam.
7-  Kutafuta kila njia ili kuleta kutokuelewana na kufarikiana pamoja na uadui baina ya Waislamu.

Mwenyezi Mungu amekwisha tutahadharisha juu ya kuwatii Ahli - lkitab (Wakristo na Mayahudi) aliposema:
"Enyi mlioamini! Mkiwatii baadhi ya wale waliopewa kitabu, watakurudisheni kuwa makafiri baada ya Uislamu wenu."
(Al - Imran - 100)

Ama kuhusu makafiri kuipiga vita nguvu ya Waislamu, yafuatayo ni katika mambo muhimu walioyafanya:
1-  Kuweka mipaka ya kuwatenganisha Waislamu.
2-  Kuutawala uchumi wa Waislamu.
3- Kufanikiwa kupata vizazi miongoni mwa Waislamu, wale waliolelewa na kufunzwa katika mikono ya makafiri na wale wataalamu wa mambo ya Bara la Asia (Orientalist) na kuweza kuwadanganya kwamba Waislam hawatoweza kuendelea ila baada ya kuipiga vita dini yao na kumfisidi mwanamke kwa kutumia mwito wa “Haki za kinamama”, ili aufisidi mwenendo wake pamoja na fadhila zake na heshima yake na pia kwa njia ya kuruhusu ulevi, uzinzi na kuipiga vita sheria ya Mweneyzi Mungu na kuibadilisha kwa kanuni za wanaadamu.

Wakoloni hawa badala ya kufanya kazi ya kueneza viwanda, mashirika, vyuo na vyuo vikuu  na maabara,  wakafanya kazi ya kuwapiga vita Waislam katika Itikadi zao, heshima zao, sheria ya dini yao pamoja na mwenendo wao, hata ukafika wakati mtu anayesali anaonekana mbele yao kama mtu asiye endelea, yuko nyuma, na kuacha Sala ndio maendeleo.
Na mwanamke anayejihifadhi, huwa hakuendelea, yuko nyuma, na yula alie fasiqi muhuni ndiye aliyeendelea.
Yule anayeilinda akili yake na mwili wake kutokana na ulevi nae pia hakuendelea, yuko nyuma, lakini mlevi ndiye aliyeendelea na yuko huru.
Viko wapi viwanda? Yako wapi mashirika? Yako wapi maabara?
Wakoloni na wanafunzi wao wametupotosha mbali na njia iliyo sawa ya kutaka kuendelea vilivyo sahihi.

MAADUI WA WAISLAMU WAMEWAFANYA WAISLAMU DAIMA WAWE WANAWATEGEMEA WAO NA KUVITEGEMEA VIWANDA VYAO NA MAZAO YAO

Na ni juu yetu pia kufahamu kwamba maendeleo yaliyopatikana katika nchi za kikafiri hayakupatikana kwa sababu ya kukufuru kwao, kwani kufru imeanza zamani sana hata kabla ya kudhihiri Uislamu, na kufru yao hiyo haikuwapatia hapo zamani ndege wala roketi wala umeme wala cho chote kile. Lakini kuendelea kwao kidunia kumepatikana kwa sababu wamefuata njia (na sababu) zilizowafikisha katika neema ambazo Mwenyezi Mungu amewatandazia viumbe vyake.
Mwenyezi Mungu anasema:-
"Wote hawa (wema na wabaya) tunawapa hawa na hawa - katika atiya (zawadi) za Mola wako;  na atiya za Mola wako hazizuiliki (kumfikia kiumbe chake)".
(Bani Israil – (Israa) - 20)
Kwa hivyo wakapata atiya ya Mwenyezi Mungu na sisi tukakosa kwa sababu tulikuwa wavivu.

NJIA YA KUFUZU

Siku Waislamu watakaposhikamana na Dini yao kama inavyotakikana, hapo ndipo utukufu wao utakaporudi na ndipo Mwenyezi Mungu atakapowanusuru kutokana na adui zao, na hapo itakuwa wepesi kwao kupata mafanikio katika Dini na dunia yao.
<<Mola wetu! usizipotoe nyoyo zetu baada ya kuziongoza na utupe rehma itokayo kwako; hakika Wewe ndiwe Mpaji mkuu>>.
Wasalamun Alal Mursalina  Walhamdu lillahi Rabbi L –aalamin.

KIMEANDIKWA NA SHEIKH ABDUL MAJEED AL ZINDANI
KIMEFASIRIWA NA MUHAMMAD FARAJ SALEM AL SAIY




[1]
Huenda pia kukaribiana kwa wakati ikawa ule urahisi wa kazi. Kwa mfano kazi iliyokuwa ikifanywa siku nzima hapo zamani hivi sasa inafanyika katika dakika chache tu, au kazi iliyokuwa ikichukua miaka hapo zamani, hivi sasa baada ya kuletwa makopyuta na vyombo vingine vya kisasa huchukua masaa machache tu pamoja na safari zilizokuwa zikichukua miezi mingi hapo zamani hivi sasa zinachukua masaa machache tu.


[2] MAHAMID = Muhammad kabla ya kupitiwa na mikono ya watu (kubadilishwa)
[3] MWALIMU WA ULIMWENGU = Mtume wa ulimwengu
[4] TANO ZILIZO TAHIRI = Sala tano
[5]Yamenukuliwa kutoka kwenye kitabu kiitwacho "Mawimbi yaliyofichika katika dini za kale za Wahindi”, kilichoandikwa na T. Muhammad
[6] "ILA KWA HAKI YA UISLAMU" = Zile hukumu za kisheria za Kiislamu zilizowajibika kusimamishiwa Muislamu yeyote anapouwa, anapozini, anapoiba au hukumu nyenginezo.

[7] Makhalifa walioongoka (AL RASHIDYN) ni:- Abubakar, Omar, Othman na Aliy(RAnhum).
Makhalifa hao pia wameoleana na Mtume (SAW) -
Aisha (Umu I Muuminina)(RA)  Mke wa Mtume(SAW),  ni binti wa Abu Bakar Al Siddique(RA).
Hafsa(RA) - Mke wa Mtume (SAW), ni binti wa Omar (RA)
Ruqayyah(RA) - Binti wa Mtume(SAW), alimwozesha Othman(RA) na alipokufa bibi Ruqayyah(RA) Mtume (SAW) akamwozesha Othman(RA) binti yake wa pili - Ummu Kulthum(RA), na ndio maana Othman(RA) alikuwa akijulikana kwa sifa ya "Dhu Nnurayn" – Mwenye Nuru mbili -, na hii ni kwa sababu ya kuoa mabinti wawili wa Mtume(SAW).
Mtume (SAW) akamwozesha Aliy bin Abi Talib (RA) binti yake Fatma(RA) "Bibi wa kina mama Peponi".
Aliy bin Abu Talib(RA) pia alimwozesha Omar bin Al Khatab(RA) binti yake Ummu Kulthum(RA) mwana wa Fatma(RA).
Makhalifa Al Rashidyni hawa walikuwa mawaziri wa Mtume (SAW) na alikuwa akishauriana nao sana katika mambo yaliyo muhimu nao pia walikuwa miongoni mwa Waislamu wa mwanzo wa Makka.
Na mwanzo wao kusilimu ni Aliy bin Abi Talib baadaye Abu Bakar, akafuatilia Othman kisha Omar(R Anahum Jamiy-an).
Zipo hadithi nyingi za Mtume (SAW) zinazoelezea ubora wao kupita Masahaba wengine wote walio wema.
[8] Katika sharhi ya hadithi hii, maulamaa wanasema kuwa pale Mtume(SAW) alipotamka;
‘Wala hawaadhibiwi kwa makubwa’ alikusudia kuwa watu hao walikuwa wakidhani kuwa madhambi yale si makubwa.
Kisha akasema; ‘Bali hivyo’, kwa lugha ya kiarabu alitamka; ’Balaa’ na hii maana yake ni kukanusha kuwa; si kama walivyokuwa wakifiria wao, bali madhambi hayo yalikuwa makubwa.

[9] Hadithi hii kwa ukamilifu ni kama ifuatavyo :
<<Mwenyezi Mungu anamlani kila anayechinja kwa ajili ya mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu anamlani kila anayewalani wazazi wake, na Mwenyezi Mungu anamlani kila anayemnusuru mwenye kuleta uzushi (katika dini), na Mwenyezi Mungu anamlani kila anayesogeza mipaka (kwa ajili ya kuiba ardhi ya mwenzake>>.
(Imetolewa na Muslim katika "Sahih" yake, Ahmad katika "Musnad" yake na An Nasai katika "Sunan" yake.)